ODM kujipima nguvu kwa mara ya kwanza bila Raila
CHAMA cha Orange Democratic Movement kimeanzisha mikakati ya ndani ya kujitathmini kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027 huku kukiwa na wasiwasi kuhusu mustakabali wake bila kiongozi wake wa muda mrefu Raila Odinga, kugombea urais.
ODM sasa imewaalika wanachama wanaotaka kuwania nyadhifa mbalimbali kupitia tiketi ya chama hicho kuwasilisha maombi yao katika hatua ambayo viongozi wa ndani wanasema inalenga kupima nguvu na udhaifu wa chama katika maeneo mbalimbali nchini.
Kupitia zoezi hilo, ODM inalenga kubaini maeneo ambayo bado ina ushawishi mkubwa kisiasa na yale ambayo huenda yanaanza kuitema baada ya Bw Odinga.
Katika tangazo lililochapishwa kwenye magazeti ya humu nchini, ODM imewaalika wanaotaka kuwania urais, ugavana, useneta, wawakilishi wa kike, ubunge na wawakilishi wa wadi kuwasilisha maombi yao kabla ya Juni 30.
Tofauti na chama cha United Democratic Alliance cha Rais William Ruto pamoja na chama cha Democracy for the Citizens Party kinachohusishwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ambavyo vinatoza hadi Sh50,000 kwa usajili wa wagombeaji, ODM haitaki ada yoyote.
“Lengo letu ni kujua maeneo tulio na nguvu kisiasa. Orodha ya wanaotuma maombi itatusaidia kupanga mikakati ya uchaguzi wa 2027,” afisa mmoja wa ODM alisema.
Kwa miaka mingi, ODM imekuwa ikitegemea ngome zake za kisiasa katika maeneo ya Nyanza, Magharibi, Pwani, Turkana, sehemu za Kaskazini Mashariki na jamii ya Wamaasai.
Hata hivyo, viongozi wa chama wana hofu kuwa hali inaweza kubadilika 2027 kwa kuwa Bw Odinga hayupo kwenye kinyang’anyiro cha urais.
Wakati huo huo, ODM inakabiliwa na mgawanyiko wa ndani kuhusu iwapo inafaa kumuunga mkono Rais Ruto katika uchaguzi wa 2027.
Mgawanyiko huo umezaa makundi mawili yanayoshindana ndani ya chama, moja likiongozwa na kinara wa chama Oburu Oginga chini ya kaulimbiu ya Linda Mwananchi na lingine likihusishwa na Katibu Mkuu Edwin Sifuna.
Lengo la mkakati mpya wa ODM ni kurejesha imani ya wanachama katika mchakato wa uteuzi wa wagombeaji ambao kwa miaka kadhaa umekumbwa na lawama za wizi wa kura na utoaji wa tiketi za moja kwa moja.
Katika kikao cha chama kilichofanyika Mombasa hivi majuzi, ODM iliagiza Kamati ya Kitaifa ya Kuratibu Uchaguzi (NECC) kuweka mifumo itakayohakikisha haki na uwazi katika kura za mchujo.
Chama hicho pia kilikataza utoaji wa tiketi za moja kwa moja.
“Tumeagiza kamati ya uchaguzi kubuni mifumo madhubuti ya kuhakikisha kura za mchujo zinafanyika kwa njia ya haki, uwazi na uaminifu,” chama kilisema.
Ripoti ya ndani ya ODM ya mwaka 2023 ilibaini kuwa mfumo wa kidijitali uliotumika katika kura za mchujo za 2022 ulikuwa na mianya iliyowezesha udanganyifu.
Ripoti hiyo ilionyesha kuwa baadhi ya vifaa vya kupigia kura havikuwa na mfumo wa kuzuia wizi wa kura huku baadhi ya wagombeaji wakidaiwa kushirikiana na maafisa wa uchaguzi kuvuruga mfumo huo.
Mwenyekiti wa Kitaifa wa ODM, Gladys Wanga, alikiri kuwa kura za mchujo zimekuwa tatizo kubwa kwa chama hicho.
“Timu ya uchaguzi imepewa maagizo madhubuti kuhakikisha kuna mfumo unaoaminika na unaowapa wagombeaji nafasi sawa,” Bi Wanga alisema.
Mbunge wa Uriri Mark Nyamita, alisema ufanisi wa ODM mnamo 2027 utategemea uwezo wake wa kuendesha kura za mchujo za haki.
“Tumaini pekee la ODM mwaka wa 2027 ni kura za mchujo zilizo huru, za haki na za kuaminika,” alisema Bw Nyamita.