Habari za Kitaifa

Alitusaidia kifedha, msamehe, wazazi wa Sharon warai korti kuhusu Obado

Na SAM KIPLAGAT September 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAZAZI wa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Rongo aliyeuawa kinyama, Sharon Otieno, wameomba Mahakama Kuu imsamehe aliyekuwa Gavana wa Migori Okoth Obado na kumpa adhabu isiyohusisha kifungo gerezani.

Douglas Zacharia Otieno na Melida Auma waliwasilisha ombi hilo mbele ya Jaji Cecilia Githua wakati wa hatua ya kumpa Obado adhabu baada ya kupatikana na hatia ya kumuua binti yao.

Wazazi hao waliomba mahakama izingatie mazingira yote ya kesi hiyo, ikiwemo mambo yanayoweza kupunguza au kuongeza uzito wa adhabu, kabla ya kutoa uamuzi.

Walisema licha ya maumivu makubwa yaliyosababishwa na kifo cha Sharon, wamechagua kumsamehe Obado na wanataka mahakama izingatie msamaha wao.

“Familia inamshukuru sana Mheshimiwa Jaji kwa kuhakikisha haki imetendeka kupitia hukumu ya kumpata na hatia. Hata hivyo, katika hatua hii muhimu ya kutoa adhabu, familia inaomba mahakama itumie busara yake kusawazisha haki na ombi la familia ya mwathiriwa,” walisema.

Sharon, aliyekuwa na umri wa miaka 26, alikuwa mwanafunzi wa mwaka wa pili katika Chuo Kikuu cha Rongo.

Alikuwa na ujauzito wa wiki 28 alipouawa kati ya Septemba 3 na 4, 2018, katika eneo la Owade, Homa Bay.

Alikuwa ametekwa nyara pamoja na mwanahabari ambaye alifanikiwa kutoroka.

Obado, aliyekuwa msaidizi wake wa kibinafsi Michael Oyamo na Caspal Obiero walipatikana na hatia ya kumuua Sharon mwezi Julai. Mahakama ilisema watatu hao walishirikiana na watu wengine ambao hawakufikishwa mahakamani kutekeleza mauaji hayo.

Katika ombi lao, wazazi walisema Sharon alikuwa tegemeo muhimu la familia na kifo chake kiliwaacha wakiwa wamevunjika moyo na pia katika hali ngumu kifedha.

Hata hivyo, walisema Obado alijitokeza baadaye kuwasaidia kifedha.

“Baada ya msiba huu, mshtakiwa wa kwanza (Obado) alifanya jambo la kipekee; alijitokeza na kusaidia familia na nyumba yetu kifedha. Hakufanya hivyo kwa amri ya mahakama, bali kwa hiari yake, akiongozwa na huruma na nia ya kuboresha hali ya maisha ya familia,” walisema.

Wazazi hao walisema msaada huo unafaa kuzingatiwa katika hatua ya kumwadhibu.

Walieleza kuwa wanataka haki ya kurekebisha madhara yaliyosababishwa na uhalifu huo izingatiwe, badala ya adhabu pekee.

“Tunaomba mahakama ikomeshe mzunguko wa maumivu. Tunaomba adhabu inayolenga kumrekebisha badala ya kulipiza kisasi pekee, na kumpa mshtakiwa wa kwanza nafasi ya kujirekebisha,” walisema.

Pia waliomba mahakama itumie Kifungu cha 23 cha Sheria ya Kulinda Waathiriwa na kuamuru fidia kwa familia pamoja na adhabu isiyohusisha kifungo.

Hata hivyo, waliomba uamuzi huo uzingatie maslahi ya umma, haja ya kuzuia uhalifu kama huo na miongozo ya kutoa adhabu.

Wazazi hao walisema wameishi na maumivu makubwa tangu Sharon alipouawa, wakieleza miaka iliyojaa machozi, kukosa usingizi na ndoto mbaya.

Walisema wanataka kufunga ukurasa wa tukio hilo na kuendelea na maisha baada ya miaka ya kupitia kile walichokiita kipindi kigumu zaidi katika maisha yao.

Ingawa walikiri uzito wa kosa lililotendwa, wazazi hao walisema hakuna anayeelewa ukubwa wa hasara yao kuliko wao wenyewe.