• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 2:10 PM
Shinikizo Rotich ang’atuke zazidi

Shinikizo Rotich ang’atuke zazidi

SAMWEL OWINO na CHARLES WASONGA

WAZIRI wa Fedha, Henry Rotich Jumatano alirejea tena katika Makao Makuu ya Upelelezi wa Jinai (DCI) kuhojiwa kuhusiana na sakata ya Sh21 bilioni ya mabwawa ya Arror na Kimwarer, huku shinikizo za kumtaka kujiuzulu zikiendelea kutolewa.

Jana, Mbunge wa Alego Usonga, Samuel Atandi alimtaka Rais Uhuru Kenyatta kumfuta kazi waziri huyo ikiwa waziri huyo hatajiuzulu kwa hiari yake.

“Nataka kumhimiza Rotich kujiuzulu kutokana na sakata hii. Na jinsi nilivyomhimiza Rais Uhuru Kenyatta amfute kazi Bw Rashid Echesa kama Waziri wa Michezo, nataka kumhimiza kumpiga kalamu Bw Rotich ikiwa waziri huyo hatasikiza miito ya viongozi na kujiuzulu,” Bw Atandi akasema.

Akiongea na wanahabari jana katika majengo ya bunge, Mbunge huyo alidai ana habari kwamba Bw Rotich alitumia kampuni moja kwa jina HEKIRO kununua ardhi katika bonde la Kerio kwa kutumia raia wa Italia kama wakurugenzi.

“Walinunua ardhi hiyo kwa Sh1 bilioni na baada ya miezi michache, wakauza ardhi hiyo hiyo kwa serikali kwa Sh6.3 bilioni. Baadaye, Bw Rotich alihakikisha pesa hizo zimetengwa katika bajeti. Alifahamu barabara kwamba alikuwa akiilaghai serikali ambayo anapaswa kulinda mali yake,” Bw Atandi akadai.

Kulingana na Mbunge huyo wa ODM, hatua ya Bw Rotich ya kutenga pesa za ununuzi wa ardhi ambako mabwawa hayo yangejengwa ilikuwa ni sawa na kutumia vibaya mamlaka ya afisi yake.

“Sharti Bw Rotich afutwe kazi. Yeye ndiye mhusika mkuu katika sakata hii ya mabwawa. Alihusika moja kwa moja katika uporaji wa pesa za umma.

Bw Atandi alisema Wakenya waliamini madai kuwa hakuna pesa zilizopotea katika sakata hiyo. “Mabilioni ya pesa ziliibiwa na wahusika sharti waadhibiwe.”

“Huu ni uporaji wa rasilimali za kitaifa katika kiwango cha sakata za Goldenberg na Anglo Leasing,” Bw Atandi akasema.

Mbunge huyo alisema ni makoa kwa watu fulani kumshika Rais Kenyatta mateka kwa kisingizio kwamba anapaswa kuwalipa deni fulani la kisiasa.

“Rais asikubali kushikwa mateka na watu kama hawa kwa sababu alikula kiapo cha kulinda na kutetea katia pamoja na sheria zote za Kenya.

Mnamo Jumanne Bw Rotich alihojiwa kwa zaidi ya saa 10 ambapo duru zinasema alikabiliwa na wakati mgumu kujibu maswali 300 kuhusu jinsi kampuni moja ya Italia ililipwa mabilioni ya fedha, hata kabla ya kuanza kazi ya kuchimba mabwawa.

You can share this post!

Wazee watishia kwenda kortini kupinga mpaka wa kaunti ndogo

Demu mfyonzaji atemwa na sponsa

adminleo