Wanne wanyakwa kwa kuiba mchele wa pishori wa Sh2 bilioni siku ya Saba Saba
WASHUKIWA wanne wamezuiliwa kwa siku 14 huku polisi wakiendelea na uchunguzi kuhusu wizi wa magunia ya mchele wa Pishori kutoka kwa shehena yenye thamani ya Sh2 bilioni iliyokuwa imehifadhiwa katika ghala moja mjini Mombasa.
Wizi huo ulisemekana kutokea Julai 7, wakati sehemu nyingi za nchi zilikuwa zikikumbwa na wasiwasi kuhusu maandamano ya kuadhimisha siku ya Saba Saba.
Washukiwa hao, Collins Wanjala Wafula, David Isata Asembo, Daniel Mwendwa Muthoka na Omar Adede Onduto walifikishwa mbele ya Mahakama ya Mombasa Jumatano, ambapo maafisa wa upelelezi walipata kibali cha kuwazuia kwa muda wa siku 14 ili kukamilisha uchunguzi.
Kwa mujibu wa hati ya kiapo iliyowasilishwa na afisa anayechunguza kesi hiyo, Bw Feisal Omar, uchunguzi unahusu kosa la kuvamia jengo na kutekeleza uhalifu, kinyume na sheria.
Kisa hicho kiliripotiwa na Bw Yusuf Swalleh Juma, Mkuu wa Idara ya Usalama katika Kampuni ya FOCUS Container Freight Station, katika Kituo cha Polisi cha Changamwe.
Wapelelezi waliiambia mahakama kuwa watu wasiojulikana walivunja ghala la kampuni hiyo na kuiba idadi ambayo haijabainishwa ya magunia ya kilo 25 ya mchele aina ya Marai Premium Pishori kutoka kwa shehena ya awali ya magunia 800,000 yenye thamani ya Sh2 bilioni.
Uchunguzi pia unaonyesha kuwa, wahusika walivamia chumba cha mfumo wa kamera za usalama (CCTV), wakaharibu kabisa mfumo huo na kuondoka na kifaa cha kuhifadhi kumbukumbu za video (DVR) zilizofaa kunaswa.
Aidha, sehemu kuu ya kuwasha na kuzima umeme iliharibiwa, jambo ambalo polisi wanaamini lililenga kuzima mfumo wa usalama kabisa kabla ya wizi kutekelezwa.
Afisa anayechunguza kesi hiyo alisema wanahitaji muda zaidi kupata rekodi za kamera za usalama kutoka kampuni na maghala jirani ili kusaidia kubaini waliohusika na wizi huo.
Polisi pia waliieleza mahakama kuwa zoezi la kuhesabu upya shehena yote bado linaendelea kutokana na ukubwa wa mzigo uliokuwa umehifadhiwa, ili kubainisha kiwango halisi cha magunia yaliyodaiwa kuibiwa.
Kwa mujibu wa hati ya kiapo, zaidi ya washukiwa 30 bado hawajakamatwa.
“Washukiwa hawa wanne wakiachiliwa wanaweza kutatiza juhudi za kuwakamata washukiwa wengine kwa kuwa wanaweza kuwasiliana nao.”
Wapelelezi waliongeza kuwa kuachiliwa kwa washukiwa kunaweza kuathiri juhudi za kurejesha vielelezo na mali zilizoibwa, pamoja na kuwakamata washirika wengine wanaoshukiwa kuhusika katika uhalifu huo.
Polisi pia walisema wanakusudia kufanya gwaride la utambuzi kwa kutumia mashahidi waliojitokeza kusaidia kubaini washukiwa na nafasi aliyotekeleza kila mmoja katika kutekeleza uhalifu huo.
Mahakama ilielezwa kuwa amri ya kuwazuilia washukiwa ni muhimu ili kuwapa wapelelezi nafasi ya kukamilisha uchunguzi kabla ya kuamua iwapo watafunguliwa mashtaka ya jinai.