Hali si shwari ndani ya Linda Mwananchi
MIVUTANO kuhusu madaraka na azma zinazokinzana za kisiasa miongoni mwa viongozi wakuu wa Linda Mwananchi imejitokeza hadharani, huku makundi tofauti yakionekana kuvutana kuhusu mwelekeo wa vuguvugu hilo kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Kiini cha mzozo huo ni kutoaminiana na mvutano kuhusu chama kitakachotumiwa na viongozi hao waliotoka ODM.
Uhasama huo mkali unashirikisha Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na wanasiasa ambao wapo katika kambi yao.
Kambi moja inayomuunga mkono Bw Owino inataka Bw Sifuna agombee urais kupitia chama kipya cha Mwananchi Party, ambacho bado hakijazinduliwa rasmi.
Kwa upande mwingine, Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya anataka Seneta huyo atumie Ukombozi People’s Party (UPP).
Bw Owino anadaiwa kupata Muungano Party, chama cha aliyekuwa Gavana wa Kitui Kivutha Kibwana, kwa ajili ya kukibadilisha kuwa Mwananchi Party.
Naye Gavana Natembeya anafanya mabadiliko katika United Democratic Party (UDP), iliyowahi kuhusishwa na marehemu Cyrus Jirongo, ili iwe UPP.
Mvutano huo umechangiwa zaidi na maslahi ya kieneo kati ya viongozi wa Nyanza na Magharibi, pamoja na tangazo la Gavana wa Siaya James Orengo kwamba anataka kuwania tiketi ya urais ya Linda Mwananchi.
Aidha, kuna swali kuhusu nani atakuwa kiongozi mkuu wa kisiasa wa vuguvugu hilo.
Kuibuka kwa Bw Sifuna kama kiongozi maarufu zaidi kumeripotiwa kuwakwaza baadhi ya viongozi wakuu wanaohisi wanapaswa kuwa na nafasi na ushawishi sawa.
Bw Owino alisema Jumanne kuwa mzozo huo unahusu zaidi chama cha kisiasa kitakachotumiwa katika uchaguzi wa 2027.
Alisema alipata chama mapema mwaka huu na alikuwa akipanga kukitumia kuwania ugavana wa Nairobi kabla ya Linda Mwananchi kuanzishwa.
Alisema awali yeye na wanachama wengine watatu walipewa jukumu la kutafuta chama. Mbunge wa Saboti Caleb Amisi alikuwa tayari ana chama, lakini baadaye alijiondoa baada ya kutofautiana na baadhi ya viongozi.
Bw Owino alisema alipomweleza Bw Sifuna kuhusu vyama hivyo viwili, Seneta huyo alimwambia hakukuwa na tatizo mradi kuwe na muungano, huku kila mmoja akiwa kiongozi wa chama chake.
Hata hivyo, alisema mvutano kuhusu chama cha kutumia bado unaendelea kuwatikisa.
“Baada ya hapo kumekuwa na kuvutana kuhusu chama atakachotumia. Nimeamua kwamba tuwe na chama kimoja, lakini ikiwa hilo haliwezekani, basi tuwe na muungano kwa sababu ni miungano ambayo imeshinda chaguzi nchini,” alisema.
Seneta wa Vihiga, Godfrey Osotsi, ambaye ni mshirika wa Bw Sifuna, alikutana na Bw Owino Jumatano katika juhudi za kusuluhisha tofauti hizo.
Hata hivyo, Bw Osotsi alipuuza ripoti za tofauti kubwa, akidai kuwa kuna juhudi za Serikali kuigawanya vuguvugu hilo kupitia propaganda.
Mbunge wa Funyula Oundo Midenyo alisema kuwa hakukuwa na makubaliano yoyote kuwa Bw Sifuna angetumia chama cha Owino.
“Bado tunaendelea kuafikiana lakini hakukuwa na muafaka wowote kwamba Sifuna atumie chama cha Owino,” akasema Bw Oundo.
Naye Mbunge wa Kabuchai Majimbo Kalasinga alihoji kwa nini Bw Owino hataki kumruhusu Bw Sifuna kuwa kiongozi wa chama chake ikiwa kweli anamuunga mkono katika azma ya urais.
Mvutano huo pia umeonekana katika mikutano ya Linda Mwananchi ambao vinara hao walikwepo wikendi.
Katika mkutano wa Jacaranda jijini Nairobi, maswali yaliibuka kuhusu itifaki baada ya Bw Owino kumwalika Bw Sifuna kuzungumza kwanza, badala ya kupewa nafasi ya mwisho kama kiongozi mkuu wa mkutano.
Mvutano mwingine ulionekana katika mkutano wa Kitale mwezi mmoja uliopita, ambapo Mbunge wa Bumula Wanami Wamboka alichukua kipaza sauti kutoka kwa Bw Owino akiwa bado anazungumza.
Aidha, kambi za Bw Orengo na Bw Sifuna zimeanza kutofautiana baada ya Gavana wa Siaya kutangaza azma yake ya kuwania urais, hatua ambayo iliwakasirisha baadhi ya wandani wa Bw Sifuna.