Habari za Kaunti

Kisa cha afisa wa DCI kudungwa kisu chaibua hofu ya ujasiri wa wahalifu

Na KALUME KAZUNGU July 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ONGEZEKO la mashambulizi dhidi ya maafisa wa polisi katika Kaunti ya Lamu limezua wasiwasi kuhusu iwapo makundi ya wahalifu yanazidi kupata ujasiri licha ya juhudi za miaka mingi zilizolenga kurejesha amani katika kaunti hiyo.

Ndani ya kipindi cha miezi miwili pekee, angalau maafisa watatu wa usalama wameshambuliwa.

Tukio la hivi majuzi zaidi lilimhusu afisa wa Idara ya Kuchunguza Uhalifu (DCI) ambaye alishambuliwa na kujeruhiwa na mwanamume alipokuwa akitembea katika eneo la Langoni, kisiwani Lamu, mwendo wa saa nne asubuhi Ijumaa iliyopita.

Mashahidi walisema afisa huyo alichomwa kisu tumboni, shingoni na mbavuni kabla ya mshambuliaji kutoroka.

Afisa huyo bado amelazwa hospitalini akiendelea kupokea matibabu.

Kwa mujibu wa mashahidi, alikuwa akitembea pamoja na mwenzake, wote wakiwa wamevalia nguo za kiraia. Ghafla, mwanamume aliwagonga kwa nguvu.

Mmoja wa maafisa hao alirudi nyuma kwa tahadhari, akamshika mkono mwanamume huyo na kumuuliza kwa ukali kwa nini alikuwa na fujo.

Badala ya kuomba radhi, mwanamume huyo alionyesha uhasama, akapaza sauti na kumsukuma afisa huyo.

Bw Abdi Osman, mchuuzi, alisema walianza kupigana ghafla kwa karibu dakika nne. Afisa wa pili aliingilia kati ili kumvuta mshambuliaji huyo.

“Hata kabla ya maafisa hao wawili kutoa bunduki zao ili kudhibiti hali, mshambuliaji alitoa kwa kasi kisu alichokuwa amekificha kiunoni na kumchoma mmoja wa maafisa. Kisu kilimdunga tumboni, mbavuni na shingoni,” alisema Bw Osman.

Bw Simon Kadenge, shahidi mwingine, alisema mara tu afisa wa pili alipoona mshukiwa ametoa kisu na kumchoma mwenzake, alikimbia kutoka eneo la tukio.

“Eneo hilo liliendelea kuvutia wananchi wengi. Walifika na kumsaidia afisa aliyejeruhiwa. Kufikia wakati huo, mshukiwa alikuwa tayari ametoweka,” alisema.

Duru za polisi zilisema maafisa hao wawili wa DCI walikuwa wamehamishiwa eneo hilo karibu wiki moja kabla ya tukio hilo.

Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Lamu Shadrack Ruto, alikashifu tabia za wananchi ambao wamekuwa wakiwalenga maafisa wa usalama na kuwadhuru akionya kuwa chuma chao kiko motoni.

Alisema katika kipindi cha miezi miwili iliyopita, maafisa watatu wa usalama wamevamiwa na kujeruhiwa na raia katika maeneo ya kisiwa cha Lamu na Hindi.

“Mbali na shambulio la Ijumaa mjini Lamu, mwezi mmoja uliopita kuna askari wetu wawili wa akiba (NPR) waliolazimika kumpiga risasi na kumuua mwanamume raia aliyejaribu kuwavamia mjini Hindi akiwa amebeba mkuki na panga. Lazima watu waepuke kushambulia polisi kwani hatutawavumilia kamwe,” akasema Bw Ruto.

Wanaharakati na wakazi pia walikashifu vitendo hivyo.

Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la kutetea haki la Vocal Africa, Bw Hussein Khalid, alisema mashambulio hayo ni ishara ya ongezeko la ukosefu wa usalama unaotendwa na vijana wa eneo hilo kwa muda sasa.

“Miaka ya zamani tumewahi kuona hata machifu wakiuawa, vijana wakikatwa miguu na sasa maafisa wa usalama wameanza kudungwa visu. Wizara ya usalama wa Ndani lazima ishuke Lamu kukabiliana na kumaliza tatizo hilo,” akasema Bw Khalid.

Bi Zeinab Ahmed, mkazi, alitoa wito kwa wazazi kufuatilia mienendo ya watoto wao ili kuwakomesha kuingilia makundi ya uhalifu.

Naye Afisa wa Haki Africa Mathias Shipeta alisema tatizo la utovu wa usalama linahitaji nyanja zote, zikiwemo zile za siasa kuhusika.