• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 6:55 PM
AKILIMALI: Wafugaji waungana kuanzisha kiwanda chao cha maziwa

AKILIMALI: Wafugaji waungana kuanzisha kiwanda chao cha maziwa

NA RICHARD MAOSI

KUNA utajiri mkubwa humu nchini katika sekta ya uzalishaji na usambazaji wa maziwa, na wakati mwingine wananchi hushangaa kuona taifa likiagiza maziwa kutoka nje ilhali tuna mifugo wengi.

Hitaji la maziwa lipo, isipokuwa wakulima wengi bado hawana tajriba ya kujitengenezea bidhaa zinazotokana na maziwa.

Hii ndiyo maana Wizara ya Kilimo huwashauri kuwa makini, na kukabiliana na changamoto za ukame na soko la bidhaa hii adimu inayotumika na kila mtu.

Akilimali ilibahatika kutangamana na shirika la Sabatia Cooperative Society, Kaunti ya Baringo, muungano unaowasaidia wafugaji vijijini kupata soko la nje kwa maziwa yao.

Shirika hilo limeamua kuja na mfumo mpya wa kuyakusanya, kuhifadhi na kusambaza maziwa kwa ushirikiano na wafugaji wadogo.

Mwenyekiti wa shirika hilo Bi Rose Maiyo anasema walianzisha mradi huo ili kutengeneza nafasi nyingi za ajira kwa vijana, na wakulima wakubwa waliowekeza katika ufugaji wa ng’ombe wa maziwa.

Wenses Arap Sang (kushoto), mtaalamu wa maziwa akiyakagua kabla ya kuruhusiwa ndani ya vifaa maalum vya kuyahifadhi. Picha/ Richard Maosi

Pili walitaka kutangamana na wakulima moja kwa moja ili wawapatie ujuzi wa namna ya kujiongezea kipato pamoja na kutatua matatizo yanayowakabili.

Alieleza kuwa shirika la Sabatia lilitaka kuwaongezea wakulima kipato, mbali na kuwahimiza kuhusu umuhimu wa kutumia vifaa vya kisasa kuyahifadhi.

“Pindi wakulima walipoanza kutuuzia maziwa yao ,shirika la Sabatia lilianza kupata pesa na kukua,huku wakulima wakiendelea kufaidika,”Rose akasema.

Mbali na hayo shirika lenyewe limeweza kuwapatia wakulima nafasi ya kupata mbolea kwa bei nafuu,lishe bora ya mifugo na mafunzo kabambe ya kuimarisha ufugaji.

Baadhi ya wakulima husafirisha maziwa hadi kwenye viwanda wakitumia pikipiki. Picha/ Richard Maosi

Kwa siku moja shirika la Sabatia linaweza kukusanya kati ya lita 10,000-12,000 kutoka kwa wakulima vijijini.ambao mara nyingi hutumia pikipiki kuyasafirisha hadi Eldama Ravine kwenye kiwanda.

Kulingana na Rose shirika lao hutengeneza kati ya milioni 8-9 kila mwezi, jambo linalowafanya waendelee kujiongezea mtaji na kuwahudumia wakulima mashinani kwa kuwapatia mikopo na kuyaboresha mazingira ya ufugaji.

Rose anasema kuwa jambo la msingi ni kuwawezesha wakulima kuongeza thamani katika maziwa yao,na hili lilionekana pale walipoanza kuzalisha maziwa ya unga.

Isitoshe Sabatia wamefanikiwa kuanzisha duka la kijumla linalotengeneza Yoghurt,Cheese na maziwa ya mgando katika mji wa Eldama Ravine linalohudumia kaunti nzima ya Baringo.

Maziwa yakichujwa kabla ya kuruhusiwa ndani ya mtambo wa baridi. Picha/ Richard Maosi

“Hatua hizi zimesaidia kupanua uwanda wa soko na kuwatengenezea vijana nafasi za ajira ,wanaopata mkate wao wa kila siku katika sekta ya uzalishaji wa maziwa,”akasema.

Lakini kabla hawajanunua maziwa kutoka kwa mkulima hatua zifuatazo zinahitajika kuzingatiwa.

Kuyakagua maziwa

Kabla ya kuchukua maziwa kutoka kwa wakulima kipengele muhimu ni ukaguaji ili kubaini endapo maziwa ni halisia au la.SAnaamini kuwa kuna mabo mengi yanayoweza kufanya maziwa yaharibike.

Ubora wa maziwa unaweza kubainika kutokana na njia nyingi,njia moja ikiwa ni kutumia harufu ya maziwa. Endapo ng’ombe alipatiwa dawa nyingi kupita kiasi wakati wa matibabu dawa zinaweza kuadhiri maziwa.

Wesnas Arap Sang, mtaalamu wa maziwa akiyakagua kabla ya kuruhusiwa ndani ya mashine ya kudumisha baridi. Picha/ Richard Maosi

Pia mkulima anaweza kuwa mwangalifu kwa kuangalia rangi ya maziwa ambayo ni weupe uliosheheni .

