Habari za Kitaifa

Kupinga matokeo ya urais kunahitaji ushahidi mzito zaidi, asema Jaji Ouko

Na JOSEPH WANGUI September 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WANAOPINGA matokeo ya uchaguzi wa urais lazima wathibitishe zaidi ya kuwepo kwa ukiukaji wa sheria au kasoro katika upigaji kura ili matokeo yaliyotangazwa yabatilishwe, Jaji wa Mahakama ya Juu William Ouko amesema.

Jaji Ouko alisema lazima wanaopinga matokeo hayo waonyeshe kuwa ukiukaji unaodaiwa uliathiri matokeo au uliharibu kwa kiwango kikubwa uadilifu wa uchaguzi kiasi kwamba mahakama haiwezi kwa njia yoyote ile kuunga mkono matokeo hayo.

Alisema hayo Jumanne wakati wa mhadhara wa umma katika Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Afrika Mashariki.

“Ni jukumu la mlalamishi kuthibitisha kuwa uchaguzi uliendeshwa vibaya sana na ukakumbwa na kasoro na ukiukaji wa sheria kiasi kwamba haijalishi nani alitangazwa mshindi. Yaani, uchaguzi ulikumbwa na kasoro nyingi ambazo kwa jumla ziliharibu kwa kiasi kikubwa uadilifu wa uchaguzi,” alisema.

Aliongeza: “Si kila ukiukaji wa sheria unaosababisha uchaguzi kutangazwa batili.”

Jaji Ouko alikumbusha kuwa kabla ya Katiba ya 2010, changamoto za matokeo ya urais zilikabiliwa na vikwazo vya kisheria na kiutaratibu.

Katika kesi ya mwaka wa 1997, kesi ya aliyekuwa mgombea wa urais Mwai Kibaki kupinga ushindi wa Rais Daniel arap Moi lilitupiliwa mbali kwa sababu Kibaki hakumfikishia Moi stakabadhi za kesi binafsi.

Kwa mujibu wa Jaji Ouko, uamuzi huo ulionyesha udhaifu wa mfumo uliokuwepo ambao haukuwezesha mzozo kuhusu uhalali wa mamlaka ya urais kushughulikiwa kikamilifu kwa misingi ya ushahidi.

Hali hiyo ilizidi kuwa mbaya baada ya uchaguzi wenye utata wa mwaka 2007 na ghasia zilizofuata. Tume ya Kriegler ilieleza wasiwasi kuhusu imani ya wananchi katika taasisi za uchaguzi na mahakama.

Jaji Ouko alisema mgogoro huo ulionyesha kuwa mizozo ya uchaguzi isipotatuliwa kupitia taasisi za kikatiba inaweza kuhamia uwanja wa kisiasa.

Katiba ya 2010 ilijibu changamoto hizo kwa kupatia Mahakama ya Juu mamlaka ya kipekee ya kushughulikia kesi zinazopinga uchaguzi wa urais.

Jaji Ouko alisema hatua hiyo ililenga kuhakikisha kuwa mzozo kuhusu kiti cha juu zaidi nchini unapata uamuzi wenye mamlaka na wa mwisho.

Kisheria, kesi ya kupinga matokeo ya urais lazima liwasilishwe ndani ya siku saba baada ya kutangazwa kwa matokeo.

Mahakama inapaswa kutoa uamuzi ndani ya siku 14, huku uchaguzi mpya ukifanyika ndani ya siku 60 endapo uchaguzi utabatilishwa.

“Hata hivyo, kufanya mambo kwa haraka hakufai kuchanganywa na pupa,” alisema Jaji Ouko, akisisitiza umuhimu wa kusawazisha kasi na haki ya kila upande kusikilizwa.

Alisema mzigo wa kisheria wa kuthibitisha madai hubaki kwa mlalamishi, ingawa mzigo wa kutoa ushahidi unaweza kuhamia upande mwingine pale mlalamishi anapowasilisha ushahidi wa kutosha unaohitaji majibu.