Lugha, Fasihi na Elimu

LUGHA: Makosa ya kutotumia upatanisho sahihi wa kisarufi katika sentensi

Na HELLEN NJAGI May 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

TUNAPOTUNGA sentensi sharti tuzingatie upatanisho wa kisarufi ili sentensi ziwe sahihi.

Upatanisho wa kisarufi katika sentensi hutokana na jinsi nomino huathiri vitenzi katika sentensi. Kila kundi la nomino huwa na viambishi vyake vya upatanisho wa kisarufi.

Watu wengi wanaowasiliana kwa lugha ya Kiswahili hasa wanafunzi huzingatia upatanisho sahihi wa kisarufi wanapotunga sentensi, japo baadhi yao hukumbwa na changamoto.

Utapata sentensi kama vile:

* Nchi nyingi barani Afrika wanahimiza umoja na amani.

* Vyombo vya habari wapeperusha taarifa kuhusu wahalifu waliokamatwa jana.

* Jamii yetu wanazingatia maadili.

Mifano hii ya sentensi imetumia viambishi vya upatanisho wa kisarufi visivyofaa.

Kosa hilo hasa linatokana na kukosa kuzingatia kiambishi ngeli cha nomino iliyotumiwa kutunga sentensi.

Katika sentensi ya kwanza, kiambishi wa- kimetumiwa kuwakilisha nomino nchi.

Hili ni kosa kwani ingawa nchi zina watu ambao ndio wanahimiza umoja na amani, nomino iliyotumiwa kutunga sentensi ni nchi, kwa hivyo tunafaa kutumia kiwakilishi ngeli cha nomino nchi si nomino watu.

Ili kusahihisha sentensi hizo tunafaa kusema: Nchi nyingi barani Afrika zinahimiza umoja na amani.

Vyombo vya habari vipeperusha taarifa kuhusu wahalifu waliokamatwa na polisi jana. Jamii yetu inazingatia maadili.

Mwanafunzi anayekumbwa na changamoto ya kutotumia viambishi sahihi vya upatanisho wa kisarufi katika sentensi, afanye mazoezi ya kutambua nomino katika ngeli mbalimbali.

Atambue viambishi sahihi vya upatanisho wa kisarufi katika kila ngeli kisha atumie nomino katika ngeli mbalimbali kutunga sentensi zenye upatanisho sahihi wa kisarufi.