• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
JAMVI: Sababu ya Uhuruto kufurahia ukaidi wa Raila kwa urais wao

JAMVI: Sababu ya Uhuruto kufurahia ukaidi wa Raila kwa urais wao

Na MWANGI MUIRURI

Kifupi:

  • Moses Kuria asema “sisi hatuna presha kwa kuwa Odinga anatumalizia mambo yetu ya 2022.”
  • Upinzani wa Odinga huwaweka wafuasi wa Jubilee wakiwa chonjo kwa kila hali na ambapo bora tu anaendelea kubishana, huwa anasaidia ngome muhimu za Jubilee kujitokeza kujisajili kama wapiga kura
  • Mlima Kenya hufurahia juhudi na uaminifu wa Ruto kwa Uhuru Kenyatta, na ndizo humwezesha ‘mtu wao’ kujinasua katika mtego wa Odinga
  • Bw Odinga angekuwa na wa kumshauri vilivyo, angetambua hawa wawili walio mamlakani kwa sasa, “lakini azidishe njama zake za kuangazia ufisadi ambao ni utamaduni wa Jubilee

WANDANI wa Jubilee wameelezea furaha yao kutokana na harakati za kinara wa chama cha ODM, Bw Raila Odinga za kutotambua urais wa Uhuru Kenyatta kwani kwa kufanya hivyo anaendelea kumjenga Naibu Rais William Ruto katika urithi wa Ikulu 2022.

Furaha yao inatokana na ukweli kuwa Jubilee imejengwa katika msingi wa makabila mawili yanayosakini ngome mbili kuu; Mlima Kenya (Gema) na Rift Valley (Kamatusa) ambapo katika kutotambua kwake Rais Kenyatta, upinzaani unazidi kuimarisha umoja wa ngome za Rais na naibu wake.

Katika hali hiyo, mchanganuzi wa siasa kutoka Mlima Kenya, Peter Kagwanja anasema “ukitaka taifa lote lilegeze misimamo mikali ya kuegemea Jubilee au muungano wa Nasa, itambidi Waziri Mkuu wa zamani atambue urais wa Kenyatta.”

Anasema kuwa hilo litawatuma wafuasi wa Nasa nje ya siasa za ukaidi na uasi huku nao wafuasi wa Jubilee wakiingiwa na mtazamo mpana wa kuanza kudai huduma bora kutoka kwa serikali yao badala ya kuitetea hata inapokosea.

Waziri wa Kilimo Mwangi Kiujuri akiwa katika hafla ya kikazi katika Kaunti ya Laikipia alifichua kuwa “wacha Odinga aendelee kupambana na UhuRuto akisema hawatambui lakini sisi kimyakimya tunajua kwamba anatujenga kwa kuwa anatupa ile motisha ya kuikinga serikali yetu”.

Kiunjuri alisema kuwa hadi sasa ni bayana kuwa mrengo wa Nasa uko katika hatari ya kusambaratika na harakati za Odinga ni mojawapo ya vichocheo hivyo vya uhasama ndani ya vyama tanzu ndani ya muungano wake.

“Akiendelea hivyo na akose kuelewana na vyama tanzu ndani ya Nasa, ina maana kuwa uchaguzi wa 2022 tutaingia tukiwa na uwezekano mkubwa wa kuwa na mrengo mwingine ndani ya Nasa, ugawe kura za Nasa na Ruto aibuke na ushindi wa zaidi ya asilimia 70,” akasema.

Aliwataka wenyeji wamuombee Odinga aendelee na mkondo wake wa sasa wa siasa “ili aendelee kuvurugika huku sisi tukiwa imara bila mawazo mengi”.

Naye mbunge wa Gatundu Kusini Moses Kuria akihutubu katika mazishi ya Esther Nyaruai Wachira ambaye ni dadake mwakilishi wa wanawake wa Nyeri, Winnie Mukami, alisema kuwa “sisi hatuna presha kwa kuwa Odinga anatumalizia mambo yetu ya 2022.”