“Mara nyingi wakulima wamekuwa wakiongezea maziwa yao maji,wakitarajia kuwapunja wanunuzi na kujiongezea kipato lakini teknolojia imefanikiwa kugundua hilo.”Rose aliongezea.

Anasema kwa kawaida kuna kipimo kinachofahamika kama lactometer,hiki ni kifaa kinachotumika kutambua kama maziwa yameongezewa maji au la.

Lactometer hutumbukizwa ndani ya maziwa, na kitaaluma kifaa hiki kinaweza kutenganisha mafuta maji na maziwa mazuri.

Kulingana na Lactometer maziwa yakiwa ni mazuri itasoma baina ya 1.026-1.036 tofauti na hapo basi maziwa yatakuwa yameonyezewa maji au kitu kingine.

Kwa kawaida ndani ya maziwa huwa kuna protini, mafuta, chumvi na sukari inayofahamika kama lactose.

Muuzaji maziwa akipewa ushauri. Picha/ Richard Maosi

Aidha Rose anatoa tahadhari akiwaeleza wakulima kulisha mifugo wao kwa kutumia majani makavu kwa wingi, badala ya yale mabichi kwani wakati mwingine kipimo kinaweza kuonyesha kuwa maziwa yameongezewa maji ingawa hayakuongezewa kitu chochote.

Kuyahifadhi maziwa yasiharibike

Kwa sababu maziwa yanaweza kuharibika haraka endapo yatahifadhiwa katika sehemu ya joto jingi,yanahitajika kuwekwa katika sehemu baridi pindi baada ya kukamuliwa.

Rose anaeleza kuwa kwa sababu maziwa yana virutubishi vingi sana bakteria waharibifu wanaweza kuzaaana kwa haraka na kuyaharibu maziwa ya mkulima.

Baadhi ya vijana walioajiriwa na shirika la Sabatia kutengeneza maziwa gururu. Picha/ Richard Maosi

“Iwapo maziwa yatakuwa na bakteria wengi yataharibika kwa urahisi,”alisema.

Aidha anaonya kuwa vifaa vya plastiki havifai kuhifadhi maziwa,kwa sababu hupatia maziwa harufu mbaya inayoweza kuyafanya yaharibike haraka.

Vifaa vya chuma kama aluminium visivyoweza kupata kutu ni mwafaka zaidi kutumika, ijapo katika swala la kuyalinda maziwa yasiharibike.

Maziwa yanapofika kwenye kiwanda hiki kwanza huchujwa na baadae, kusafirishwa hadi ndani ya cooling plants ambapo kiwango cha joto huwa kimepunguzwa.

Cooling plants hutumika kuhakikisha maziwa yanahifadhiwa katika sehemu safi , mbali na kupunguza kiwango cha joto ambacho kinaweza kufanya maziwa kuganda.

Huduma zinazotolewa na shirika la Sabatia ni pamoja na kuwauzia lishe pamoja na kuwapa ushauri. Picha/ Richard Maosi

Mtambo wenyewe umetengenezwa kwa chuma aina ya aluminium ambayo ina uwazi mkubwa wenye mzunguko wa hewa safi.

Maziwa yanahitajika kuhifadhiwa katika kiwango cha nyuzi joto zinazopungua sita hivi kabla ya maziwa mengine kuruhusiwa ndani ya mtambo wenyewe masaa manne baadae.

Kwa kutumia umeme wa stima, kiwango cha joto kinaweza kupunguzwa na kuongezwa sawia kulingana na muda unaotakiwa kuyahifadhi.

Kuyaongezea maziwa thamani

Kulingana na Rose kiwanda cha Sabatia kimegundua kuwa wakazi wengi kutoka kaunti ya Baringo ni wafugaji wa ng’ombe kwa ajili ya maziwa. Kwa hivyo, wanategemea mifugo kwa takriban kila kitu.

Pana haja kubwa ya kuboresha malisho ya ng’ombe,maji na utafiti wa mbegu za vidume wakati wa kutunga ujauzito ili kuendeleza kizazi.

Awali walikuwa wakikabiliana na changamoto za kupata soko kwa maziwa yao yaliyobaki kuharibikia majumbani pao, na hata wakati mwingine wakalazimika kuyamwaga.

Mwenyekiti wa shirika la Sabatia akionyesha taji alilopokezwa na serikali ya Kaunti ya Baringo kwa kuwawezesha wakulima wadogo mashinani. Picha/ Richard Maosi

“Kando na kuwashauri wakulima kufanya ufugaji unaostahili pia tunawapatia huduma za matibabu kwa mifugo wao ili kufanya ufugaji wenye tija.”akasema.

Sabatia wamefanikiwa kuanzisha duka la kijumla mjini Eldama Ravine wanakotengenezea maziwa ya mgando,cheese,ghee na yoghurt kama juhudi za kuongezea maziwa yao thamani.

Biashara hiyo imewasaidia vijana wengi kutoa msururu wa huduma za kuyasambaza na kujifungulia maduka yao ya kibinafsi katika kaunti nzima ya Baringo.

You can share this post!

Kioja cha mwaka kichwa cha mume kukwama ndani ya uke wa...

Chipu yaikomoa Brazil Raga ya Dunia U-20

adminleo