• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 10:15 AM
Ukambani walia matunda ya handisheki hayajawafikia

Ukambani walia matunda ya handisheki hayajawafikia

Na PIUS MAUNDU

SIKU chache baada ya kiongozi wa ODM kuzindua miradi kadhaa katika ngome yake ya Nyanza kutokana na muafaka kati yake na Rais Uhuru Kenyatta, baadhi ya viongozi wa Ukambani sasa wanalalamika kuwa eneo hilo halijafaidi kutokana na maelewano hayo.

Hii ni licha ya kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka kutangaza kuwa anaunga mkono handisheki hiyo na kuahidi kufanya kazi kwa karibu na Rais Kenyatta.

Gavana wa Kitui Charity Ngilu na Seneta wa Makueni Mutula Kilonzo Junior wanasema kuwa Ukambani wamefaidi kwa kiwango kidogo zaidi kutokana muafaka huo ikilinganishwa na Nyanza.

“Mbali na watu wetu wachache kuteuliwa katika nyadhifa ndogo serikalini, eneo hilo halijavuna matunda yoyote kimaendeleo licha ya kushirikishwa katika handisheki,” Bi Ngilu akasema Jumamosi.

Aliunga mkono kauli ya Seneta Kilonzo Junior kwamba uteuzi wa baadhi ya wanasiasa kutoka Ukambani walioshindwa katika uchaguzi uliopita katika mashirika ya serikali una faida finyu zaidi kwa jamii ya eneo hilo.

Katika teuzi zilizofanywa na Rais Kenyatta, juzi wabunge kadhaa wa zamani kutoka eneo hilo walipewa nafasi katika mashirika ya serikali.

Baadhi yao ni; aliyekuwa mbunge wa Kibwezi Magharibi Kalembe Ndile, Kisoi Munyao (Mbooni), aliyewania kiti cha Mwingi Magharibi Mwende Mwinzi, aliyewania ugavana wa Machakos Wavinya Ndeti na aliyekuwa Gavana wa Kitui Julius Malombe.

“Hii handisheki ya kumwezesha mtu kupokea mshahara haina maana yoyote. Tunataka kusherehekea kuanzishwa kwa miradi kama Konza City na Bwawa la Thwake kwa sababu hiyo ni miradi ambayo italeta manufaa makubwa kwa jamii yetu,” akasema Bw Kilonzo Junior.

Walisema hayo katika Shule ya Msingi ya Yambae katika Kaunti ya Makueni wakati wa hafla ya mazishi ya aliyekuwa diwani wa Mbooni Joseph Musya na mwanawe, Steven Kyove.

Wawili hao walifariki katika ajali ya barabarani katika barabara ya Wote-Machakos majuma mawili yaliyopita. Shughuli hiyo pia ilihudhuriwa na Naibu Gavana wa Makueni Adelina Mwau na wabunge; Daniel Maanzo (Makueni), Patrick Makau (Mavoko) na Mbw Ndile na Kisoi.

Manung’uniko hayo kuhusu manufaa ya handisheki yanajiri wakati ambapo Bw MusyokA amekuwa akijitetea dhidi ya madai kuwa hakujali masilahi ya jamii yake alipotangaza kuwa atafanya kazi na Rais Kenyatta.

Gavana wa Makueni Prof Kivutha Kibwana ni miongoni mwa viongozi ambao wamemlaumu Bw Musyoka kwa kutopigania uanzishwaji wa miradi Ukambani wakati wa mazungumzo yake na Rais Kenyatta alivyofanya Bw Odinga.

You can share this post!

HISTORIA: Liverpool timu ya kwanza kuzoa pointi zaidi ya 90...

Tumesota, ODM sasa walilia ufadhili

adminleo