• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 3:23 PM
AFCON: Kenya na TZ zapokea kichapo sawa

AFCON: Kenya na TZ zapokea kichapo sawa

Na GEOFFREY ANENE

HARAMBEE Stars ilianza kampeni yake ya Kombe la Afrika (AFCON) vibaya baada ya kuzimwa 2-0 dhidi ya Desert Foxes ya Algeria uwanjani 30 June jijini Cairo nchini Misri, Jumapili usiku.

Vijana wa kocha Sebastien Migne, ambao hawakuwa wamefungwa bao katika kipindi cha kwanza katika mechi saba, walikuwa chini mabao mawili kufikia wakati wa mapumziko baada ya Baghdad Bounedjah na nyota wa Manchester City kuona lango dakika za 34 na 43 mtawalia.

Bao la kwanza lilipatikana baada ya beki Dennis Odhiambo, ambaye ndiye mchezaji mwenye umri mkubwa katika timu ya Kenya (34), kuangusha Youcef Atal ndani ya kisanduku akijaribu kuondosha hatari.

Bounedjah alimwaga kipa Patrick Matasi kupitia penalti iliyopatikana. Matasi aliingia mechi akiwa na rekodi nzuri ya kupangua penalti mbili katika mechi za kirafiki wakati Kenya ilizaba Madagascar 1-0 Juni 7 jijini Paris nchini Ufaransa ilikokuwa imekita kambi na kutoka 1-1 Juni 15 dhidi ya DR Congo jijini Madrid nchini Uhispania.

Mwanasoka bora wa Afrika mwaka 2016 Mahrez, ambaye alikuwa mwiba sana kwa Wakenya, alifuma wavuni bao la pili baada ya Sofiane Feghouli kummgea pasi nzuri ndani ya kisanduku. Shuti lake liliguswa na Abud Omar na kupiga chenga kipa bora wa Kenya mwaka 2016 na 2017 Matasi.

Stars illingia mchuano huu wa Kundi C na ushindi mbili katika mechi tatu dhidi ya Algeria. Hata hivyo, rekodi hiyo ilisalia kuwa tu historia baada ya Algeria kutawala mechi, huku Stars ikipoteza mipira ovyo, kupiga pasi mbovu, kulegea katika ngome yake pamoja na kupata nafasi chache sana za kupata bao.

Ayub Timbe na Eric Johanna walikaribia kuona lango dakika za mwishomwisho za kipindi cha kwanza, lakini makombora yao yalijaa nje.

Kenya iliimarika katika kipindi cha pili hasa baada ya Mfaransa Migne kupumzisha kiungo Francis Kahata na kujaza nafasi yake na beki wa kupanda na kushuka Eric Ouma.

Hata hivyo, mabingwa hawa wa Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) walikosa ujuzi wa kufunga bao na kuishia kupoteza alama zote dhidi ya wafalme hao wa Afrika wa mwaka 1990.

Inaonekana Kenya iliingia mchuano huu kutafuta sare kwa sababu ilikuwa na shuti moja pekee kwenye goli dhidi ya tano za Algeria, ambayo pia ilimiliki mpira kwa asilimia 60. Kenya iliadhibiwa mara 28 ikiwemo Omar na Philemon Otieno kulishwa kadi ya njano kila mmoja dhidi ya ikabu 12 wa upande wa Algeria.

Kenya na Tanzania, ambazo zinarejea katika kombe hili baada ya kuwa nje miaka 15 na 39 mtawalia, zitalimana katika mechi ijayo hapo Juni 27.

Timu hizi zote zinauguza vichapo kwani Tanzania ilitangulia kupepetwa 2-0 na Senegal katika mechi ya kwanza ya kundi hili.

Taifa Stars ilizamishwa na magoli kutoka kwa Keita Balde dakika ya 28 na Krepin Diatta dakika ya 64. Timu mbili za kwanza kutoka makundi yote saba zitaingia moja kwa moja katika raundi ya 16-bora. Timu nne zitakazomaliza katika nafasi ya tatu zikiwa na alama nyingi pia zitaingia awamu hiyo.

You can share this post!

Ngome ya Rais Kiambu imechoshwa na handisheki – Kuria

UG yapiga Kenya na kupanda nafasi saba viwango vya raga

adminleo