Makala

UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Viambajengo vikuu katika nadharia ya Ufeministi

February 27th, 2019 1 min read

Na MARY WANGARI

NADHARIA ya ufeministi inanuia kuwasawazisha wanadamu kwa upande wa jinsia na utamaduni na kupigania jamii mpya yenye msingi katika amali za kibinadamu na wala si za kimaumbile na za kijadi.

Ni mtazamo unaokuza na kuendeleza hisia za umoja wa wanawake kama kundi linalodhulumiwa.

Aidha, lengo muhimu la nadharia hii ni kuvumbua na kuziweka wazi kazi za sanaa zilizotungwa na wanawake ambazo zimepuuzwa kwa sababu ya utamaduni unaompendelea mwanamume.

Pia inanuia kuchunguza historia ya fasihi ya jadi ya kike na kuwamulika waandishi wa kike waliotambua hali za wanawake na ambao wanaweza kuchukuliwa kama vielelezo kwa wasomaji wao.

Kama anavyosema Mbatiah, lengo kuu la uhakiki wa kifeministi na hasa Ufeministi wa Kiafrika ni kuzua mikakati ambayo itaangazia kutathmini jinsia ya kike, mitazamo, thamani na matakwa ya wanawake – sio tu katika fasihi, bali nyanja zote za maisha ya binadamu.

Nadharia hii hunuia kuzindua mwamko kwa wanawake na jinsi wanavyojiona na uhusiano wao na watu wengine.

Baruapepe ya mwandishi: [email protected]

Marejeo

Wamitila, K. W. (2003). Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus.

Wa Thiong’o, Ngugi (1998). Penpoints Gunpoints and Dreams. Oxford: Clarendon.

Wellek Rene & Austin Warren ( 1986). Theory of Literature. Harmondworth: Penguin