Habari

Kanja, NPSC motoni kwa kufurusha makurutu wajawazito Kiganjo

May 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAPAMBANO ya kisheria yameibuka kufuatia kufurushwa kwa makurutu 18 wa kike wa polisi kutoka Chuo cha Kitaifa cha Polisi cha Kiganjo kwa sababu ya ujauzito, hatua inayozua mjadala mkubwa wa kikatiba kuhusu usawa wa kijinsia, haki za uzazi na sheria za uajiri katika sekta ya usalama.
Wanaharakati wawili wa haki za binadamu wameenda mahakamani kupinga hatua hiyo wakidai serikali imekiuka Katiba kwa kuwabagua wanawake na kuvunja haki za uzazi.
Makurutu hao walijiunga na chuo hicho baada ya zoezi la kitaifa la kuajiri polisi Novemba 2025 lililoajiri takriban askari 10,000.
Hata hivyo, wiki chache baada ya kuripoti katika chuo cha mafunzo cha Kiganjo, Kaunti ya Nyeri, wanawake hao waliondolewa kwenye Kozi ya Msingi ya Mafunzo ya Polisi kufuatia vipimo vya lazima kutambua ujauzito.
Habari hizo zilitolewa mapema Mei baada ya Kamanda wa Chuo cha Kitaifa cha Polisi, Gideon Munga Nyale, kutangaza kutimuliwa kwao wakati wa ziara rasmi ya Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen katika chuo hicho mnamo Mei 7, 2026.
Katika taarifa yake, kamanda huyo alisema wanafunzi 54 walitimuliwa, wakiwemo 18 kutokana na ujauzito.
Wengine walifukuzwa kwa sababu ya vyeti vya kughushi, rekodi za uhalifu, matatizo ya kiafya na makosa ya kinidhamu.
Sasa walalamishi wawili, Peter Agoro na John Wangai, wakisema wanatetea maslahi ya umma, wanataka Mahakama ya Ajira na Mahusiano ya Kazi kutangaza kufukuzwa huko kuwa kinyume cha Katiba, kibaguzi na kusiko halali.
Walioshtakiwa ni Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja, Tume ya Huduma ya Polisi ya Kitaifa (NPSC) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Walalamishi hao wanadai kuwa wanawake hao walifukuzwa kazini kwa sababu tu walikuwa wajawazito, licha ya serikali kukiri hadharani kwamba hakuna aliyepata ujauzito akiwa ndani ya chuo hicho.
“Wanafunzi wa kike walioathiriwa walikuwa tayari wajawazito kabla ya kuripoti chuoni,”wanasema katika kesi yao.
Walalamishi wanasema wanawake hao tayari walikuwa wamepata barua za ajira na walikuwa na matarajio halali ya kuajiriwa baada ya kufaulu hatua zote za mchakato wa kuajiri.
Wanadai kufukuzwa huko kulikiuka haki za kikatiba kuhusu usawa, utu, haki za wafanyakazi, afya ya uzazi na haki ya kushughulikiwa kwa haki katika maamuzi ya kiutawala.
Lakini Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) imetetea hatua hiyo.
Kupitia msemaji wake Muchiri Nyaga, NPS ilisema wanawake hao waliondolewa kwa mujibu wa sheria za mafunzo makali ya polisi.
“Mafunzo haya yanahusisha mazoezi magumu, kupita vizuizi na mafunzo ya silaha, hali ambazo zinaweza kuhatarisha maisha ya mwanafunzi mjamzito na mtoto ambaye hajazaliwa,” alisema.
Bw Nyaga alisisitiza kuwa hatua hiyo haikuwa adhabu kwa utovu wa nidhamu bali “utaratibu wa kawaida wa kiutawala unaolenga kulinda afya ya mama na mtoto”.