Ruto ajipalia makaa agizo lake likiweka Wakenya ughaibuni hofu ya kulengwa na waajiri
RAIS William Ruto ameshinikizwa kuhakikisha agizo lake la kuwabana raia wa kigeni wanaojihusisha na biashara ndogo nchini halichochei ubaguzi, chuki au hatua zinazoweza kuwa na madhara kwa Wakenya wanaoishi na kufanya kazi nje ya nchi.
Wasiwasi umeanza kutanda miongoni mwa Wakenya walio ughaibuni, huku baadhi wakisema wanaajiriwa na raia wa kigeni, wakiwemo raia wa Burundi, na kuhofia kuwa huenda wakalengwa iwapo mvutano huo utaendelea.
Wasiwasi huo umeibuka baada ya baadhi ya raia wa Burundi nchini Kenya kuripotiwa kutishwa na kubaguliwa kufuatia agizo la Rais Ruto kuhusu wafanyabiashara wa kigeni katika sekta ya biashara ndogo.
Chama cha Wanasheria Afrika Mashariki (EALS) kimeitaka Serikali kuhakikisha utekelezaji wa hatua hizo haugeuki kuwa kampeni ya kuwabagua watu kwa misingi ya uraia.
Katika taarifa yake iliyotolewa Arusha Jumatatu, EALS ilisema imeingiwa na wasiwasi kutokana na hofu miongoni mwa raia wa Burundi na mataifa mengine ya Jumuiya ya Afrika Mashariki wanaoishi Kenya.
“Mtu akishtakiwa kwa kukiuka sheria za Kenya anapaswa kushughulikiwa kwa misingi ya sheria husika na mazingira ya kesi yake. Uraia pekee haupaswi kuchukuliwa kuwa ushahidi wa uhalifu,” ilisema EALS.
Shirika hilo lilisema kuwa Kenya ina haki ya kudhibiti shughuli za kiuchumi nchini, ikiwa ni pamoja na kutekeleza sheria za uhamiaji, leseni, ushuru na ajira.
Hata hivyo, lilisema utekelezaji huo lazima uwe wa haki na mtu binafsi ashughulikiwe kulingana na kosa alilotenda, bila kuangalia taifa analotoka.
EALS ilionya kuwa hali hiyo inaweza kuathiri pia Wakenya wanaoishi na kufanya biashara katika nchi nyingine za Afrika Mashariki.
Hofu hiyo imeongezeka kutokana na taarifa kwamba mamia ya raia wa Burundi walifika katika ubalozi wao jijini Nairobi kutafuta hati za kusafiria na usaidizi wa kibalozi.
Baadhi yao walionekana wakibeba mizigo yao, yakiwemo magodoro na masanduku, huku wengine wakitafuta usafiri kurejea Burundi.
Wengine walilazimika kulala katika mazingira magumu ndani ya ubalozi huo wakihofia kurejea walikokuwa wakiishi baada ya biashara zao kuvamiwa.
Serikali ya Kenya, hata hivyo, imejaribu kutuliza hali hiyo kwa kutangaza muda wa siku 90 kwa raia wa kigeni wanaofanya biashara nchini kurekebisha hali yao ya uhamiaji, vibali vya kazi, usajili wa biashara na leseni.
Msemaji wa Ikulu Hussein Mohamed alisema raia wa kigeni wasio na nyaraka zinazohitajika wanapaswa kujitokeza katika balozi za nchi zao ili kusajiliwa.
Alisema watakaokuwa katika mchakato huo watachukuliwa kuwa wako nchini kihalali Serikali ikishirikiana na balozi zao kurekebisha hali yao.
Serikali pia imeonya Wakenya dhidi ya kuchukua sheria mkononi mwao na kuwanyanyasa wageni.
“Hakuna mtu au kundi lenye mamlaka ya kunyanyasa, kuwatisha au kuingilia shughuli za raia wa kigeni au biashara zao,” ilisema taarifa ya Ikulu.
Serikali ilisema baada ya siku 90, sheria kuhusu uhamiaji, vibali vya kazi, usajili wa biashara na leseni zitatekelezwa kwa ukali na kwa mujibu wa sheria.
Katibu wa Masuala ya Kigen Korir Sing’oei pia aliomba msamaha kwa raia wa Burundi waliokumbwa na unyanyasaji.
“Nataka kuwaomba msamaha raia wote wa Burundi hapa,” alisema alipofika katika Ubalozi wa Burundi jijini Nairobi Jumatatu.
Seneta Danson Mungatana, anayeongoza ujumbe wa Kenya katika Bunge la Pan-Afrika, ametaka Wizara ya Usalama wa Ndani kuchukua hatua dhidi ya ripoti za chuki na unyanyasaji wa raia Burundi, hasa Nakuru.
Alisema masuala ya wageni kufanya biashara nchini yanapaswa kushughulikiwa kupitia sheria za uhamiaji, leseni, ushuru na ajira, badala ya makundi ya watu kujichukulia sheria mikononi mwao.
Nchini Burundi, Waziri wa Masuala ya Kigeni Edouard Bizimana alionya kuwa hali hiyo inaweza kuwa na madhara kwa Wakenya wanaoishi nchini humo.
“Wakenya nchini Burundi wanaishi kwa amani, lakini ikiwa matamshi ya chuki dhidi ya Burundi yataendelea, mambo yatabadilika,” alisema.
Mkuu wa Chama cha raia wa Burundi wanaoishi Kenya, Alexis Ntinanirwa, pia alionya kuwa mzozo huo unaweza kuathiri uhusiano wa kikanda.
Alisema Wakenya wengi wanafanya biashara ndogo katika Burundi, Tanzania na Uganda.
“Suala hili halitasababisha matatizo kwa Waburundi wanaofanya kazi Kenya pekee, bali pia litasababisha matatizo katika eneo hili kwa sababu kuna Wakenya wanaofanya kazi hizi ndogo katika nchi zetu,” alisema.
Wakati huo huo, EALS imetaka Serikali kuweka wazi sheria na taratibu zitakazotumika katika kuwashughulikia wafanyabiashara wa kigeni.
Shirika hilo pia limetaka raia walioathirika wapewe nafasi ya kupata maelezo, msaada wa kisheria na kukata rufaa pale sheria inaporuhusu.
Rais Ruto amesema hatua hizo zinalenga kulinda nafasi za kiuchumi za Wakenya, hasa katika biashara ndogo zinazotegemewa na mamilioni ya watu.
Amesema Kenya iko tayari kupokea wawekezaji wa kigeni, lakini wawekezaji hao wanapaswa kuanzisha biashara zinazozalisha ajira badala ya kushindana na Wakenya katika biashara ndogo kama uchuuzi na maduka madogo.
Hata hivyo, hatua hiyo imezua mjadala mkali kuhusu namna ya kulinda maslahi ya Wakenya bila kuhatarisha uhusiano wa Kenya na majirani zake au maisha ya Wakenya wanaofanya kazi na biashara nje ya nchi.