Kifungo cha maisha gerezani kwa mwanajeshi aliyeua mke na wanawe wawili Laikipia
ALIYEKUWA Meja wa Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF), Peter Mugure Mwaura, amehukumiwa kifungo cha maisha jela baada ya Mahakama Kuu kumpata na hatia ya kumuua mkewe na watoto wao wawili.
Jaji Martin Muya alisema mauaji hayo yalikuwa ya kinyama na yaliyopangwa kwa umakini.
“Nimezingatia ripoti kuhusu athari za mauaji haya kwa familia ya waathiriwa. Mauaji ya watu hawa watatu yalikuwa ya kinyama,” alisema Jaji Muya.
Jaji pia alisema Mugure hakuonyesha hata chembe ya majuto kwa kitendo chake.
“Kwa kuzingatia mazingira ya kesi hii, nakuhukumu kifungo cha maisha gerezani,” akaamua.
Hukumu hiyo ilitolewa siku chache baada ya mahakama kumpata na hatia ya kumuua mkewe Joyce Syombua Maua, mwenye umri wa miaka 31, binti yao Shanice Mugure Mwaura mwenye miaka 10 na mwanao Peter Mwaura Junior, almaarufu Prince Michael, mwenye miaka mitano.
Waendesha mashtaka walitaka Mugure ahukumiwe kifo wakisema aliangamiza familia yake kwa mpango uliotekelezwa kwa umakini.
Hata hivyo, mahakama iliamua kifungo cha maisha baada ya kuzingatia uzito wa uhalifu huo, athari zake kwa familia ya marehemu na muda ambao Mugure alikuwa amezuiliwa rumande.
Baada ya hukumu kutolewa, Mugure alisema hakukubaliana nayo.
“Kwa heshima kubwa kwa mahakama, sikubaliani na uamuzi huu,” alisema akiwa kizimbani.
Jaji Muya alimweleza kuwa ana haki ya kukata rufaa katika Mahakama ya Rufaa.
Kesi hiyo ilianzia Oktoba 2019 baada ya Mugure kumwalika Joyce na watoto wao kwenda kumtembelea katika Kambi ya Jeshi la Anga la Kenya mjini Nanyuki.
Joyce alisafiri kutoka Nairobi akiwa na watoto hao akiamini walikuwa wanaenda kuungana kama familia.
Hawakurudi tena nyumbani.
Ushahidi ulionyesha walikesha nyumbani kwa Mugure kabla ya kwenda kula chakula cha mchana katika Hoteli ya Kilimara Springs.
Hiyo ndiyo ilikuwa mara ya mwisho kuonekana wakiwa hai.
Mahakama ilibaini kuwa waliporejea kambini, Mugure aliwaua wote watatu.
Kisha aliweka miili yao kwenye mifuko maalumu ya kuhifadhia maiti, akaipakia kwenye buti ya gari lake na kuipeleka Thigithu, Kaunti ya Laikipia, ambako aliizika katika kaburi la kina kifupi.
“Ushahidi unaonyesha mshtakiwa alimuua mkewe na watoto wake wawili, akaweka miili yao kwenye mifuko ya maiti na kuificha kwenye buti ya gari kabla ya kuwazika Thigithu,” alisema Jaji Muya.