Habari

Wakazi wa Magadi wahofia kukosa huduma za hospitali baada ya kampuni kufurushwa

Na STANLEY NGOTHO September 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HUDUMA za matibabu katika Hospitali ya Magadi zinaendelea bila kukatizwa licha ya mzozo unaoendelea kati ya Serikali na kampuni ya Tata Chemicals.

Hata hivyo, hofu imetanda miongoni mwa wakazi baada ya Rais William Ruto kuelekeza Serikali ya Kaunti ya Kajiado kuchukua usimamizi wa hospitali hiyo.

Hospitali hiyo ya kiwango cha nne inahudumia wakazi kutoka Shompole, Olkiramatian na Olkeri Oldonyonyokie, wakiwemo wajawazito na wagonjwa wanaohitaji upasuaji, huduma za nje na kulazwa.

Rais Ruto alitoa agizo hilo Jumamosi alipokuwa katika ziara ya maendeleo Kajiado, siku moja kabla ya kuagiza Tata Chemicals kuondoka nchini.

“Hospitali ni ya wananchi. Serikali ya kaunti ichukue usimamizi wa hospitali ili kuwawezesha wakazi kuendelea kupata huduma za matibabu,” alisema Rais Ruto.

Hata hivyo, wakazi wana hofu kuwa mabadiliko ya ghafla ya usimamizi yanaweza kuvuruga huduma.

Ziara ya Taifa Leo hospitalini humo Jumatatu ilionyesha idadi kubwa ya wagonjwa, hasa katika kitengo cha uzazi.

Hii ni tofauti na hali ya wiki mbili zilizopita, ambapo idadi ya wagonjwa ilikuwa imepungua baada ya kampuni kufungwa na kusababisha mzunguko wa fedha katika eneo hilo kudorora.

Hospitali hiyo iliyo na vitanda 54 ilijengwa na kuwekewa vifaa na Tata Chemicals, ambayo pia imekuwa ikiendesha shughuli zake.

Inatoa huduma kwa wakazi kwa gharama nafuu, huku madaktari, wauguzi, wahudumu wa afya na wafamasia wakiajiriwa na kampuni hiyo.

Bi Purity Naisiae alisema alifikishwa hospitalini usiku baada ya kuanza kupata maumivu ya kujifungua nyumbani. Alijifungua mtoto wa kiume kwa njia ya upasuaji.

“Hospitali hii ni tegemeo letu. Imeendelea kudumisha viwango vyake kwa miaka mingi,” alisema.

Mama yake, Bi Esther Nganoni, alisema hospitali hiyo imechangia kupunguza vifo vya watoto katika maeneo ya mashambani.

“Tunapita maeneo yenye wanyama hatari usiku tukiwa na matumaini ya kupata matibabu hapa,” alisema, akiomba kaunti isibadilishe usimamizi kwa haraka.

Wakazi walisema hospitali hiyo ndiyo tegemeo lao kuu kwa huduma maalumu, hasa uzazi, upasuaji na kulazwa.

Hofu yao imeongezwa na mgomo wa wahudumu wa afya katika hospitali za umma, ambao tayari umeathiri huduma katika kaunti kadhaa.

Hospitali ya Rufaa ya Kajiado, ambayo ndiyo mbadala karibu, iko zaidi ya kilomita 100 kutoka Magadi.

Msimamizi wa Hospitali ya Magadi, Dkt Raymond Birya, alisema hospitali hiyo hupokea angalau wanawake 21 wanaojifungua kila mwezi.

Alisema hospitali ina dawa za kutosha kwa takriban miezi mitatu na inaendelea kutoa huduma saa 24.

“Milango yetu bado iko wazi kwa wagonjwa,” alisema Dkt Birya.

Mzozo huo ulianza baada ya Wizara ya Madini kuagiza Tata Chemicals kusitisha shughuli zake Julai 29 kwa madai ya kutofuata masharti.