Babu, Murango mbele kwa uchapakazi, utafiti wa Infotrak wasema
WANASIASA kadhaa wanaowania ugavana katika uchaguzi mkuu wa 2027 wameibuka miongoni mwa viongozi waliopewa alama za juu zaidi katika utafiti mpya wa kitaifa uliofanywa na shirika la Infotrak.
Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino anaongoza orodha ya wabunge kisha Seneta wa Kirinyaga, Kamau Murango akawa mbele miongoni mwa maseneta.
Waliohojiwa walisema matumizi mazuri ya fedha za Hazina ya Kitaifa ya Ustawi wa Maeneobunge (NG-CDF), uwepo wa viongozi hao mashinani na kushiriki mijadala bungeni ndiyo sababu kuu zilizowafanya wawape alama za juu.
Wabunge walioongoza walitumia vizuri fedha za NG-CDF kwa kutoa ufadhili wa masomo kupitia basari na kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika maeneo yao.
Pia, kuwasilisha miswada bungeni, kushiriki mijadala ya sheria, kusimamia miradi ya serikali ya kitaifa na kuwajibu wapigakura kwa haraka kulitajwa kuwa mambo muhimu yaliyowapa viongozi hao alama za juu.
Uchambuzi wa matokeo unaonyesha kuwa wengi wa viongozi waliopata alama za juu ni wale waliotangaza nia ya kugombea ugavana mwaka 2027.
Bw Owino, ambaye ametangaza nia ya kuwania ugavana wa Nairobi, aliongoza kwa asilimia 80 za uungwaji mkono.
Alifuatwa na Mbunge wa Kabuchai Joseph Kalasinga aliyepata asilimia 78, huku Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro na mwenzake wa Taveta John Okano Bwire wote wakishikilia nafasi ya tatu kwa asilimia 76.
Mbunge wa Samburu Magharibi Naisula Lesuuda, Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa, ambaye pia anawania ugavana wa Bungoma, pamoja na Reuben Kiborek (Mogotio), Gideon Kimaiyo (Keiyo Kusini) na Nelson Koech (Belgut), wote walipata asilimia 73.
Kwa upande wa Seneti, Seneta Murango aliongoza kwa asilimia 69, huku Mwakilishi wa Kike wa Kirinyaga, Jane Njeri Maina akiwa mwanamke aliyeongoza kitaifa kwa asilimia 67.
Seneta Murango amekuwa mstari wa mbele kupigania mageuzi katika sekta ya kilimo.
Amekuwa akipambana ili ushuru uondolewe katika majanichai na kutaka marufuku ya usafirishaji wa makadamia yenye maganda uzuiwe na bei za mazao hayo ziboreshwe.
Zaidi ya wabunge 20 waliopata alama za juu tayari wametangaza nia ya kuwania ugavana katika uchaguzi wa Agosti 10, 2027.
Miongoni mwao ni Mbunge wa Uriri Mark Nyamita, anayewania ugavana wa Migori. Nyamita aliongoza Nyanza kwa asilimia 71, akifuatiwa na Walter Owino wa Awendo na Peter Masara (Suna Mashariki), waliopata asilimia 70.
Mbunge wa Ugenya David Ochieng, anayewania ugavana wa Siaya, pia alipata asilimia 70.
Wengine wanaowania ugavana waliopata alama za juu ni Mbunge wa Nyali Mohammed Ali (Mombasa), Mbunge wa Emuhaya Omboko Milemba (Vihiga) na Mbunge wa Embakasi Kaskazini James Gakuya (Nairobi).
Kwa upande wa maseneta, wanaowania ugavana waliopata alama za juu ni Murango (Kirinyaga), Richard Onyonka (Kisii), Godfrey Osotsi (Vihiga), Enoch Wambua (Kitui), Boni Khalwale (Kakamega) na Tom Ojienda (Kisumu).