• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Western Bulls na Kisumu warejea ‘meza ya wanaume’

Western Bulls na Kisumu warejea ‘meza ya wanaume’

Na GEOFFREY ANENE

WANARAGA wa Western Bulls na Kisumu wamerejea katika Ligi Kuu baada ya kunyakua tiketi kwa kushinda mechi za nusu-fainali za Ligi ya Daraja ya Pili, Jumamosi.

Bulls kutoka Kaunti ya Kakamega, ambayo ilitemwa 2016-2017, imechabanga Chuo Kikuu cha USIU kutoka Nairobi kwa alama 22-16.

USIU, ambayo pia iliwahi kushiriki Ligi Kuu miaka 11 iliyopita, iliongoza 6-0 kabla ya Bulls kupata mguso na mkwaju na kuongoza 7-6 wakati wa mapumziko. Bulls iliimarisha uongozi wake kipindi cha pili kilipoanza hadi 17-6.

Hata hivyo, USIU ilirejea dakika za mwisho na kupunguza mwanya huu hadi alama moja 17-16 kabla ya Bulls kujiwekea nafasi ya kupumua kupitia mguso kutoka kwa Miller Oroto.

Kisumu kutoka Kaunti ya Kisumu, ambayo ilishiriki Ligi Kuu mara ya mwisho msimu 2013-2014, ilirejea baada ya kuzima timu nyingine ya zamani wa Ligi Kuu, Catholic Monks kwa alama 14-11 katika muda wa nyongeza baada ule wa kawaida kumalizika 11-11.

Monks ilitemwa kutoka Ligi Kuu mwisho wa msimu 2014-2015.

Bulls na Kisumu zinachukua nafasi za Mean Machine ya Chuo Kikuu cha Nairobi na Leos ya Chuo Kikuu cha Strathmore zilizoshushwa ngazi baada ya kumaliza msimu huu wa 2018-2019 katika nafasi mbili za mwisho.

You can share this post!

Polisi wavunja kambi ya MRC na kunasa silaha msituni

Afisi ya Rais yatengewa pesa ambazo ‘tayari...

adminleo