Khalwale azindua chama, asema analenga wanasiasa watakaopoteza makao vyama vikubwa
SENETA wa Kakamega, Dkt Boni Khalwale amesema kuwa amesajili chama kipya ambacho kitawapa makao wanasiasa waasi wa vyama vikubwa nchini.
Kwenye mahojiano na Taifa Leo, Dkt Khalwale alithibitisha kuwa amekisajili chama cha UPM na mipango inaendelea ya kukizindua rasmi.
Rekodi katika Afisi ya Msajili wa Vyama inaonyesha kuwa chama hicho kimetimiza matakwa yote ya kusajiliwa.
Kati ya vigogo ambao UPM inatarajiwa kuvutia ni wanasiasa wa Linda Mwananchi ambao wamekosana na ODM.
Pia wapo wanasiasa wa DAP-K inayoongozwa na Waziri wa zamani Eugene Wamalwa, chama tawala cha UDA na pia Ford Kenya ambayo kiongozi wake ni Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetangúla.
Zikiwa zimesalia chini ya miezi 13 kabla ya uchaguzi mkuu, baadhi ya viongozi waliochaguliwa katika vyama mbalimbali vya kisiasa wameonyesha nia ya kuungana na vyama vingine.
“UPM ni chama cha kitaifa kitakachowakusanya viongozi mashuhuri wa kisiasa nchini wanaounga mkono ajenda ya kumwondoa Rais Ruto uongozini. Hiki ndicho chama cha baadaye, si kwa eneo la Magharibi pekee bali kitaifa. Ndiyo maana naweza kuthibitisha kuwa ninahusishwa nacho,” akasema seneta huyo.
Ingawa hivyo, alikataa kueleza iwapo Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna na wanasiasa wengine kadhaa wa ODM watajiunga na UPM.
“Mawasiliano rasmi kuhusu suala hili yatatolewa katika wiki chache zijazo, lakini matarajio yetu yanafuata ratiba na mwongozo uliowekwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC),” akaongeza.
Mnamo Jumapili Gavana wa Trans Nzoia, George Natembeya ambaye yuko kambi moja na Dkt Khalwale na Bw Sifuna, alifichua mpango wa baadhi ya viongozi kutoka Magharibi mwa nchi kuunda chama kipya cha kisiasa.
Bw Natembeya anayehudumu muhula wa kwanza alisema kuwa chama hicho kipya kitazinduliwa wiki tatu zijazo na kitawajumuisha wanasiasa wakuu akiwemo Bw Sifuna na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi.