Habari Mseto

Mwanamume aambia korti hajuti kukuza bangi baada ya kukosa ajira

Na TITUS OMINDE September 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MSHUKIWA ameambia mahakama kwamba hajuti kujihusisha na kilimo cha bangi baada ya kushindwa kupata ajira licha ya kuwa na cheti cha ufundi wa magari.

Bw Geoffrey Lingori, 58 alifikishwa mbele ya Hakimu Mwandamizi Mkuu, Kimani Mukabi katika Mahakama ya Eldoret, akikabiliwa na mashtaka mawili ya kulima na kusafirisha bangi.

Kesi hiyo itatajwa Septemba 18, 2026, kwa maelekezo zaidi.

Alishtakiwa kwa kulima bangi katika shamba la robo ekari kijijini Malel, Kapseret, ambako maafisa walidai kumpata na mimea hiyo yenye uzito wa gramu 34,000 na thamani ya Sh1.032 milioni.

Anakabiliwa pia na shtaka la kusafirisha gramu 50 za bangi zenye thamani ya Sh1,500.

Badala ya kuonyesha majuto, Lingori aliambia mahakama kuwa kilimo hicho ndicho chanzo chake kikuu cha mapato.

“Mheshimiwa Hakimu, ni kweli kwamba mimi hupanda bangi katika kipande changu kidogo cha ardhi kama chanzo changu kikuu cha mapato,” alisema.

Alisema alianza kulima bangi zaidi ya miaka 10 iliyopita baada ya kuhitimu kutoka Rift Valley Technical Training Institute (RVTTI) jijini Eldoret.

Lingori alisema alitafuta ajira akiwa na matumaini ya kujenga taaluma yake, lakini akakumbana na changamoto nyingi ikiwemo kukosa kazi.

Kesi hiyo itatajwa Septemba 18, 2026, kwa maelekezo zaidi.