Jhanda sasa adai wakazi wa Keumbu walichokozwa na Linda Mwananchi
MBUNGE wa Nyaribari Chache, Zaheer Jhanda, amevunja kimya chake kuhusu uvamizi dhidi ya msafara wa viongozi wa Linda Mwananchi katika Soko la Keumbu, Kaunti ya Kisii, zaidi ya wiki moja iliyopita.
Uvamizi huo ulisababisha mauti ya mtu mmoja baada ya watu wanaoshukiwa kuwa wahuni kurusha mawe kwenye magari yaliyokuwa katika msafara huo.
Akilaani tukio hilo, Bw Jhanda alijitenga na vurugu hizo na badala yake akailaumu kambi ya upinzani kwa madai ya kuwasafirisha wahuni kutoka maeneo mengine ili kuwashambulia wakazi wa eneobunge lake.
“Mimi ni mtu wa amani. Je, mmewahi kuniona nikihusika na vurugu?” akasema Bw Jhanda.
“Mmenipa jukumu la kuhimiza amani ilhali wanasema nilihusika na vurugu. Sisi watu wa Nyaribari Chache tunapenda amani na nataka kutumia fursa hii kulaani vurugu zilizotokea hapa,” akaongeza mbunge huyo.
Alikuwa akizungumza na maelfu ya wakazi, wengi wao wakiwa wanawake, katika maeneo ya Birongo na Keumbu wakati wa shughuli ya kugawa sukari, maharagwe, mafuta ya kupikia na mchele.
Bw Jhanda bila kuwasilisha ushahidi alidai kwamba viongozi wa Linda Mwananchi waliwasafirisha wahuni waliowavamia wakazi wa eneo hilo na hivyo kuwafanya kujibu mashambulizi hayo.
“Watu hao walikuja hapa kutuchokoza. Walikuwa na mishale, marungu na silaha nyingine na wakaanza kuwashambulia wanawake wetu. Walianza kuturushia mawe ndipo watu wetu walipojibu kwa kujilinda,” akaongeza Bw Jhanda.
Mbunge huyo alikanusha madai kuwa wakazi wa Keumbu ndio walioanzisha vurugu hizo.
Alisema mapigano yalianza baada ya wakazi kujitetea dhidi ya wavamizi hao wanaodaiwa kuwa waliletwa kutoka maeneo mengine.
“Sijawahi kumhimiza mtu yeyote kumshambulia au kumuua mwingine. Nimeambiwa mtu mmoja alipoteza maisha na alikuwa akisafiri kwenye gari lililokuwa likiendeshwa kwa kasi na akaanguka,” akasema Bw Jhanda.
Hata hivyo, video zinazosambaa mtandaoni kuhusu tukio la Keumbu zilionyesha hali tofauti.
Video hizo zinaonyesha wanaume na wanawake waliokuwa na mawe wakishambulia msafara wa viongozi wa Linda Mwananchi.
Magari yalipokuwa yakiondoka kwa kasi huku vioo vyake vikivunjwa kwa mawe, mwanamume mmoja anaonekana akianguka kutoka kwenye gari la aina ya SUV baada ya kugongwa na jiwe.
Baada ya kuanguka, mwathiriwa anaonekana akijaribu kutembea huku akichechemea kabla ya kukamatwa na kupigwa kwa silaha butu.
Mwanamume huyo, aliyetambuliwa kama Vincent Osiemo maarufu kama Mapinduzi, baadaye alithibitishwa kufariki.
Wakati wote wa tukio hilo, maafisa wa polisi walikuwepo eneo la tukio lakini hawakuingilia kati huku wahuni wakiendelea kurusha mawe kwenye msafara huo.
“Watu wa Nyaribari Chache tunatuma salamu za rambirambi kwa familia ya mwanamume aliyeanguka kutoka kwenye gari lililokuwa likiendeshwa kwa kasi na kufariki. Tunawapa pole familia yake,” akasema Jhanda.