• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 12:30 PM
Mhadhiri mpenda lugha mama na aliye na historia pevu

Mhadhiri mpenda lugha mama na aliye na historia pevu

Na MWANGI MUIRURI

ALITOKA hapa nchini baada ya kujiondoa kutoka kikosi cha polisi – ambapo kwa wakati mmoja alikuwa mlinzi wa Hayati Mzee Jomo Kenyatta – na akaelekea ng’ambo.

Leo hii, Bw Gatua wa Mbugwa ni mhadhiri wa kilimo cha kisayansi nchini Amerika.

Aidha, ameweka historia ya kuwa mwanafunzi wa kipekee ulimwenguni wa kuandika utafiti wa mtihani wake wa PhD kwa lugha mama.

SWALI: Tuelezee historia yako fupi

JIBU: Mimi nilizaliwa mwaka wa 1956 katika kijiji cha Mutunguru Wilayani Thika. Mimi ndiye kifungua mimba wa Mzee Mbugwa Mwatha na mama Lucy Wanjiku ambao kwa jumla walijaliwa watoto 11 wanane wetu tukiwa vijana. Nilijiunga na kikosi cha Polisi mwaka wa 1977 kama Konstebo na nikatekeleza wajibu wangu kama mlinzi wa Mzee Jomo Kenyatta akiwa ikulu ya Nakuru. Lakini nilisononeka kazini na ndipo nikajitoa mwaka wa 1980.

SWALI: Ni matukio gani katika kazi yako ya polisi unayoyakumbuka sana?

JIBU: Mwaka wa 1978 nilikuwa katika kikosi cha polisi ambacho kilienda kupambana na wezi wa ng’ombe katika kijiji cha Manzille Wilayani Moyale. Ufyatulianaji risasi ulitanda na zaidi ya watu 10 wakaaga dunia kutoka pande zote mbili.

SWALI: Na ikawaje ukaamua kujiondoa kazini kama afisa wa polisi?

JIBU: Nilinyimwa kupandishwa ngazi licha ya kuhitimu kimasomo. Niliamua hakuna vile ningevumilia dhuluma na nikajitoa. Ni vyema ieleweke kazi hiyo haikuwa mwito wangu na sikuwa na raha kazini. Nilikuwa nimejiamini sana na hakuna jinsi ambavyo ningeendelea kunyanyaswa na wakubwa ambao wengi wao hata hawakuwa wameuona mlango wa Shule ya Sekondari.

SWALI: Kwa sasa unafanya nini maishani?

JIBU: Mimi ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Wyoming, Amerika. Mimi hufundisha masuala ya Kilimo cha Kisayansi na pia masuala ya tamaduni za Kiafrika.

SWALI: Ni ukweli kuwa uliandika nakala ya utafiti ya kutuzwa shahada kwa lugha ya mama?

JIBU: Ndio! Niliandika kwa lugha ya Gikuyu na kwa sasa mimi ndiye tu mwanafunzi wa kwanza wa Kiafrika kutimiza wajibu huo kwa lugha mama. Utafiti huo unajulikana kama Nditi ya ?r?mi wa Mbayotethib? Kenya K?r? Magetha ma Th?k?ma na Maguni Th?ini? wa Cio. Ulikuwa ni utafiti wa kilimo cha sukumawiki kisayansi na manufaa yake. Nilifanya utafiti na nikagundua kuwa kuna jinsi ambavyo unaweza kuzalisha mmea huo Kisayansi na uimarishe kilimo chake bila kutumia fatalaiza. Niliwasilisha utafiti huo kwa Mkuu wa Kitengo cha Utafiti katika Chuo Kikuu cha Wyoming mwaka wa 2008 na ndipo nikatuzwa shahada yangu ya uzamifu.

SWALI: Ilikuwa namna gani hadi ukajipata umejiunga na uhadhiri?

JIBU: Ni safari ndefu ambayo ilianzia na mahangaiko na kisha nikafanikiwa. Nilipojiuzuru kazi kama afisa wa polisi, nilihangaika si haba. Nilianza shughuli za kilimo mashambani lakini ikawa hakuna manufaa. Nikatafuta kazi katika kasino moja ya Mombasa na mshahara ukawa duni. Nikaweka biashara ya duka la jumla lakini sikufanikiwa. Mwaka wa 1990 nilijiunga na taasisi ya Manor House Agricultural Centre iliyoko Kitale. Kwa miaka miwili nilisomea taaluma ya Kilimo cha Kisayansi. Mwaka wa 1992 nilihamia nchini Amerika ambapo kwa miezi sita niliimarisha masomo yangu ya kilimo katika Chuo Kikuu cha Santa Cruz katika jimbo la California. Taasisi ya Manor House ndiyo ilinifadhili katika masomo hayo. Baadaye niliendelea na masomo katika taasisi ya Cabrillo Community College. Nilirejea katika Chuo cha Santa Cruz ambapo mwaka wa 1997 nilipata shahada ya digrii kuhusu Kilimo, Siasa na pia masomo ya Mazingira. Mwaka wa 1998 nilijiunga na Chuo Kikuu cha Cornell nchini Amerika na nikapata shahada yangu ya digrii ya juu kuhusu kilimo cha Kisayansi na utafiti kuhusu udongo mwaka wa 2003. Hapo ndipo nilipata kazi ya uhathiri katika Chuo Kikuu cha Wyomin ambapo hata kwa sasa natekelezea wajibu huo.

