Maraga abuni muungano kushinikiza mageuzi IEBC, asema kuhesabu kura Bomas ni haramu
MUUNGANO unaoongozwa na aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga umetaka mageuzi makubwa kufanyiwa mchakato wa uchaguzi kabla ya kura za mwaka ujao na ukatishia kuongoza Wakenya kwenye maandamano iwapo mabadiliko hayo hayatafanywa.
Muungano huo, unaojulikana kama People’s Coalition on Electoral Reforms, umeibua mjadala mpya kuhusu maandalizi ya uchaguzi huku ukielekeza lawama kwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), Bunge na serikali.
Miongoni mwa mageuzi unaopendekeza ni kufutwa kwa kituo cha kitaifa cha kujumlisha kura za urais katika ukumbi wa Bomas, ukaguzi huru wa sajili ya wapigakura, kuongezwa kwa adhabu kali kwa makosa ya uchaguzi, kugatuliwa kwa matumizi ya mfumo wa teknolojia ya uchaguzi na mchakato wa wazi wa kuajiri maafisa wa IEBC.
Muungano huo unawaleta pamoja Maraga, Mbunge wa Saboti Caleb Hamisi, Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi, kiongozi wa Thirdway Alliance Ekuru Aukot na aliyekuwa Spika wa Bunge la Kitaifa Justin Muturi.
Akizungumza kwa niaba ya muungano huo, Maraga alisema mageuzi hayo lazima yatekelezwe kabla ya uchaguzi wa Agosti 2027 ili kuhakikisha uchaguzi unakuwa huru, wa haki, wenye uwazi na unaoaminika.
“Kenya haiwezi kumudu uchaguzi mwingine ambao uaminifu wake ni wa kutiliwa shaka. Ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007/2008 ni onyo la kitaifa ambalo hatuko tayari kulirudia,” alisema Maraga.
Muungano huo unasema suala la uaminifu wa uchaguzi wa 2027 si la kisiasa pekee bali ni jambo la maslahi ya taifa linalohitaji wahusika wote-wapigakura, wagombeaji, serikali, upinzani na wananchi kwa jumla.
Kwa mujibu wa Caroli Omondi, muungano huo unapinga kuwepo kwa kituo cha kitaifa cha kujumlisha kura za urais, ukisema Katiba inahitaji kura zihesabiwe na kutangazwa katika vituo vya kupigia kura na katika ngazi ya eneo bunge.
“Hakutakuwa na kituo cha kitaifa cha kujumlisha kura za urais kinachoendeshwa na IEBC au mwenyekiti wake katika Bomas au mahali pengine popote,” alisema Omondi.