Habari za Kitaifa

Ruto akabiliwa na ugumu wa kuridhisha wapigakura wa Nyanza

Na RUSHDIE OUDIA, DOMNIC OMBOK September 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto anakabiliwa na kitendawili cha kuvutia uungwaji wa wapigakura wa Luo Nyanza, ikisalia miezi michache kabla ya uchaguzi mkuu 2027.

Kilichosawiriwa kama ishara ya umoja kabla ya ziara ya siku nne ya Rais Ruto eneo la Nyanza, kiligeuka upesi pale ushindani ulipochipuka pamoja na orodha ya matakwa kutoka kwa uongozi wa ODM.

Ujumbe kutoka kwa viongozi waliochaguliwa mashinani ulikuwa rahisi: wako tayari kumuunga kinara huyo wa Kenya Kwanza kuwania awamu ya pili naye awape maendeleo na nyadhifa za kisiasa.

Hata hivyo, ndani ya vifijo na nderemo, uhalisia mgumu unakabili eneo hilo ambalo bado linasaka mwelekeo wake kisiasa mwaka mmoja baada ya kifo cha Raila Odinga.

Matakwa ya viongozi yalijumuisha kuanzia mgao wa nusu kwa nusu (50-50) wa serikali hadi wadhifa wa naibu rais 2027, huku wengine wakisisitiza kuwa Nyanza isalie ngome ya ODM na kumwonya Ruto dhidi ya kuingilia makabiliano ya kisiasa eneo hilo.

Mkutano wa viongozi wa mashinani Jumapili ulifichua jinsi Rais anavyojaribu kujitosa kwenye siasa za Nyanza baada ya Raila, huku viongozi eneo hilo wakijitahidi kubuni masharti yao binafsi kwa ushirikiano kisiasa.

Ingawa kulikuwa na muafaka wa jumla kuhusu kuunga mkono Rais Ruto kuchaguliwa tena, masharti yanayohusiana na uungwaji mkono huo yalitofautiana pakubwa na kufichua mianya katika eneo ambalo mpangilio wake kisiasa umetikiswa na kifo cha Odinga.

Dan Nyibule, akizungumza kwa niaba ya vijana alitumia hotuba yake kushinikiza matakwa ya kwanza kisiasa kwamba ni sharti Nyanza izingatiwe kwa wadhifa wa naibu rais katika serikali ijayo.

“Eneo letu limetembea nawe katika safari hii na hivyo basi tunaamini tunastahili wadhifa wa Naibu Rais katika serikali ijayo. Ikiwa kuna mtu unafaa kuwazia kuhusu nafasi hii ni Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi,” alisema Nyibole.

Mwakilishi wa wanawake aliyezungumza katika kikao na Rais alitofautiana na kauli hiyo akihoji kuwa wanawake ni wengi na kwa hivyo wanafaa kuzingatiwa kwa wadhifa wa mgombea mwenza 2027.

Mdahalo huo ulitokota zaidi Waziri wa Fedha John Mbadi alipojitokeza kama mgombea wa ngazi za juu akitaja tajriba yake serikalini, bunge, upinzani na ODM.

Bw Mbadi vilevile alionekana kutangaza mapema azma ya kugombea 2032.