Afya na Jamii

Kunywa chai moto sana huongeza hatari ya saratani ya umio – Utafiti

Na CECIL ODONGO September 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KUNYWA chai, kahawa au vinywaji vingine vikiwa moto sana kunaweza kuongeza hatari ya kupata saratani ya umio, kulingana na utafiti uliofanywa na watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Oxford Uingereza.

Utafiti huo, uliochapishwa katika Jarida la International Journal of Cancer, ulihusisha watu 977,282 wenye umri wa juu na umeelezwa kuwa mojawapo ya tafiti kubwa zaidi kuchunguza uhusiano kati ya joto la vinywaji na saratani ya umio.

Watafiti waligundua kuwa watu waliokunywa vinywaji vilivyo na joto la nyuzi 65 au zaidi walikuwa na hatari karibu mara tatu zaidi ya kupata saratani hiyo ikilinganishwa na waliokunywa vinywaji vya vuguvugu.

Kulingana na watafiti, mvuke wenye joto kali unaweza kuharibu chembe zinazofunika umio wakati unapopita kuelekea tumboni.

“Kunywa vikombe sita au zaidi vya vinywaji vya moto kwa siku kunaweza kuongeza hatari hiyo. Kuongezwa kwa maziwa kunaweza kupunguza joto kidogo, lakini chai au kahawa yenye maziwa bado inaweza kuwa moto kupita kiasi,” unasema utafiti huo.

Chai inayotengenezwa mara tu baada ya maji kuchemka inaweza kuwa na joto la karibu nyuzijoto 100. Inapomiminwa kwenye kikombe, joto hilo hupungua hadi karibu nyuzi 90–95.

Wataalamu wanashauri watu kusubiri kwa dakika chache kabla ya kunywa ili kinywaji kipoe hadi joto linalofaa.

Mtaalamu wa Afya, Dk Keren Papier, alisema tafiti za awali Amerika Kusini, ambako watu wengi hunywa kinywaji cha mitishamba kikiwa moto sana, pia zilionyesha uhusiano wa kupata aina hiyo ya saratani.

Hata hivyo, watafiti walisema hatari ya jumla ya kupata saratani ya umio bado ni ndogo hata kupitia unywaji wa vinywaji moto.

Njia muhimu zaidi za kupunguza hatari ni kutovuta sigara na kupunguza unywaji wa pombe.

Dalili za saratani ya umio zinaweza kujumuisha kiungulia, maumivu ya koo au kifua na kupungua uzani wa mwili.