• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 6:55 AM
Handisheki haina maana bila mageuzi ya katiba – ODM

Handisheki haina maana bila mageuzi ya katiba – ODM

Na RUTH MBULA

VIONGOZI wa Chama cha ODM wamewapa Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wao Bw Raila Odinga makataa ya hadi Machi 2020 kuandaa kura ya maamuzi. Kulingana na viongozi hao waliojumuisha wakuu wa chama hicho, handisheki haitakuwa na maana yoyote ikiwa kura ya maamuzi haitafanywa kufikia wakati huo.

Walieleza wasiwasi wao kuwa kufikia sasa, Rais Kenyatta na Bw Odinga hawajaonyesha nia ya kuhimiza wabunge kujumuisha suala la kura ya maamuzi kwenye bajeti ya mwaka wa 2019/2020.

Vilevile, wametilia shaka hatua zinazopigwa na jopo maalumu lililoundwa na wawili hao kukusanya maoni ya wananchi kitaifa kuhusu marekebisho ya katiba.

Kwa kauli moja, Kiongozi wa Wachache katika Seneti James Orengo, Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa John Mbadi aliye pia Mwenyekiti wa ODM, na Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna walisema ni kura ya maamuzi pekee ambayo itadhihirisha kwamba handisheki ilikuwa ya kweli.

Viongozi hao walikuwa wakizungumza katika eneo la Rongo, Kaunti ya Migori walipokuwa wakiongoza mkutano wa kuchangisha fedha za kusaidia Kanisa Katoliki la St Martin De Pore.

“Ili kuonyesha kwamba handisheki kati ya Rais Kenyatta na Bw Odinga ilikuwa ya kweli, basi serikali haina budi kujumuisha kura ya maamuzi katika bajeti ya 2019/2020,” akasema Bw Orengo.

“Fedha za kuendesha kura ya maamuzi haziwezi kupatikana bila kuweka mipango kabambe. Ninachosema ni kwamba wabunge wanafaa kuongeza kura ya maamuzi katika bajeti ya mwaka wa fedha utakaoanza Julai mwaka huu,” akasema Bw Orengo.

Alisema Wakenya wanangojea kura ya maamuzi kwa hamu na ghamu na viongozi hawana budi kuwapa mwelekeo.

Bw Mbadi alimtaka Bw Odinga na Rais Kenyatta kuwahimiza wabunge kujumuisha kura ya maamuzi katika bajeti.

“Rais Kenyatta na Bw Odinga wanafaa kuwaagiza wabunge wao kuhakikisha kuwa fedha za kura ya maamuzi zinajumuishwa katika bajeti,” akasema.

Kwa upande wake, Bw Sifuna alisema: “Ninaomba kwa unyenyekevu mkubwa, Rais atende yale anayosema. Amekuwa akisema anataka kukomesha jinsi mshindi wa urais hunyakua mamlaka yote serikalini. Lazima tubadilishe mbinu zetu za kisiasa.”

Bw Odinga amekuwa akiwataka Wakenya kujiandaa kwa ajili ya mabadiliko ya katiba kupitia kura ya maamuzi.

Kwa upande mwingine, Rais Kenyatta hajatangaza wazi kuhusu kura ya maamuzi lakini matamshi yake katika hafla mbalimbali yanaashiria kwamba anaunga mkono mabadiliko.

Alipokuwa akihutubia Waislamu katika msikiti wa Jumia jijini Nairobi wiki jana, Rais Kenyatta alisema ni mabadiliko ya katiba pekee ambayo yatawezesha sherehe ya mwisho wa mfungo wa Ramadhan, Eid-Ul Fitr kuwa sikukuu ya kitaifa kila mwaka.

You can share this post!

MAPISHI: Muffins

Kiambu tayari kwa upanzi wa miti ulimwengu ukiadhimisha...

adminleo