Alisema jinsi anavyoendelea kuhangaika akisaka kura ya 2017 iandaliwe tena kabla ya Agosti 2018, ndivyo anavyotupa shinikizo za dhati za kuendelea kuunga mkono hawa wetu ambao tulijichagulia. Anasema kila siku ya Odinga akiwa katika siasa za ukaidi na uasi ni siku ya kampeni kwa Jubilee na njama yake ya 2022 ya kumpa urais Ruto.

 

Ghasia za 2007

“Sisi tunajua hatari ya kusambaratika kama Jubilee. Tunajua kuwa tumewekeza si haba katika mikakati ya kuleta amani kati ya jamii zetu ambazo zilikuwa zinazozana kisiasa na kutumbukia katika ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007.

Kila harakati za Odinga ambazo zinaangazia njama ya kuturejesha katika hali hiyo ya ghasia ni baraka kwetu kwa kuwa tutazidi kuwa pamoja ili tumfungie nje,” akasema.

Naye mwakilishi wa wanawake wa Murang’a, Bi Sabina Chege anasema “Odinga amekuwa baraka kwetu katika msukumo wake wa siasa za upinzani.

Jinsi arukavyo juu akilenga kutuangamiza kisiasa, ndivyo sisi humngojea arejee chini tukiwa ngome thabiti.”

Anasema kuwa hali hiyo ya upinzani wa Odinga huwaweka wafuasi wa Jubilee wakiwa chonjo kwa kila hali na ambapo bora tu anaendelea kubishana, huwa anasaidia ngome muhimu za Jubilee kujitokeza kujisajili kama wapiga kura na pia kupiga kura katika siku ya uchaguzi.

Bi Chege anatoa mfano wa jinsi idadi Mlima Kenya na Rift Valley zilipendeza katika usajili na upigaji kura, lakini kujiondoa kwa Odinga katika kura ya marudio ya Oktoba 26 kukapunguza idadi hizo.

 

Kumwandama debeni

“Msingi wetu wa dhati ni kuwa, bora tu Odinga ana makali yake ya kisiasa, huwa anatufaa zaidi katika kuwasukuma wafuasi wetu kuwajibikia vita vya kumwandama ndani ya debe kupitia upigaji kura wa uhakika,” asema.

Mchanganuzi wa siasa, Prof Ngugi Njoroge anasema kuwa “Mlima Kenya na Rift Valley pamoja na jamii zingine ambazo hujihusisha na mpangilio huo wa kisiasa ungependa zaidi Odinga azidishe makali yake ya upinzani hadi 2022, ashindwe na kwa uhakika awe sasa amewakoma Jubilee.

Anasema kuwa ikiwa Odinga ataendelea na mkondo wake wa sasa wa kupinga ushindi wa rais Kenyatta, ako na hatari ya kutumiwa na Jubilee kuwa kama mwandani wao wa kimikakati “ambapo ataendelea kuwaweka wafuasi hawa katika ngome zao za kikabila wakiwa wameungana.”

Anasema Mlima Kenya hufurahia juhudi na uaminifu wa Ruto kwa Uhuru Kenyatta, na ndizo humwezesha ‘mtu wao’ kujinasua katika mtego wa Odinga.

“Kwa hilo, Mlima Kenya huendelea kukwamilia dhana kuwa wana deni kwa ngome ya Ruto ambayo ingekuwa haikujiunga na Uhuru, basi 2013 rais angeishia kuwa Odinga na apate awamu ya pili 2017,” asema.

 

Kuunganisha Mlima Kenya na Rift Valley

Katika hali hiyo, Prof Njoroge anasema kuwa “hakuna cha kupendeza Ruto na Uhuru kuliko kumwona Odinga akiendelea mbele na kuwakosea heshima wakiwa mamlakani kwa sasa kwa kuwa kufanya hivyo kuna baraka zake katika kudumisha Mlima Kenya na Rift Valley pamoja.

