• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 5:55 AM
Serikali kupimia wazee hewa

Serikali kupimia wazee hewa

Na PAUL WAFULA

SERIKALI imewapimia hewa wafanyikazi wanaostaafu kabla ya kufikisha miaka 60 kwa kuwazima kupokea akiba yao yote ya pensheni.

Kulingana na kanuni mpya ya Serikali, wafanyikazi wanaostaafu sasa hawataweza kupokea mchango wa mwajiri wao kama ilivyo sasa hadi wafikishe miaka 60.

Awali, wafanyikazi wanaostaafu kabla ya kutimiza miaka 60 walipokea nusu ya mchango wa mwajiri pamoja na kiasi chao chote walichoweka kwenye akiba ya uzeeni.

Kanuni hiyo iliyotangazwa na Waziri wa Fedha, Henry Rotich, ni pigo kubwa kwa wale wanaofutwa kazi kabla ya umri wa kustaafu ama wanaotaka kuacha kazi ya kuajiriwa

“Inamaanisha kuwa sasa wafanyikazi hawataweza kupata akiba ya mwajiri wao hadi wastaafu. Sasa wataweza kupokea sehemu yao pekee ya akiba,” alisema Meneja Mkurugenzi wa kampuni ya Enwealth Financial Services, Simon Wafubwa.

Wataalamu wa masuala ya fedha wanasema hatua hii inalenga kuwezesha Serikali kupata pesa zaidi za kukopa ndani ya nchini, na hivyo kuacha kutegemea mikopo ya kigeni.

“Hatua hii itasaidia Serikali kupunguza ukopaji kutoka nchi za kigeni kwa sababu kutakuwa na pesa nyingi za kukopa katika soko la hapa nchini,” akasema Bw Wafubwa.

Uamuzi huo pia utasaidia kampuni za akiba ya malipo ya uzeeni, kwani sasa zitaweza kuendelea kuzalisha pesa hizo na kupata faida za juu kwa kipindi kirefu zaidi.

Kampuni hizo zimesifu uamuzi huo ambao wafanyikazi wanauona kama unyanyasaji.

Hatua hii inaendeleza sera za utawala wa Jubilee wa kutumia mbinu mbalimbali kufaidi mashirika makubwa makubwa na wakati huo huo kukadamiza wananchi wa tabaka la chini.

Tayari kuna kesi kortini inayopinga utozaji wa ushuru walioajiriwa kufadhili nyumba za mradi wa Serikali, licha ya kuwa wahusika wengi hawatafaidika nazo.

Pia ushuru umeendelea kupanda kila mara kwa bidhaa nyingi, hali ambayo imesababisha kupanda kwa gharama ya maisha na kuongezeka kwa umaskini ambao Jubilee iliahidi kupunguza.

Mazoea ya Jubilee kukopa sana katika soko la humu nchini yamefanya kampuni za kifedha kupendelea kuikopesha, hali ambayo kwa upande mwingine imefanya iwe vigumu kwa wenye biashara ndogo ndogo na wananchi wa kawaida kupata mikopo ya kujiendeleza.

Bw Wafubwa alieleza kuwa wafanyikazi wanaweza kutumia mbinu zingine kunufaika na akiba hiyo kama vile kutumia pesa hizo kama dhamana ya mkopo wa kununua nyumba, ama kuhamisha baadhi ya pesa hizo kwa hazina ya matibabu baada ya kustaafu.

Hatua hiyo ya Serikali imetokea wakati ambapo inakabiliwa na mzigo mkubwa wa kulipa pensheni ya watumishi wa umma.

Kufikia Juni mwaka huu, Serikali ililipa pensheni ya jumla ya Sh50.8 bilioni kwa watumishi wa umma waliostaafu, hili likiwa ni ongezeko kubwa kutoka Sh15 bilioni mnamo 2002.

Kiasi hicho ni zaidi ya Sh42 bilioni ambazo Kenya imetumia katika sekta ya afya.

Tangu Kenya ijinyakulie uhuru, watumishi wa umma waliostaafu wamekuwa wakipokea malipo ya uzeeni kwa gharama ya walipa ushuru.

You can share this post!

Muungano mkuu wa upinzani wanukia nchini Uganda

MAPISHI: Jinsi ya kupika maini ya ng’ombe

adminleo