Habari za Kitaifa

Wezi wapora masanduku yaliyojaa pesa nyumbani kwa kamanda wa zamani wa GSU

Na STANLEY NGOTHO August 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAJAMBAZI wanaoshukiwa kuwa wanachama wa genge la watu sita walivamia nyumba ya aliyekuwa Kamanda wa Kikosi cha Kukabiliana na Fujo (GSU), Ranson Lolmodooni, katika eneo la Kitengela Police Sacco Estate, Kaunti ya Kajiado, na kuiba kiasi kisichojulikana cha fedha taslimu.

Kulingana na taarifa za polisi na mashahidi, washukiwa hao walijifanya waumini waliokuwa wakielekea kwenye mkutano wa maombi na kufanikiwa kuingia katika mtaa huo wa makazi ya kifahari mnamo Jumapili, Agosti 16.

Mtaa huo unaoishi maafisa wa polisi wanaohudumu na waliostaafu, yanachukuliwa kuwa miongoni mwa maeneo yenye ulinzi mkali zaidi mjini Kitengela.

Ripoti ya polisi inaonyesha kuwa wahalifu hao walitumia mashine za kukata, kuvunja na kuingia ndani ya nyumba ya Bw Lolmodooni, ambaye alistaafu wadhifa wa Kamanda wa GSU mnamo Juni mwaka huu baada ya kuhudumu kwa miaka miwili.

Inadaiwa kuwa waliondoka na masanduku yaliyokuwa yamejaa fedha taslimu. Hata hivyo, sehemu ya fedha hizo zilipatikana barabarani baada ya kuanguka walipokuwa wakiondoka.

Majirani waliambia Taifa Leo kuwa noti za Sh1,000 zilionekana zimetapakaa kwenye Barabara ya 5 ndani ya mtaa huo. Pia walidai kuwa wahalifu waliwatupia walinzi na watu waliokuwa karibu noti za fedha walipokuwa wakitoroka.

Katika ujumbe uliosambazwa kwenye kundi la WhatsApp la usalama katika mtaa huo, ilielezwa kuwa wanaume wanne wenye silaha na wanawake wawili waliingia kwa hila kabla ya kuvamia nyumba hiyo na kuiba fedha.

Wahalifu hao walipokuwa wakijaribu kutoroka, mmoja wa walinzi alijaribu kuzuia gari lao katika lango kuu.

Kamera za CCTV zilinasa wawili wa washukiwa wakimshambulia kwa ngumi, mateke na fimbo hadi wakamshinda na kufanikiwa kutoroka kuelekea Isinya.

Baadaye, moja ya magari yaliyotumiwa na washukiwa lilipatikana mjini Isinya, kilomita 21 kutoka eneo la tukio.

Polisi walipata nambari kadhaa za usajili wa magari, bastola inayodaiwa kumilikiwa na afisa huyo wa zamani wa polisi pamoja na fedha zaidi.

Hata hivyo, Bw Lolmodooni alikanusha madai kuwa fedha ziliibwa nyumbani kwake.

“Kwangu kulikuwa jaribio la wizi. Majirani waligundua kilichokuwa kinaendelea na kupiga kamsa. Hakuna fedha zilizoibwa. Sisi hatuweki fedha nyumbani. Huo ni uvumi tu,” alisema.

Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Kajiado Alex Shikondi, alithibitisha kuwa uchunguzi unaendelea na hakuna mshukiwa aliyekuwa amekamatwa.

Tukio hilo linajiri wakati Kitengela inakumbwa na ongezeko la visa vya ukosefu wa usalama.

Katika muda wa wiki mbili zilizopita, wanaume watatu wameuawa katika matukio tofauti huku wakazi wengi wakijeruhiwa na magenge ya wahalifu wanaoshambulia usiku.