NCIC yasema itaendelea kufuatilia matamshi ya Duale, Gachagua na wengine sita
TUME ya Kitaifa ya Uwiano na Utangamano (NCIC) imesema itaendelea na uchunguzi dhidi ya Waziri wa Afya Aden Duale na aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua kuhusu matamshi ya chuki na uchochezi wa kikabila, licha ya wawili hao kutangaza hadharani kwamba hawataitikia wito wa tume hiyo.
Mwenyekiti wa NCIC Askofu Kepha Nyamweya, alisema tume hiyo haitaruhusu wanasiasa kuamua namna uchunguzi wake unavyofanywa na kwamba itaendelea kutekeleza wajibu wake bila uoga, upendeleo wala msukumo wa kisiasa.
“Kuna wakati wa siasa na kuna wakati wa kazi na hatuwezi kuruhusu mchezo wa aina hiyo. Mtu hawezi kusema atafika mbele ya tume baada ya mwingine kufika. Tutafanya kazi yetu kwa mujibu wa sheria,” akasema Bw Nyamweya.
Kauli hiyo ilijiri baada ya Bw Duale kusema hatafika mbele ya NCIC hadi pale Bw Gachagua atakapoitwa kwanza kujibu matamshi yake yaliyofasiriwa kuwa ya uchochezi.
“Kama hakuna Gachagua, hakuna Duale,” alisema waziri huyo, akisisitiza kuwa sheria inapaswa kutumika kwa usawa kwa wote.
Hata hivyo, Bw Nyamweya alisema watu wanaochunguzwa hawawezi kuielekeza tume yake jinsi ya kutekeleza majukumu yake.
“Tunatoa wito kwa wanaohitajika kufika mbele yetu. Wakikosa kufika, sheria imeweka utaratibu wa kushughulikia hali hiyo. Tutachukua hatua bila mapendeleo,” akaongeza.
Kwa upande wake, Bw Gachagua ameendelea kutetea matamshi yake aliyosema “watamuua nyoka pamoja na mayai yake,” akidai yalikuwa ya kimethali, yakimaanisha kuwashinda kisiasa Rais William Ruto na washirika wake kupitia kura, wala si kutumia vurugu.
Alisema iwapo NCIC inahitaji maelezo yake, imuandikie rasmi naye atajibu.
Mbali na viongozi hao wawili, NCIC pia imeanzisha uchunguzi dhidi ya Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku, Gavana wa Busia Paul Otuoma, Naibu Gavana wa Mandera Ali Maalim Mohamud, Mbunge wa Sirisia John Waluke pamoja na Tipape Naini Musa na Dkt Dennis Adison Ouma kwa madai ya matamshi ya chuki na uchochezi.
Tume imesisitiza kuwa wote wanaochunguzwa wanachukuliwa kuwa hawana hatia hadi uchunguzi utakapokamilika.
Nyamweya alionya kuwa matamshi ya kisiasa nchini yanazidi kuwa makali huku baadhi ya viongozi wakitumia lugha inayowagawa wananchi kwa misingi ya kikabila badala ya kushindana kwa sera.
“Lugha inatumiwa kuwafanya wapinzani waonekane maadui badala ya majirani wenye mitazamo tofauti. Hali hii inaweza kuhatarisha umoja wa taifa,” alisema.
Alieleza kuwa NCIC imepewa mamlaka chini ya Sheria ya Uwiano na Utangamano ya kuchunguza matamshi ya chuki, kuwaita mashahidi, kukusanya ushahidi na kuwasilisha faili kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) kwa hatua zaidi.
Bw Nyamweya alikanusha madai kwamba tume hiyo inaweza kushinikizwa kisiasa, akisema itaendelea kutekeleza wajibu wake kwa haki huku ikishirikiana na Baraza la Kidini Kenya kuimarisha juhudi za kuzuia matamshi ya chuki na kuhakikisha uchaguzi wa 2027 unafanyika kwa amani.