• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 4:28 PM
Manchester City juu ya EPL, Spurs na Blues wapaa

Manchester City juu ya EPL, Spurs na Blues wapaa

Na MASHIRIKA

MANCHESTER, Uingereza

WENYEJI Manchester City, Tottenham Hotspur na Chelsea walitumia ardhi yao vyema kutia kapuni alama tatu kwenye Ligi Kuu, Jumatano.

City ya kocha Pep Guardiola ililipua Cardiff 2-0 kupitia mabao ya wachezaji Kevin De Bruyne na Leroy Sane na kufungua mwanya wa alama moja juu ya jedwali dhidi ya wapinzani wao wa karibu Liverpool kwa kuzoa alama 80.

Guardiola ambaye timu yake itamenyana na Brighton katika nusu-fainali ya Kombe la FA hapo Jumamosi, alifanyia kikosi chake mabadiliko sita akipumzisha wachezaji muhimu akiwemo Sergio Aguero, ingawa alimtumia Gabriel Jesus.

Raia wa Brazil, Jesus alikosa nafasi kadha muhimu dhidi ya vijana wa Neil Warnock ambao wanakodolea macho kupoteza nafasi yao kwenye Ligi Kuu kwa sababu wako katika mduara hatari wa kutemwa.

De Bruyne alipachika bao lake la kwanza baada tu ya dakika tano akipokea pasi safi kutoka kwa Aymeric Laporte kabla ya Sane kuimarisha uongozi huo baada ya kumegewa krosi tamu na Riyad Mahrez zikisalia sekunde chache kipindi cha kwanza kitamatike.

Liverpool itakuwa uwanjani kuzichapa dhidi ya Southampton leo kwa hivyo uongozi wa ligi hii ya klabu 20 huenda ukabadilika vijana wa Jurgen Klopp wakishinda.

Spurs nambari tatu

Tottenham, ambayo Mkenya Victor Wanyama anachezea, ilimaliza ukame wa mechi tano bila ushindi kwa kupepeta Crystal Palace 2-0 kupitia mabao ya Son Heung-min na Christian Eriksen katika kipindi cha pili katika uwanja wao mpya wa Tottenham Hotspur.

Ushindi huu ulirejesha vijana wa Mauricio Pochettino katika nafasi ya tatu wakisukuma Arsenal nafasi moja chini hadi nambari nne.

Baada ya mechi, raia wa Argentina, Pochettino alidai kwamba klabu yake sasa ni “Washindi wa Kombe la Dunia” kwa sababu ya vifaa katika uwanja mpya na kutaka vijana wake waandikishe matokeo sawa na uwanja huo wa kisasa.

Naye Maurizio Sarri aliwasifu Callum Hudson-Odoi na Ruben Loftus-Cheek kama nyota wa siku zijazo wa Chelsea baada ya chipukizi hawa kuisaidia kulemea Brighton 3-0 uwanjani Stamford Bridge na kurukia nafasi ya tano iliyoshikiliwa na Manchester United.

Hudson-Odoi alimega pasi iliyofungwa na Olivier Giroud dakika ya 38 naye Loftus-Cheek akampa Eden Hazard pasi nzuri iliyozalisha bao la pili dakika ya 60. Loftus-Cheek alifungia Chelsea bao la tatu.

You can share this post!

Reds wazuru St Marys jicho likiwa kileleni

DOMO KAYA: Mbosso mshikaji wangu, kweli ungekuwa wakili tu

adminleo