Mhathiri wa somo la kisiasa, Gasper Odhiambo anasema kuwa mtazamo huo umegonga ndipo kwa kuwa “Odinga huwa ni mwaathiriwa wa mbinu mbovu za kisiasa”.

Anasema kuwa Odinga angekuwa na wa kumshauri vilivyo, angetambua hawa wawili walio mamlakani kwa sasa, “lakini azidishe njama zake za kuangazia ufisadi ambao ni utamaduni wa Jubilee na katika hali hiyo ajipange upya katika kuunda muungano mwingine.”

Anasema kuwa kwa sasa kile Jubilee inadhaniwa kufanya ni kumtenga Odinga aonekane kama aliye tu na upinzani kwa Jubilee, “huku ikidaiwa kuwa inagawa pesa kama njugu kwa vyama tanzu vya Nasa kwa nia ya kuvunja muungano huo.”

 

Mhaini

Katika hali hiyo, Odhiambo anasema kuwa Odinga anabakia tu kuwa “mhaini wa kisiasa kwa Mlima Kenya na Rift Valley, huku ngome za washirika wake ndani ya kabila zao wakionyeshwa kuwa kuwekeza kwa Odinga ni kujihakikishia hasara ya kura 2022, lakini kukerwa na Odinga kuendelee kuweka ngome za Jubilee za sasa pamoja.”

Odhiambo anasema kuwa “wazo la busara kwa Odinga hadi sasa ni ajipange kama upinzani ambao alizindua kupitia kuapishwa kwake kama rais wa wananchi na hatimaye aanze harakati za uhakika za kulenga wandani wa Jubilee ambao daima hawatawahi kujiuzuia kupora uchumi wa taifa.”

Anaeleza kuwa wakati Odinga anaangazia ufisadi ndani ya “hizi serikali za jamii za ukiritimba wa urais, ndivyo hujivunia umaarufu katika maeneo yote ya hapa nchini.”

Anasema kuwa Odinga ni mwaniaji anayependeza ngome zote lakini wapinzani wake ni wale tu wa kupendeza vijiji vyao na ambapo huviunganisha kuzua kura ya ushindi.

 

‘Ufisadi ni utamaduni wa Jubilee’

Anaongeza kuwa Odinga angekuwa na wa kumshauri vilivyo, angetambua hawa wawili walio mamlakani kwa sasa, “lakini azidishe njama zake za kuangazia ufisadi ambao ni utamaduni wa Jubilee na katika hali hiyo ajipange upya katika kuunda muungano mwingine.”

Kwa sasa kile Jubilee inadhaniwa kufanya ni kumtenga Odinga aonekane kama aliye tu na upinzani kwa Jubilee, “huku ikidaiwa kuwa inagawa pesa kama njugu kwa vyama tanzu vya Nasa kwa nia ya kuvunja muungano huo.”

Katika hali hiyo, Odhiambo anasema kuwa Odinga anabakia tu kuwa “haini wa kisiasa kwa Mlima Kenya na Rift Valley, huku ngome za washirika wake ndani ya kabila zao wakionyeshwa kuwa kuwekeza kwa Odinga ni kujihakikishia hasara ya kura 2022, lakini kukerwa na Odinga kuendelee kuweka ngome za Jubilee za sasa pamoja.”

Odhiambo anasema kuwa “wazo la busara kwa Odinga hadi sasa ni ajipange kama upinzani ambao alizindua kupitia kuapishwa kwake kama rais wa wananchi na hatimaye aanze harakati za uhakika za kulenga wandani wa Jubilee ambao daima hawatawahi kujiuzuia kupora uchumi wa taifa.”

 

 

You can share this post!

JAMVI: Dhamira fiche ya Uhuru kuzuia wabunge wa Jubilee...

Joho achemsha Wiper kuhusu kiapo

adminleo