Wanaopinga kuongezewa muhula kwa Rais Tshisekedi wa DRC wanyakwa
KINSHASA, DR Congo:
POLISI nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) Jumanne waliwatia nguvuni waandamanaji katika miji kadhaa waliokuwa wakipinga mabadiliko yanayopendekezwa ya Katiba.
Wakosoaji wanahofia mabadiliko hayo yanaweza kumruhusu Rais Felix Tshisekedi kuwania muhula wa tatu.
Katika jiji kuu la Kinshasa, polisi walitumia vitoza machozi na kufyatua risasi hewani wakati ambapo maandamano yalikuwa yamechacha.
Maandamano hayo yaliitishwa na Muungano wa upinzani wa C64, unaohusishwa na waliokuwa wagombea urais Martin Fayulu, Moise Katumbi na Delly Sesanga.
Mamia ya watu walishiriki maandamano hayo Kinshasa, kulingana na yaliyonakiliwa na vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi.
Maandamano hayo yalikuwa yameidhinishwa na yalianza kwa amani, lakini vurugu ziliibuka kati ya waandamanaji na wafuasi wa serikali.
Pande zote zilitupiana mawe na baadhi ya waandamanaji wakaonekana wakiwa na mapanga, hali iliyosababisha polisi kuingilia kati.
Katika miji ya Lubumbashi na Uvira, maandamano yalipigwa marufuku na serikali za mitaa, lakini waandamanaji walijibwaga barabarani kabla ya polisi kuwatawanya.
Hii ni mara ya pili ndani ya miezi michache kwa C64 kuandaa maandamano dhidi ya mabadiliko ya Katiba.
Maandamano ya awali yaliyofanyika Kinshasa mwezi Juni yalivunjwa kwa nguvu na vikosi vya usalama.
Mvutano huo unatokea wiki tatu baada ya Rais Tshisekedi kutangaza mpango wa kuandaa mazungumzo ya kitaifa yatakayoleta pamoja vyama vya upinzani, mashirika ya kiraia na viongozi wa dini.
Hata hivyo, waasi wanaodhibiti maeneo ya mashariki mwa nchi hawakujumuishwa.
Tshisekedi amesema mazungumzo hayo yanalenga kushughulikia changamoto za kisiasa nchini humo.
Hata hivyo, vyama vya upinzani na Kanisa Katoliki wamepinga mabadiliko yanayopendekezwa ya Katiba.
Katiba ya DRC inasema mihula ya kuhudumu kwa rais huwa ni miwili ya miaka mitano kila mmoja.
Hata hivyo, Bunge lilipitisha mswada mnamo Juni unaoruhusu mabadiliko ya Katiba kupigiwa kura ya maoni.
Baadhi ya viongozi wa muungano unaounga mkono Tshisekedi wameunga mkono marekebisho ambayo yanaweza kumruhusu kuendelea kugombea urais.
Hatua hiyo imezua wasiwasi miongoni mwa wapinzani na taasisi za kidini kuhusu mustakabali wa demokrasia na utulivu wa kisiasa nchini humo.