• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Ufugaji ajira ya maana baada ya kustaafu, Sh165,000 kila mwezi

Ufugaji ajira ya maana baada ya kustaafu, Sh165,000 kila mwezi

Na MWANGI MUIRURI

WAKATI Bw Laurence Munyua alistaafu kutoka ajira ya serikali kama mwalimu katika shule za msingi mnamo 1994, hofu yake kuu ilikuwa jinsi ya kuendelea kujipa pato na asiishie kuwa masikini.

Alikuwa na uhakika kuwa kitita cha kustaafu cha Sh90, 000 alichokabidhiwa kama marupurupu ya kuaga kazi yake na pia Sh8, 500 alichokuwa apokezwe kila mwezi kama penseni yake hakikuwa na uthabiti wowote wa kumpa afueni ya maisha ya kustaafu.

“Nilijua tu ikiwa ningekosa kumakinika katika kuwekeza pesa hizo, basi nilikuwa naalika maisha ya mahangaiko na ambayo yangenituma kaburini mapema,” asema.

Katika mawazo yake ya kutumia pesa hizo kama mtaji wa kujiimarisha, alikuwa anahofia kuwa shamba lake ndogo la robo ekari halikuwa na umuhimu wowote katika maisha ya kilimo.

“Nilimwalika mtaalamu wa mipango ya mashamba na ambaye alinifahamisha kuwa shamba hilo lilikuwa kubwa zaidi. Aliniambia kuwa lilikuwa na uwezo wa kuhifadhi zaidi ya mifugo 200. Sikumwamini na ndipo nikampa kazi ya kunipangia jinsi ya kujenga manyumba ya kuhifadhi ng’ombe wa maziwa 100,” asema.

Mkazi wa kijiji cha Ndenderu katika Kaunti ya Kiambu, Bw Munyua kwa sasa anamilki ng’ombe 41 wa gredi na ambao kwa siku humpa lita 250 za maziwa.

Bw Laurence Munyua akiwa katika shamba lake Kaunti ya Kiambu ambapo kwa sasa anamiliki ng’ombe 41 wa gredi wa maziwa katika shamba lenye upana wa robo ekari. PICHA/ Mwangi Muiruri

“Kwa siku, nikiwa nimeondoa gharama zote za mradi wangu wa ufugaji, mimi huzoa Sh5, 500 kwa siku, kiasi ambacho ni Sh165, 000 kwa mwezi. Hakuna mwalimu ambaye analipwa kiasi hicho cha pesa kwa mwezi,” asema.

Anasema kuwa yeye huuza maziwa yake kwa ushirika wa wafugaji wa Kiambaa katika masaa ya asubuhi huku akiyapeleka sokoni katika mtaa wa Ndenderu jioni.

Huku uzee akisema unamsonga kwa sasa, anaamini kuwa angekosa kumakinika katika uwekezaji wake baada ya kustaafu, miaka 73 aliyo nayo kwa sasa ingekuwa imemtuma kaburini.

“Ni wengi tulistaafu pamoja lakini leo hii hawako tena. Waliokimbilia anasa za ulevi na mahaba mitaani baada ya kupkezwa pesa zao za kustaafu waliishia kuzimaliza haraka na wakapishwa katika maisha ya mauti,” asema.

Anaelezea kuwa alianza mradi huo wake wa ufugaji kwa kununua ng’ombe wawili wa gredi na ambao alizalisha kupitia teknolojia za kisasa hadi akaafikia ubora wa kiwango cha juu.

“Kuanzia 1994, nilikuwa katika harakati hizo za kuwazalisha ng’ombe hao wangu hadi mwaka wa 2006 ambapo nilikuwa nimeafikia kiwango cha juu cha ubora,” asema.

Kufuatia ueledi wake wa ufugaji na pia sifa zake kusambaa kote nchini, wafugaji wengi hujitokeza katika shamba lake ili kueleimishwa kuhusu jinsi ya kutunza ng’ombe wa maziwa.

“Kwa kila mfugaji ambaye hunikujia ili nimwelimishe, huwa namtoza ada ya Sh200 kwa siku, hali ambayo hunizidishia pato hadi Sh200, 000 kwa mwezi mmoja, ukijumuisha na lile pato la Sh165, 000 la maziwa,” asema.

