Sababu ya IEBC kuruhusu wasio na digrii kuwania urais na ugavana 2027
WAKENYA wasio na digrii ya chuo kikuu wataweza kuwania urais, ugavana na ubunge katika uchaguzi mkuu ujao baada ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kuthibitisha kuwa hitaji la kuwa na shahada halitumiki kwa sasa kufuatia maamuzi ya mahakama yaliyolitangaza kuwa kinyume cha Katiba.
Kamishna wa IEBC Ann Nderitu alisema Jumatatu kuwa tume hiyo haiwezi kutekeleza sharti la wawaniaji kuwa na digrii kwa sababu mahakama tayari ililitupilia mbali.
“Tunapoanza maandalizi sasa, hakuna sharti la digrii kwa mtu yeyote. Hiyo ndiyo hali ilivyo kwa sasa,” Nderitu alisema katika mahojiano na Citizen TV.
Ufafanuzi huo unamaliza miaka ya sintofahamu iliyoshuhudia baadhi ya wagombea maarufu wakikabiliwa na maswali kuhusu vyeti vyao vya masomo.
Mojawapo ya kesi zilizovutia hisia za wengi ni ile ya Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja mnamo 2022.
Tume ya Elimu ya Vyuo Vikuu (CUE) ilieleza kuwa, digrii yake kutoka Team University ya Uganda haikuwa imethibitishwa, na kesi tatu zikawasilishwa kupinga ugombeaji wake.
Hata hivyo, IEBC ilimuidhinisha kwa hoja kwamba jukumu lake ni kupokea stakabadhi, si kuzithibitisha. Mahakama Kuu iliunga mkono uamuzi huo na Sakaja akashinda uchaguzi.
Kaunti ya Turkana nayo ilishuhudia mkanganyiko kama huo wakati Gavana Jeremiah Lomorukai aliidhinishwa na IEBC licha ya Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) kudai digrii na diploma yake zilikuwa ghushi na kutaka akamatwe siku nne kabla ya uchaguzi.
Mahakama ilimruhusu kuendelea kugombea na hatimaye akashinda.
Kesi hizo zilifuatia maamuzi mawili muhimu ya Jaji Anthony Mrima mnamo 2021 na 2022 yaliyobatilisha Kifungu cha 22 cha Sheria ya Uchaguzi.
Kwanza, jaji huyo alifuta kifungu kilichowataka wagombeaji ubunge kuwa na digrii, akisema hakikupitishwa kupitia ushirikishaji wa umma wa kutosha.