MakalaMichezo

Shakers FC mjini Thika ni kiwanda cha kupika vipaji

February 27th, 2019 Kusoma ni dakika: 2

Na LAWRENCE ONGARO
 
UNAPOFIKA katika Uwanja wa Kanisa la Redeemed Church, Makongeni, Thika, majira ya saa 3 hadi saa 5 za asubuhi utampata kocha Harub Swaleh wa timu chipukizi ya Thika Shakers FC, akiendesha mazoezi kwa vijana wake.
Anasema kikosi hicho ni cha vijana chipukizi wenye umri wa miaka kati ya tisa hadi miaka 15 ambao wanatoka eneo la Makongeni na vitongoji vyake.
“Kikosi hiki nilikibuni mwaka wa 2018 ambapo nimeweza kusajili vijana wapatao 40. Vijana wengi wamekubaliwa na wazazi wao kujiunga na kikosi hicho,” alisema Kocha Swaleh
Anasema kila  mchezaji hujiunga na timu hiyo akiwa hana ujuzi wowote wa kutembeza boli, lakini baada ya kupitia mikononi mwake wao hubadilika na kuwa wachezaji stadi kwelikweli.
Kocha wa Thika Shakers FC Harub Swaleh na baadhi ya wachezaji wa timu hiyo. Picha/ Lawrence Ongaro
Anasena kwa siku za hivi karibuni amepitia changamoto tele kwa sababu wakati fulani wazazi wamekuwa wakiwakataza watoto wao kufika uwanjani kwa mazoezi, lakini hivi majuzi waliridhika na kazi ambayo anafanya baada ya wao kufika uwanjani na kujionea kazi yake.
“Wazazi hao sasa wanafurahia kazi kubwa ninayotekeleza ambapo hata wengi wao huwaleta watoto wao uwanjani wenyewe. Hii ni ishara kwamba kazi yangu inaonekana kuwa bora,” alisema Kocha Swaleh.
Hivi majuzi vijana hao wa Thika Shakers walicheza mechi ya kirafiki na Delmonte ambapo walilazimika kutoka sare ya 1-1.
Kushindwa
Timu hiyo pia iliweza kucheza na Destiny FC ambapo walipoteza kwa kushindwa mabao 2-0.
“Mimi kama kocha nitafanya juhudi kuona ya kwamba nimeiweka timu hiyo imara licha ya kupitia pandashuka tele za hapa na pale. Hata hivyo wazazi wa vijana hao wamekuwa wakinipa sapoti kubwa na hiyo ndiyo imenifanya  nizidi kuendelea hadi sasa,” anasema Kocha Swaleh.
Anasema licha ya kuwa pekee katika kibarua hicho anazidi kutafuta  wafadhili ambao wanaweza kumpa ufadhili zaidi ili aweze kufanikisha ndoto yake ya kuinua vijana mitaani na kuwaweka katika kiwango kingine.
“Nitazidi kujitolea kuona ya kwamba nimewanoa vijana hao ambao wameonyesha matumaini makubwa ya kupiga hatua zaidi katika soka,” asema Swaleh.
Kocha huyo anasema lengo lake ni kuona ya kwamba anataka kuwaweka vijana hao kuwa kitu kimoja kama familia  moja ili kucheza soka  inayotamanika na wengi.
“Vijana wadogo kama hawa wanastahili kuonyeshwa nidhamu ili kukuza  hali yao ya kujiendeleza kwa kucheza soka. Hii inahitaji ushirikiano mwema na kuwa mnyenyekevu kwao ili kuwapa matumaini,” alisema Swaleh.
Baadhi ya wachezaji ambao wanakipa kikosi hicho matumaini ya kuendelea mbele ni Treva Mbugua, Jimmy Lewis, Samuel Ndeti, na Alvin Karani. Wengine ni Arafat Harub, Frank Njuguna Brian Kinyanjui, na Onel Njoroge. Pia kuna David Awuor, Fesal Harub na Paul Clement.
Anawahimiza wazazi kuwapeleka wana wao kujiunga na kikosi hicho kwani watatoka na jambo la kujivunia na pia vijana hao watakuwa wa kutegemewa na jamii siku zijazo.