• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:15 AM
TAHARIRI: Haki itendewe wote Turkana

TAHARIRI: Haki itendewe wote Turkana

Kituo cha utathmini wa mafuta cha Ngamia 1, Turkana. Picha/ Maktaba

Na MHARIRI

SUALA kuhusu ugawaji wa mapato yanayotokana na uchimbaji wa madini limekuwa likijadiliwa katika siku za majuzi. Sababu kuu ya mjadala huu mpya ni pendekezo kwenye Mswada unaopendekezwa kuhusu ugawanaji wa mapato hayo.

Kulingana na mapendekezo ya mswada huo, Serikali za kaunti zinapaswa kupata asilimia 15 huku jamii za maeneo kunakochimbwa madini zikipata asilimia tano. Sehemu nyingine ya asilimia 80 inafaa kwenda kwa Serikali.

Mapendekezo hayo ni kinyume na mswada wa 2016, ambao haukutiwa sahihi, uliopendekeza asilimia 20 kwa serikali husika ya kaunti na asilimia 10 kwa jamii.

Wale wanaopinga mswada mpya wanaonelea kuwa kaunti na jamii husika wameonewa kwa kupunguziwa mgao wao. Wale wanaoshikilia maoni haya wana kila sababu ya kuchukua msimamo huo.

Hii ni kwa sababu jamii yoyote ile inafaa kupata manufaa kutokana na raslimali inayopatikana mahala wanapoishi.

Jamii ambayo zaidi inahusika katika suala hilo ni ya kaunti ya Turkana, ambako kumegunduliwa kiasi kikubwa cha mafuta.

Ugunduzi huu ulipotangazwa ulileta matumaini makubwa kwa wakazi wa Turkana, kuwa hatimaye wamejaaliwa raslimali ambayo itakuwa chombo cha kuwatoa kwenye matatizo na umaskini, ambao wamekuwa nao kwa miongo na miongo.

Sehemu kubwa ya Turkana ni kame, jambo ambalo limefanya wakazi wake kutegemea zaidi ufugaji. Hata hivyo, ufugaji huo mara kwa mare umekuwa unatatizwa na ukame. Hivyo kupatikana kwa mafuta katika kaunti yao kulitarajiwa kusaidia kubadilisha hali ya maisha ya wakazi.

Ingawa raslimali zote ni za kitaifa, ni makosa kwa Serikali Kuu kujitengea sehemu kubwa ya mapato na kupunguza inayofaa kufika mashinani ili kunufaisha jamii inayoishi sehemu husika. Usawa unafaa kuwepo ili wakazi hao nao wafurahie matunda ya raslimali zao.

Kile Serikali ingefanya ni kushikilia pendekezo la awali la asilimia 20 kwa kaunti na 10 kwa jamii husika. Hatua ya kupunguza mapato yanayofika mashinani inatoa picha mbaya, kwani inaonekana kama serikali haijali maslahi ya jamii zinazoishi maeneo yenye madini.

Tunaomba Serikali kutathimini upya pendekezo lake na kuhakikisha kuwa haki inatendewa wakazi wa Turkana na maeneo mengine yenye raslimali za madini.

You can share this post!

Kanisa alimozikwa Yesu lafungwa

SHANGAZI: Nilimfumania ndani ya gari akigawa asali....

adminleo