Habari za Kitaifa

Familia zaomboleza jamaa zao waliouawa kwa risasi mkutano wa Kindiki Embu

Na GEOGE MUNENE September 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

FAMILIA mbili katika Kaunti ya Embu zinaandaa mazishi ya wana wao wawili waliopigwa risasi wakati wa makabiliano kati ya vijana na polisi katika mkutano wa kisiasa uliohudhuriwa na Naibu Rais Kithure Kindiki Jumamosi iliyopita.

Mike Macharia, 23, alikuwa ameenda kucheza kandanda katika Shule ya Msingi ya Nembure, huku Moses Munene, 30, akiwa njiani kuenda kazini mjini Embu.

Wote walikumbana na ghasia zilizoibuka nje ya Uwanja wa Nembure.

Familia zao zinasema vijana hao hawakuwa sehemu ya makabiliano hayo na sasa zinataka maelezo kuhusu jinsi walivyopoteza maisha.

Mama ya Macharia, Charity Wanja, alisema mwanawe alikuwa mtoto wake wa pekee na alikuwa amejitahidi kumlipia masomo ili apate maisha bora.

Alisema Macharia alikimbia baada ya makabiliano kati ya vijana na polisi wa kutuliza ghasia kuzuka, lakini alipigwa risasi kwenye nyonga.

Wasamaria wema walimkimbiza katika Hospitali ya Rufaa ya Embu, ambako alifariki alipowasili.

“Mwanangu hakuwa miongoni mwa vijana waliokuwa wakipigana na polisi na alipaswa kuachwa. Maafisa waliomuua wanapaswa kufichuliwa na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria,” akasema Bi Wanja.

Alisema anatoka katika familia maskini na alifanya kazi kwa bidii kuhakikisha mwanawe anapata elimu.

“Nilikuwa nikifanya kazi kwa bidii kumsomesha mwanangu ili asiteseke kama nilivyoteseka. Kwa bahati mbaya, mwanangu aliuawa kabla hajamaliza masomo yake,” akaongeza.

Katika kijiji cha Gichugu, mama mwengine, Cecilia Wambeti, 58, alikuwa akiomboleza kifo cha mwanawe Munene, ambaye hufanya kazi kwenye karakana.

Bi Wambeti alisema mwanawe alikuwa ameondoka nyumbani saa moja asubuhi kuelekea kazini mjini Embu akiwa kwenye pikipiki.

Alikutana na vijana waliokuwa wakikimbia polisi na akaacha pikipiki yake kabla ya kuanza kukimbia.

Alipigwa risasi nyuma ya kichwa na kufariki papo hapo.

“Alipigwa risasi mgongoni na akapoteza maisha,” akasema.

Bi Wambeti alisema alijulishwa kuhusu kifo hicho akiwa nyumbani na baadaye akafika katika Hospitali ya Rufaa ya Embu, ambako aliambiwa aende katika chumba cha kuhifadhi maiti.

Familia hiyo pia haijapata pikipiki ya Munene tangu tukio hilo.

“Tulienda eneo la tukio lakini hatukupata pikipiki. Polisi watuambie iko wapi,” akasema.

Alimtaja mwanawe kuwa mtu mwenye bidii na mkarimu aliyekuwa akimsaidia kifedha.

“Mwanangu alikuwa mchangamfu na mkarimu. Nilipohitaji pesa za chakula na mahitaji mengine, alikuwa akinisaidia. Nimepoteza mtoto mzuri,” akasema.

Wambeti alishangaa kwa nini mwanawe alipigwa risasi ilhali, kwa mujibu wake, hakuwa miongoni mwa vijana waliokuwa wakikabiliana na polisi.

Ghasia hizo zilizuka wakati Prof Kindiki alipokuwa akihutubia maafisa wa UDA katika Uwanja wa Nembure, Manyatta.

Vijana waliokuwa nje ya uwanja walipiga kelele na kurusha mawe, hali iliyosababisha polisi wa kutuliza ghasia kuingilia kati.

Makabiliano hayo yalidumu kwa saa kadhaa na magari sita yakachomwa moto.