SWALI: Ni msukumo gani uliokuelekeza kuandika utafiti wako kwa lugha ya mama?

JIBU: Ni vyema ieleweke kuwa Waafrika wengi hawajivunii utamaduni wao wa lugha. Ninapenda lugha yangu sana. Nilikuja kuelewa kuwa fani ya uandishi inaweza kutumika kuangazia lugha zetu za Kiafrika lakini wengi wa wasomi wanahusisha lugha za kiasili na udhaifu wa kimawazo katika enzi za ukoloni mamboleo. Waafrika ndio wanamilki asilimia 60 ya lugha zote za ulimwengu ambazo ni takriban 6,000. Niliamua kuweka lugha yangu ya Gikuyu katika vitabu vya historia nikafanikiwa.

SWALI: Ni changamoto gani ulikumbana nazo katika utayarishaji wa utafiti huo kwa lugha ya mama?

JIBU: Nakubali kuwa hilo ndilo suala gumu zaidi ambalo nishawahi kutekeleza kimasomo. Niliteseka nikitafuta majina ya kuelezea majina ya Kisayansi bila kupoteza utafsiri wake. Aidha, nilihitajika kujikosoa mimi mwenyewe kwani hakukuwa na mwingine ambaye alikuwa akishiriki uandishi wa utafiti wake kwa lugha hiyo. Kompyuta nayo haikuwa na majina ya Gikuyu na ikawa lazima ningetafuta majina hayo kivyangu. Ilikuwa ni kazi ngumu lakini ambayo hatimae ilinipa ugwiji wa kipekee katika fani ya wasomi. Aidha, nilikuja kuelewa kuwa lugha yangu ya mama ina utajiri wa maneno ambayo yamepotelea katika athari za lugha zingine ambazo zinatiliwa mkazo kama Kiingereza na Kiswahili.

SWALI: Kuna mtu yeyote ambaye alikupea motisha katika uandishi huo wa kipekee?

JIBU: Ndio! Nilipata motisha kutoka kwa msomi na pia mwandishi wa kuheshimika ambaye ni Profesa Ngugi wa Thiong’o. Kama mfuasi wa kazi zake, nilimdokezea kuwa nilikuwa na ari ya kukuza lugha yangu ya mama na akaniunga mkono. Hata alinipa wajibu wa kuandikia jarida lake la Gikuyu ambalo alianzisha nchini Amerika kwa jina Mutiiri. Aidha, alinihimiza niwe nikitunga mashairi kwa lugha ya Gikuyu na ndipo mwaka wa 1999 nikatoa kanda ya mashairi kwa jina Maitu ni Ma Iitu (Mama ni Ukweli wetu). Ilizinduliwa na Bw Thiong’o mwaka wa 2000 katika hafla ya kusherehekea kongamano la ‘Against All Odds: African Languages and Literatures into the 21st Century’ lililosherehekewa katika Mji wa Asmara, Eritrea. Mwaka wa 2005 nilizindua kanda nyingine za mashairi ya Gikuyu. Ushawishi huo ndio ulinisukuma hadi kuandika utafiti wangu kwa lugha ya mama. Naye Bw Thiong’o akanihimiza nishikilie ari hiyo mpaka nifanikiwe.

SWALI: Una na nia ya kurudi hapa nchini usaidie katika ujenzi wa Taifa ukitumia masomo ya Kilimo ambayo umeyapata huko ng’ambo?

JIBU: Kwa sasa nina shughuli nyingi katika wadhifa wangu wa uhadhiri. Pia, nahisi kuwa maendeleo na ufanisi katika teknolojia kuhusu mbinu mpya za kilimo zinafaa kusomewa zaidi na bado nakimbizana na masomo hayo. Ni wakati nitajihisi nimepata maarifa na ujuzi kamili ambapo nitafikiria mambo ya kurejea nyumbani. Lakini tuna wataalamu wa kutosha hapa nchini na ambao wanaweza kufanikisha utaalamu wa kilimo. Tukijiamini tunaweza kuondoa mahangaiko ya njaa na tuinue hali ya mapato ya wakulima wetu; hasa jamii ambazo ni za wafugaji na ambazo huishi katika maeneo tambarare ndio wanafaa kuinuliwa ili wawekeze katika kilimo cha kisasa. Ni aibu kuwaona wakiombewa misaada ya chakula na kukumbwa na mauti kila mwaka kutokana na kutegemea kwao kwa mifugo ambayo haina faida.

SWALI: Ebu tuelezee kuhusu furaha yako na pia sikitiko lako katika maisha?

JIBU: Furaha yangu ni kuwa na familia ambayo ninaipenda na imebarikiwa. Mke wangu ambaye ni Mary Wairimu na watoto wangu watatu ambao ni wa kati ya umri wa miaka 12 na mwaka mmoja ni baraka kubwa sana kwangu. Sikitiko langu kuu ni wakati nilipoteza mamangu Machi 2007 kabla ya kushuhudia kufanikiwa kwangu maishani. Nilitamani sana awe karibu nami wakati nilikuwa nikituzwa shahada yangu ya uzamifu kwa kutukuza lugha ya mama. Hata hivyo, ninajua baraka zake bado zinaniandama maishani hata akiwa ameshatangulia mbele ya haki.

You can share this post!

Wizara yawataka watalii waepuke mitego ya matapeli...

Wito wakulima wachukulie viwavi hatari hatua nyingine

adminleo