• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 8:50 AM
WANGARI: Serikali imepuuza maslahi ya vijana wa Kenya

WANGARI: Serikali imepuuza maslahi ya vijana wa Kenya

Na MARY WANGARI

MAJUZI kumekuwa na misururu ya visa na masimulizi ya kutamausha kuhusu vijana waliosoma na kupata shahada za digrii na hata uzamili, wanaoishi maisha ya uchochole kwa kukosa ajira.

Ripoti hizo zimewaacha Wakenya wakijiuliza nini hasa umuhimu wa elimu katika kizazi cha leo.

Idadi kubwa ya vijana walioathiriwa ni werevu katika masomo na walipata alama za juu zilizowawezesha kufanya kozi tajika. Ole wao! Hawakuwa tayari kwa kilichowasubiri katika ulimwengu usio na huruma uliochekelea ushauri waliopatiwa kwamba ‘elimu ndio ufunguo wa maisha!

Kisa cha Kevin Ochieng aliyekuwa akiishi barabarani bila makao baada ya kukosa kazi licha ya kufuzu kwa daraja ya kwanza katika Sayansi ya Hisabati na Takwimu, ni mfano mzuri.

Kinaya ni kwamba iligharimu masaibu yake kuangaziwa na vyombo vya habari, ndipo mashirika chungu nzima mashuhuri ya kiserikali na kibinafsi, yalipojitokeza kumpa kazi, ikiwemo kampuni zilizokuwa zimemkataa hapo mbeleni, na kuwaacha wengi wakishangaa zilikotoka ghafla nafasi hizo za kazi.

Hii ni ishara thabiti kwamba tatizo si vijana bali ni sera mbovu na unafiki katika jamii kwa jumla iliyowasaliti vijana wetu.

Ni kinaya na unafiki wa kiwango cha juu kuwasikia baadhi ya watu waliojitwika ghafla cheo cha ujuzi kuhusu masuala ya kiuchumi, wakiwashauri vijana kufikiria mbinu nyinginezo za kujipatia riziki badala ya kutegemea ajira etu kwa sababu hakuna nafasi za kazi nchini.

Inakera mno kuwasikia baadhi ya watu wakiwasuta vijana kwa kuzembea na kukosa ubunifu wa kuvumbua mbinu nyinginezo badala ya kusaka ajira ilhali wanaowakashifu vijana hao wameajiriwa.

Wa kulaumiwa ni nani wakati mfumo wa elimu waliopitia vijana hao uliwaandaa kwa ajira? Ni vigumu mno kubadili ghafla mawazo ya kijana aliyeandaliwa kwa zaidi ya miaka 15 tangu shule ya chekechea hadi chuo kikuu ‘kusoma kwa bidii’ ndipo ‘apate kazi nzuri.’

Ikiwa ni biashara, ni wazi kwamba unahitaji mtaji kuanza pamoja na mazingira mwafaka ili biashara inawiri. Baadhi ya vijana waliobahatika kupata mtaji na kuanza biashara kwa lengo la kuunda ajira, wamesimulia masaibu waliyopitia kutokana na sera mbovu zilizowalazimu kufunga biashara zao na kurejea walipoanzia.

Ukweli mchungu ni kwamba, serikali na jamii kwa jumla imewasaliti vijana na ndiposa tunashuhudia idadi kubwa ya vijana gerezani kwa kutenda uhalifu baada ya kukata tamaa maishani. Ni sharti tubuni sera mwafaka zitakazowezesha kuwepo kwa mazingira bora kwa vijana kupata nafasi za kujipatia riziki na kujiendeleza kimaisha, la sivyo, mustakabali wetu kama taifa unaning’inia hatarini.

[email protected]

You can share this post!

MBURU: Raia wahamasishwe kuhusu athari za uchafuzi wa mito

ONYANGO: Baringo sasa ni kitovu cha malaria, serikali iwe...

adminleo