Habari za Kitaifa

IEBC yasema imepungukiwa na Sh33 bilioni kwa uchaguzi wa 2027

Na EDWIN MUTAI May 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imesema inakabiliwa na upungufu wa Sh33 bilioni katika maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2027 baada ya kuongeza makadirio ya bajeti yake kwa Sh13.1 bilioni, hali iliyowafanya wabunge kuhoji kwa nini makadirio hayo yanaendelea kubadilika.

Naibu Afisa Mkuu Mtendaji wa IEBC Obadiah Keittany aliambia Kamati ya Bunge kuhusu Haki na Sheria kuwa tume hiyo inahitaji jumla ya Sh74.8 bilioni kufanikisha uchaguzi mkuu, lakini imetengewa Sh41.3 bilioni pekee katika mwaka wa kifedha wa 2026/27.

Keittany alisema kuna pengo la fedha la Sh33.4 bilioni kwa maandalizi ya uchaguzi wa mwaka ujao.

Alieleza kuwa katika bajeti ya mwaka wa kifedha wa 2025/26, IEBC ilikuwa imeomba Sh61.74 bilioni kwa uchaguzi huo, fedha zilizopaswa kutolewa katika miaka mitatu ya kifedha ya 2025/26, 2026/27 na 2027/28.

Akijitetea mbele ya Kamati ya Bunge, Keittany aliwaomba wabunge kuongeza bajeti hiyo ili kuhakikisha uchaguzi unaendeshwa bila matatizo.

IEBC ilisema imeongeza bajeti kutokana na matarajio ya ongezeko la wapigakura waliosajiliwa kutoka milioni 22.1 mwaka 2022 hadi milioni 28.5 mwaka 2027.

Tume hiyo pia ilieleza kuwa, vituo vya kupigia kura vinatarajiwa kuongezeka kutoka 46,000 hadi 55,000.

Kamishna wa IEBC Profesa Francis Aduol alisema tume inapanga kubadilisha vifaa vyote 45,000 vya KIEMS vilivyotumika katika uchaguzi wa 2022 kwa sababu vimepitwa na wakati.

“Vifaa hivyo vimezeeka na tunasubiri ripoti ya ukaguzi kutoka kwa wataalamu wa Mamlaka ya ICT kabla ya kufanya uamuzi wa mwisho,” alisema Prof Aduol.

Aliongeza kuwa, kuna vifaa vingine 14,000 vilivyonunuliwa kutoka kampuni ya Smartmatic mnamo 2022, lakini vilikumbwa na matatizo ya kuunganishwa na vifaa vya zamani wakati wa uchaguzi uliopita.

“Tunaweza kuvitumia, lakini hatutaki kuhatarisha mfumo siku ya uchaguzi,” alisema.