Dondoo

MCAs wawili mashakani kwa kuzozania mwenzao wa kike

Na MWANDISHI WETU July 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BONDE LA UFA:

BUNGE moja la kaunti limegubikwa na minong’ono baada ya madiwani wawili wa wadi, ambao wote ni wanaume waliooa, kuripotiwa kutofautiana vikali kutokana na uhusiano wao na mbunge mwenzao wa kike.

Kwa mujibu wa duru za kisiasa, wawili hao waliokuwa marafiki wa karibu na waliokuwa wakionekana pamoja katika mikutano ya kamati na shughuli za bunge sasa hawasemezani wala kusalimiana.

Inadaiwa pia hawaonekani tena wakinywa chai pamoja au kuketi karibu wakati wa shughuli rasmi.

Chanzo cha mzozo huo kinadaiwa kuwa ni ukaribu wa diwani huyo wa kike na viongozi hao wawili, hali iliyochochea wivu na ushindani wa kisiasa na kibinafsi.

Wadokezi wanasema juhudi za wenzao kuwapatanisha zimegonga mwamba.

Hata shughuli za kawaida za bunge zimeripotiwa kuwa na mvutano kila mara watatu hao wanapokutana katika kikao au hafla moja.