Katika safari yetu katika shamba la Bw MUnyua, tulikumbana na kundi la wafugaji 500 kutoka Kaunti za Narook, Kirinyaga, Murang’a, Nyandarua na Nyeri ambao walikuwa wamemwendea ili waelimishwe jisni ya kutunza ng’ombe wa maziwa.

Bw Laurence Munyua akionyesha jinsi huhifadhi majani ya ng’ombe katika shimo la kuyakausha kama njia ya kujiwekea akiba kwa siku za kiangazi. Picha/ Mwangi Muiruri

Kando na mapato hayo, Bw Munyua huuzia wafugaji limbukeni au walio bado katika uwekezaji huo ndama wa gredi ambao bei yake huwa ni kati ya Sh50, 000 na Sh180, 000.

“Kwa mwaka, naweza kuwa nimeunda pato la Sh2 milioni kupitia mauzo hayo, hali ambayo ni ushuhuda kuwa sekta ya ufugaji wa ng’ombe ina manufaa tele na huwezi ukalia njaa au umasikini wa kustaafu. Mimi naishi maisha kama ya hawa wanasiasa ambao ni lazima waibe kutoka kwetu ili watajirike. Mimi ni bidii na jasho langu,” asema.

Bw Munyua amenunua mashine kadhaa ya kukamua ng’ombe hao wake ili kupunguza gharama za uzalishaji.

“Ukikumbatia teknolojia katika kilimo chako, utapunguza gharama za uzalishaji. Teknolojia humaanisha kuwa utaajiri vibarua wachache na kazi yako itafanyika kwa wepesi na haraka,” asema.

Katika mradi huo wake wa ng’ombe 41 wazima na ndama 28, Bw Munyua ameajiri vibarua watatu tu ambao humsaidia tu katika kufagia boma za ng’ombe hao, kuwapa chakula na hatimaye kumsaidia katika upakiaji wa mitundi ya maziwa inayoandaliwa kuwasilishwa sokoni.

Ili kukimu mahitaji ya chakula cha ng’ombe hao, Bw MUnyua amekodi shamba la ekari tatu na ambalo hupanda nyasi spesheli aina ya Kakamega I na II, na pia mahindi ambayo huvunwa kabla ya kukomaa ili kuwapa mifugo wake nyongeza ya protein muhimu za kuwafanya watoe maziwa mengi.

Anasema kuwa kinyume na hofu ya wengi kuwa kazi hii ni ngumu, yeye huamka asubuhi mwendo wa saa kumi na nusu ili kunyapara vibarua wake wakiwapa ng’ombe hao chakula na kuwakamua.

Ni katika harakati hizo ambapo masaa hayo ya asubuhi hupulizia kiingilio cha boma lake madawa ya kuua wadudu na viini hatari vya magonjwa ili kukinga shamba lake dhidi ya kuingizwa magonjwa na wageni.

Aidha, amejisajili katika mradi wa serikali wa kupewa mbegu za uzalishaji ili awe na uwezo wa kufuatilia uzalishaji katika mradi wake.

Katika uwekezaji huu wake, anasema kuwa Desemba na Januari za 2007/8 ndiyo miezi aliyokumbana na hatari kubwa ya uwekezaji wake.

“Maziwa yetu yakipokelewa katika ushirika wetu wa Kiambaa, huwa yanasafirishwa hadi Nairobi. Ni katika miezi hiyo ambapo kulizuka utata wa uchaguzi mkuu wa 2007 na ambapo magenge yalijitokeza mitaani. Kwa miezi hiyo ya ghasia, nilipoteza takriban pato la Sh300, 000,” asema.

Anasema kuwa kufikia sasa, sekta ya ufugaji inahitaji sera maalum za kukabiliana na mfumko wa bidhaa.

“Gharama za chakula kwa mifugo imepanda kwa asilimia 130 tangu mwaka wa 2012. Kwa sasa, wafugaji chipukizi wanapata shida sana wanapoingilia sekta hii ya ufugaji ng’ombe wa maziwa. Sisi tunabahatika kwa kuwa tumekuwa tukijiwekea akiba kwa miaka mingi ambayo tumekuwa katika ufugaji,” asema.

You can share this post!

‘Afufuka’ kabla ya kuzikwa

Wazee wataka mkewe Ken Okoth ‘arithiwe’...

adminleo