Pambo

Unaweza kuishi maisha ya furaha kabisa bila kuwa na mpenzi, utafiti wadai

Na ESTHER INTABO September 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KWA miongo mingi, ndoa na mahusiano ya kimapenzi yamekuwa yakitazamwa kama msingi wa furaha na utulivu wa kihisia.

Hata hivyo, utafiti mpya umeonyesha kuwa maisha ya useja yanaweza kuleta manufaa makubwa kwa maendeleo binafsi, ustawi wa kisaikolojia na kuridhika na maisha kwa ujumla.

Utafiti huo, uliochapishwa hivi majuzi kupitia mfululizo wa tafiti tatu zilizojumuisha majaribio na uchambuzi wa kumbukumbu za washiriki, uligundua kuwa watu wasio katika mahusiano ya kimapenzi hupata nafasi kubwa ya kujitambua, kujikuza na kushiriki katika uzoefu mpya unaoongeza ubora wa maisha yao.

Kwa mujibu wa watafiti, watu wanaochukulia useja kama fursa ya ukuaji binafsi huwa na kiwango kikubwa cha kuridhika na maisha yao.

Aidha, wanaripoti kutosheka kwa mahitaji yao ya kisaikolojia, furaha zaidi na hofu ndogo ya kubaki bila uwepo wa mpenzi.

Utafiti huo, uliopewa jina la Riding Solo: The Associations Between Singlehood Self-Expansion Potential, Self-Expansion Experiences, and Singlehood Outcomes, unaeleza kuwa zaidi ya asilimia 40 ya watu wazima hupitia kipindi cha maisha ya useja katika hatua mbalimbali za maisha yao.

Hii inajumuisha wale ambao hawajawahi kuingia katika ndoa au mahusiano ya kudumu pamoja na wale waliorejea kwenye useja baada ya talaka au kuvunjika kwa mahusiano.

Watafiti walibaini kuwa watu wanaochagua kwa hiari kubaki bila wachumba huwekeza muda mwingi katika taaluma zao, masomo, biashara, usafiri, michezo, burudani na mahusiano ya kifamilia.

Wengi wao huchukulia shughuli hizi kama njia ya kujenga maisha yenye maana na mafanikio.

Miongoni mwa shughuli zilizotajwa kuwa chanzo kikuu cha ukuaji binafsi ni mazoezi ya mwili, sherehe za kijamii, kujumuika na marafiki, kula nje, mafanikio ya kitaaluma, matamanio mbalimbali na safari za mapumziko.

Kinyume na dhana kwamba watu wasio na wachumba huishi maisha ya upweke, utafiti ulionyesha kuwa asilimia 83 ya washiriki walifanya shughuli zao za maendeleo binafsi wakiwa pamoja na watu wengine.

Marafiki walikuwa kundi kubwa zaidi la waliowasaidia, wakifuatiwa na wanafamilia, huku asilimia 18 pekee wakifanya shughuli hizo wakiwa peke yao.

Wanasaikolojia wanaeleza hali huu ni mchakato wa mtu kupanua maarifa, uzoefu na mtazamo wake wa maisha kupitia shughuli na mahusiano mbalimbali.

Ingawa tafiti nyingi zimehusisha mchakato huo na mahusiano ya kimapenzi, utafiti huu unaonyesha kuwa ukuaji huo unaweza pia kupatikana nje ya mapenzi.

Hata hivyo, watafiti waligundua kuwa watu wanaotamani kuingia katika mahusiano ya kudumu au wanaoamini kuwa furaha inapatikana tu kupitia mapenzi walikuwa na uwezekano mdogo wa kuona useja kama fursa ya maendeleo.

Kwa upande mwingine, watu wenye kiwango kikubwa cha kujiamini walionekana kufurahia zaidi maisha ya useja na kuona fursa nyingi za kujikuza.

Watafiti waliongeza kuwa matokeo hayo yalitokana na washiriki walio katika umri wa miaka ya 30 na 40, hivyo huenda yasiwakilishe kikamilifu uzoefu wa makundi yote ya watu wasio katika mahusiano.

Hata hivyo, utafiti huo unaibua mtazamo mpya kwamba maisha ya useja yanaweza kuwa kipindi muhimu cha ukuaji, mafanikio na kujitosheleza binafsi.