Wasichana wengi wanaobalehe Tana River ni wajawazito – Utafiti
ZAIDI ya msichana mmoja kati ya wanne aliyefikia umri wa kubalehe katika Kaunti ya Tana River alikuwa mjamzito kati ya Januari na Juni mwaka huu, utafiti mpya umebaini.
Utafiti huo uliofanywa na Shirika la Kimataifa la Utafiti kuhusu Wanawake Afrika (ICRW Africa) kwa ushirikiano na Shirika la Kitaifa kuhusu Takwimu Kenya (KNBS), umeonyesha kuwa asilimia 27.5 ya wasichana wanaobalehe katika kaunti hiyo walikuwa wajawazito wakati wa utafiti huo.
Matokeo hayo pia yanaonyesha hali ya kutatanisha katika kaunti za Garissa, Homa Bay, Samburu na Pokot Magharibi, ambako wasichana wengi wanakosa taarifa sahihi kuhusu afya ya uzazi kufanya maamuzi yanayofaa.
Utafiti huo uliandaliwa kabla ya kuanza kwa mpango wa miaka mitano unaoitwa Her Health Initiative, unaolenga kuboresha afya ya uzazi kwa wasichana katika kaunti hizo tano.
Ripoti hiyo iliyoidhinishwa Nairobi Ijumaa iliyopita ilibaini kuwa ni asilimia 53 pekee ya wasichana wa Tana River ambao wamewahi kuhudhuria shule, huku asilimia 51 wakiwa hawajui kusoma wala kuandika.
Aidha, wastani wa umri wa wasichana kuanza kushiriki ngono ni miaka 15.8.
Kati ya wasichana wanaoshiriki ngono, asilimia 81.3 wamewahi kupata ujauzito, huku asilimia 27.5 ya wote waliohojiwa wakiwa wajawazito wakati wa utafiti.
Mkurugenzi wa Reproductive Health Network Kenya (RHNK), Bi Nelly Munyasia, alisema viwango vya chini vya elimu na maarifa vinachangia ongezeko la mimba za mapema.
“Wasichana wasiohudhuria shule hukosa elimu. Kukosa elimu kunawanyima taarifa sahihi. Kukosa taarifa kunapunguza matumizi ya njia za kupanga uzazi, na mimba huwafanya wengine kuacha shule. Mzunguko huo unaendelea kujirudia,” alisema.
Ripoti hiyo pia ilibaini kuwa ni asilimia 41.3 pekee ya shule za Tana River zinazotoa elimu kuhusu afya ya uzazi, kiwango cha chini zaidi kati ya kaunti zote zilizoshirikishwa.
Hata hivyo, watafiti walisema sababu za hali hiyo zinatofautiana kati ya kaunti hizo, hivyo suluhu pia zinapaswa kuwa tofauti.
Katika Samburu, wasichana huanza kushiriki ngono wakiwa na wastani wa miaka 15.5, kiwango cha chini zaidi kati ya kaunti zote.
Ingawa zaidi ya asilimia 89 wanafahamu kuhusu sindano kupanga uzazi na asilimia 92 wanajua kuhusu kondomu, zaidi ya asilimia 82 walisema wanahitaji elimu zaidi kuhusu afya ya uzazi.
Kwa upande wa Homa Bay, utafiti ulionyesha hali tofauti.
Kaunti hiyo ina kiwango cha juu zaidi cha mahudhurio shuleni cha asilimia 99.1 na asilimia 98.7 ya wasichana wanajua kusoma na kuandika.
Hata hivyo, asilimia 36.4 ya wasichana wanaoshiriki ngono wamewahi kupata ujauzito, huku asilimia 7.5 wakiwa wajawazito wakati wa utafiti.
Garissa ndiyo kaunti iliyorekodi kiwango cha chini zaidi cha wasichana waliowahi kushiriki ngono, asilimia 1.3 pekee, na hakuna aliyekuwa mjamzito wakati wa utafiti.
Hata hivyo, utafiti ulionyesha kuwa maarifa kuhusu matumizi ya kondomu katika kaunti hiyo ni ya chini zaidi, yakifikia asilimia 27.2 pekee.
Ripoti hiyo ilibaini kuwa katika kaunti zote tano, walimu ndio chanzo kikuu cha taarifa kuhusu afya ya uzazi kwa wasichana wa balehe, huku akina mama wakishika nafasi ya pili.
Bi Munyasia alisema matokeo hayo yanaonyesha umuhimu wa kuwawezesha walimu na wazazi kwa mafunzo na nyenzo zinazohitajika ili kuwapa vijana taarifa sahihi kuhusu afya ya uzazi.