• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 12:48 PM
Kirwa, Cheshari na Kosgei kushiriki Hannover Marathon

Kirwa, Cheshari na Kosgei kushiriki Hannover Marathon

Na GEOFFREY ANENE

WAKENYA Gilbert Kirwa, Jacob Cheshari na Recho Kosgei wameingia mbio za kilomita 42 za Hannover Marathon zitakazoandaliwa nchini Ujerumani mnamo Aprili 8, 2018.

Taarifa kutoka Shirikisho la Riadha duniani (IAAF) zinasema Kirwa ataanza kitengo cha wanaume kama mgombea halisi wa taji naye Mjerumani Fate Tola anapigiwa upatu kutetea ubingwa wa wanawake.

Kirwa na Tola pia wamepigiwa upatu kuvunja rekodi za Hannover Marathon za saa 2:08:32 (wanaume) na 2:27:07 (wanawake) zinazoshikiliwa na washindi wa mwaka 2013 Lusapho Aprili (Afrika Kusini) na Olena Burkovska (Ukraine).

Muda bora wa Kirwa ni saa 2:06:14 naye Tola anajivunia kutimka kasi ya juu ya 2:25:14.

Kirwa alinyakua mataji ya Vienna Marathon (Austria) na Frankfurt Marathon (Ujerumani) kwa saa 2:08:21 na 2:06:14 mwaka 2009, mtawalia.

Amekuwa akisumbuliwa na majeraha. Hajashiriki mashindano yoyote mwaka 2018. Mpinzani wake mkuu ni Cheshari, ambaye alishinda Hannover Marathon mwaka 2015 kwa saa 2:09:32.

Anajivunia muda wake bora wa saa 2:07:46 alioweka alipomaliza Frankfurt Marathon katika nafasi ya nne mwaka 2013. Raia wa Poland, Henryk Szost, ambaye anajivunia muda bora wa saa 2:07:39, hawezi kupuuzwa.

Tola, ambaye alibadili uraia kutoka Ethiopia hadi Ujerumani mwaka 2016, alishinda Hannover Marathon mwaka 2017 kwa saa 2:27:48. Alikosa rekodi ya Burkovska pembamba.

Kosgei, ambaye taji la Warsaw Marathon nchini Poland lilimponyoka akiona aliposhiwa nguvu zikisalia mita 800 mwaka 2017, na Mchina Yue Chao ni baadhi wa washindani wakuu wa Tola. Muda bora ya Chao na Kosgei ni saa 2:29:26 na 2:30:09, mtawalia.

You can share this post!

Magufuli apiga marufuku maandamano nchini mwake

Wanyama ashinda tuzo ya goli bora la Februari EPL

adminleo