Mzozo wa fidia Mau wazuka tena familia 15,000 zikidai kuachwa nje
MPANGO wa kufidia familia zilizofurushwa kutoka Msitu wa Mau umeibua tena mzozo wa kibinadamu na kisiasa katika eneo la South Rift, huku maelfu ya waathiriwa wakidai serikali imewatelekeza.
Zaidi ya familia 15,000 ambazo hazikujumuishwa katika mpango wa fidia sasa zinataka kulipwa. Zinadai baadhi ya maafisa wa serikali waliingiza majina ya jamaa na washirika wao katika orodha ya walionufaika, licha ya kutokuwa waathiriwa.
Mzozo huo ulizuka baada ya Rais William Ruto kutangaza Agosti 26 katika uwanja wa Shule ya Sekondari ya Tendwet, Narok Kusini, kuwa serikali ilikuwa imelipa familia 13,000 zilizofurushwa Mau mwaka 2019.
Serikali ilikuwa imesajili familia 28,000 kuwa waathiriwa wa zoezi hilo. Hata hivyo, haikutoa maelezo ya kwa nini familia 15,000 ziliachwa nje ya mpango wa fidia.
Rais Ruto alisema Sh2.6 bilioni zimetolewa kwa familia 13,000, kila moja ikipokea Sh200,000 kupitia simu zao.
“Leo tunatoa Sh2.6 bilioni kwa jumla ya familia 13,000 zilizofurushwa kutoka Msitu wa Mau. Kila familia sasa itapokea Sh200,000 kama fidia,” alisema.
Alisema familia nyingine 2,000 zilizokuwa zinaishi katika kambi za wakimbizi wa ndani zilishapokea fidia ya Sh300,000 kila moja, hatua iliyowezesha kufungwa kwa kambi hizo baada ya zaidi ya miaka sita.
Rais Ruto alisema suala la Mau lilikuwa limefikia mwisho. Hata hivyo, tangazo hilo limefufua mzozo huo badala ya kuumaliza.
Familia zilizoachwa nje zimelalamika na kutishia kurejea katika Msitu wa Mau iwapo serikali haitazifidia kama wenzao waliolipwa.
Katika mkutano uliofanyika Olmekenyu mnamo Alhamisi, maelfu ya waathiriwa walitaka serikali ieleze kwa nini waliondolewa kwenye orodha ya walionufaika.
Walisema serikali ina siku saba kutoa suluhisho kabla yao kuchukua hatua zaidi.
Diwani wa wadi ya Mara, Kipngeno Chepkwony, ambaye ndiye kiongozi pekee aliyezungumza na waathiriwa hao, aliitaka serikali kuchunguza suala hilo upya.
“Tuongee na serikali na hasa Rais kuhusu suala hili ili tupate suluhisho la kudumu. Tusiruhusu suala hili kutumiwa kisiasa ili watu walioachwa nje ya mpango wa fidia waweze kuzingatiwa na kulipwa,” alisema.
Mmoja wa waathiriwa, Fred Mutai, alisema familia zimevumilia kwa muda mrefu.
“Familia zimeteseka kwa muda mrefu, lakini serikali imeongeza chumvi na pilipili kwenye kidonda cha zamani na kufanya hali ambayo tayari ilikuwa dhaifu kuwa mbaya zaidi,” alisema.
Afisa wa DCP Leonard Cheruiyot alisema Sh200,000 hazitoshi na serikali ilipaswa kununua ardhi na kuwapa waathiriwa makazi mapya.