• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
‘Vijana wanaofanya kulihali kuepuka maovu katika jamii wanastahili pongezi’

‘Vijana wanaofanya kulihali kuepuka maovu katika jamii wanastahili pongezi’

NA SAMMY WAWERU

UKOSEFU wa ajira miongoni mwa vijana nchini unanyooshewa kidole cha lawama kama njia mojawapo inayochangia visa vya uhalifu.

Vijana wanalalamikia kufungiwa nje katika nafasi za kazi licha ya serikali ya Jubilee kudai inaendelea kubuni ajira.

Wahalifu kuuawa hasa mijini, si suala geni asasi za usalama zinapoarifiwa ili kukabiliana nao.

Licha ya kwamba kuna wanaoshiriki uhalifu si kwa sababu ya kukosa kazi, ila ni mazoea, wengi wanadaiwa kuushiriki ili kuzimbua riziki.

Ni kutokana na hilo ambapo baadhi ya mashirika ya kijamii na yasiyo ya kiserikali yanajaribu kadri yawezavyo kushirikisha vijana katika gange, zingine zikiwa kutoa huduma bila malipo.

Kwa kufanya hivyo, yanawaepusha kushiriki maovu. Pia, baadhi ya mashirika yanawapendekeza kwa kampuni ili kupata ajira.

Mbali na kuhamasisha jamii kuhusu maambukizi ya Ukimwi na magonjwa ya zinaa, Kikundi cha Liberty na ambacho ni cha kijamii, pia kinajaribu kunasua vijana dhidi ya kushiriki uhalifu.

Paul Kahiro, mmoja wa waasisi wacho anasema kinalenga vijana wa kaunti ya Nairobi na Ruiru, Kiambu.

“Tumefanikiwa kubadili mienendo ya vijana kadhaa ambao awali walishiriki uhalifu. Kuna baadhi yao wameweza kuweka kazi,” anaeleza Bw Kahiro.

Kulingana na mwenyekiti Ezra Aswani, Liberty Group hutumia sanaa kama vile michezo ya kuigiza na kukariri mashairi yenye mada husika kupasha ujumbe na kuhamasisha jamii.

“Tunanoa vijana waliobadili mienendo kuvutia walioshikwa na minyororo ya matendo maovu. Waonapo wenzao wanaishi maisha huru na ya kujitegemea, wanayatamani na hawana budi ila kujiunga nasi,” anafafanua Bw Aswani.

Kando na mashirika ya kijamii, kuna wananchi wazalendo wanaotumia vipaji vyao kunusuru vijana. Jamal Njambe, kutoka kaunti ya Nyeri ni mmoja wao.

Historia ya kaunti hiyo ikiandikwa, jina la Bw Jamal halitakosa kujumuishwa kwa juhudi zake kudhibiti visa vya uhalifu katika mtaa wa Majengo, ambao awali uligonga vichwa vya habari kwa kukita mizizi uhalifu.

Barobaro huyu amekuwa akitumia sanaa kubadilisha mawazo ya vijana.

Ni mkufunzi wa michezo ya kuigiza na sarakasi, malenga na mwanamasumbwi hodari, na anatumia vipaji vyake kuwateka dhidi ya kushiriki matendo haramu.

Jamal pia ni muundaji hodari wa bidhaa za urembo na utanashati kwa kutumia shanga.

“Kwa muda wa miaka mitano sasa nimekuwa nikiwashirikisha katika sanaa zote nilizobobea. Furaha yangu ni kuona vijana wanabadili mienendo na tabia, na kujiimarisha kimaisha kwa kufanya kazi halali,” anaelezea.

Kazi ipo

Hata hivyo, juhudi za kukabiliana na visa vya uhalifu nchini si rahisi.

Waliofanikisha wanahoji safari hiyo inahitaji uvumilivu na uzalendo.

Ukosefu wa fedha za kutosha ni baadhi ya changamoto ambazo wazalendo waliojituma hukumbana nazo.

“Wakati mwingine tunalazimika kuchangana kama wanachama ili kusafiri mitaa tunayolenga,” anasema Paul Kahiro wa Liberty Group.

Kwa upande wake Jamal Njambe, anasema wakati mwingine hutumia mapato yake kugharimia lishe kwa vijana anaokomboa kutoka kwa minyororo ya uhalifu.

Lingekuwa jambo la busara kwa serikali kutambua wazalendo na makundi yanayobeba mzigo huo na kuwapiga jeki kifedha.

Madhehebu ya dini pia yanahimizwa kushirikiana nao kwa karibu ili kudhibiti visa vya uhalifu.

You can share this post!

‘Wanaotaka kura za Mlima Kenya watangaze ni jinsi...

KNCHR yapinga kupunguzwa kwa idadi ya makamishna wa IEBC

adminleo