• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
CHOCHEO: Kukataliwa ni kawaida, jinyanyue na maisha yasonge

CHOCHEO: Kukataliwa ni kawaida, jinyanyue na maisha yasonge

Na BENSON MATHEKA

DAVY, barobaro mwenye umri wa miaka 25 alipoanza kumrushia chambo Agie, 23, alikuwa na matumaini makubwa kuwa atakubali kuwa mpenzi wake.

Walikuwa wamejuana kwa miaka mingi, walikuwa wamefanya mengi pamoja na alikuwa ameridhika kuwa mwanadada huyo alikuwa mwenye nidhamu ya hali ya juu na mwaminifu.

Hata hivyo, jibu alilolipata kutoka wa Agie lilimvunja moyo akahisi kuwa hakufaa kuendelea kuishi ulimwenguni.

“Aliniambia hawezi kukubali kuwa mpenzi wangu. Kwamba alikuwa na mwanamume bora kuniliko. Kilichoniudhi ni jinsi alivyonijibu kwa dharau. Nilijiona kama mtu asiye na maana katika ulimwengu huu, asiyeweza kupendwa,” alisema Davy.

Kama haingekuwa rafiki yake aliyemshauri atafute ushauri nasaha, Davy angechukua hatua ambazo zingemfanya ajute.

“Kukataliwa na mchumba au mtu uliyeweka matumaini atakupenda sio rahisi, kuna uchungu na kunaweza kufanya mtu kujitumbukiza katika matatizo makuu,” asema mwanasaikolojia Beth Wandei wa shirika la Big Hearts jinini Nairobi.

Anasema watu wanafaa kufahamu kuwa kila mtu anaweza kukataliwa maishani hata na watu waliowekeza rasilmali, nguvu na wakati ili kuwasaidia wakidhani wanawapenda.

Wataalamu wanasema ni kawaida mtu kukasirika, kutamauka na kusononeka akikataliwa au kutemwa na mpenzi au mtu aliyekuwa akimezea mate.

“Ni tukio linaloweza kusababishia mtu matatizo ya kiafya kama kuumwa na kichwa, maumivu ya tumbo, mfadhaiko na shinikizo la damu na kumfanya apate matibabu,” asema Bi Wandei.

Hata hivyo, anasema ingawa ni kawaida mtu kujipata katika hali hii haifai kumlemaza kimaisha.

“Hakuna anayeweza kusema kuwa ana nguvu kiasi cha kutohisi athari za kukataliwa na mtu aliyewekea matumaini kuwa mchumba wake maishani. Unaweza kulia, kukasirika na hata kufadhaika ukajipata katika hospitali. Kilicho kibaya na hatari ni kuchukua sheria mikononi mwako kwa sababu unaweza kujuta zaidi,” aeleza.

Wataalamu wanasema hali inaweza kuwa mbaya kwa mtu anayekataliwa mara ya kwanza.

“Kwa watu kama hao ni kawaida kulia. Tunawashauri wakihisi kulia wasijizuie, wajifungie mahali salama walie ili wapunguze machungu moyoni,” aeleza.

Kulingana na Dkt Seth Aboo wa shirika la Light Care mjini Athi River, Machakos, baada ya mtu kupunguza hasira kwa kulia hafai kunyamaza.

“Zungumza na mtu unayemwamini umweleze kuhusu masaibu yako. Anaweza kuwa rafiki, kiongozi wa kidini au mtu aliyepitia hali sawa. Sikiliza wanayokueleza na unaweza kugundua kuwa wewe sio wa kwanza kukataliwa duniani. Watu wametendwa, wakazama, wakaibuka na kunawiri zaidi katika mapenzi,” aeleza Aboo.

Kufanya uchambuzi

Mtaalamu huyu ansema baada ya mtu kutulia anafaa kuchambua yaliyotendeka na manufaa yake kwa kukataliwa au kutemwa.

“Kukasirika kwa sababu umekataliwa ni sawa na kunywa sumu na kutarajia mtu mwingine afe. Unavyoendelea kusononeka, aliyekutema anaendelea na maisha yake kama kawaida,” asema Aboo.

Bi Wandei anasema watu wengi huwa wanakosea kwa kutaka kulipiza kisasi kwa kuzua ghasia.

“Mtu akikukataa, ana haki ya kufanya hivyo. Kamwe usiwahi kulipiza kisasi kwake na usipeleke hasira zako kwa watu wengine kwa kuwa mkali au kuzua vurugu. Ukifanya hivi, watu watakuepuka na ukataliwe zaidi,” asema.

Wataalamu wanashauri watu kuepuka hulka mbaya kama vile kulewa kupindukia, kuvuta sigara, kutumia dawa za kulevya au kujiingiza katika vitendo vya ufuska baada ya kukataliwa au kupigwa teke na wachumba wao.

“Hulka kama hizi ni hatari, zitakuongezea shida na kukuacha katika hali mbaya zaidi,” aeleza Aboo.

Kulingana na Davy, baada ya kupata ushauri nasaha, alisahau masuala ya mapenzi kwa muda, akajiunga na kilabu ya muziki kanisani kisha akajiunga na chuo kimoja jijini kwa masomo ya muda.

“Baada ya mwaka mmoja, hali yangu ilibadilika na kuwa bora zaidi. Niliwapata marafiki wapya na nikajifunza kuwa mwangalifu katika masuala ya mapenzi. Siko tayari kujipata katika hali aliyonisababishia Agie kwa kunikataa,” aeleza.

You can share this post!

Netanyahu kushtakiwa rasmi kwa ufisadi, asema hatingisiki

Yafichuka jinsi watumishi wa umma wanavyofyonza nchi

adminleo