• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 12:45 AM
Kalameni aoa wake wengi ili asifiwe

Kalameni aoa wake wengi ili asifiwe

Na TOBBIE WEKESA

KETEBAT, TESO

Kalameni alishangaza ndugu zake alipowaambia kuwa anataka kuoa wanawake wengi kama babu yake.

Kulingana na mdokezi, jamaa aliaandaa mkutano wa familia na kuweka wazi mipango yake.

Alitoa tangazo hilo na kuwajuza kwamba sababu yake kuu ni kutaka kufata nyayo za babu yake aliyekuwa jogoo kijijini.

“Ninataka kusema hivi. Babu yetu aliheshimiwa sana kwa sababu alikuwa na wake wengi. Hiyo heshima lazima tuidumishe,” alianza kwa kusema.

Ndugu zake walibaki vinywa wazi. “Lazima nimfurahishe babu kwa kufuata nyayo zake. Yeyote atakeyeniletea pingamizi tutakabiliana ipasavyo,” kalameni aliendelea.

Duru zinasema kabla ya kuitisha kikao hicho tayari kulikuwa na lalama kutoka kwa wake zake wa sasa, kwamba amewatelekeza.

“Kwa sasa uko na wanawake watatu, wote wanalalamika. Eti bado unataka kujiongezea wengine ili kufuata nyayo za babu. Utafaulu kweli?” jamaa aliulizwa na kaka yake mmoja.

Alipuuzilia mbali madai hayo. “Kila mwanamke ana shamba lake. Wako na nguvu za kulima ili wajitafutia chakula na mazao mengine ya kuuza sokoni wapate mapeni kidogo.

“Shida yao ni kulalamika tu. Kama babu alifaulu mbona nisifaulu,” kalameni alijibu kwa ukali.

Isitoshe, jamaa aliwakanya dada zake dhidi ya kuungana na wake zake hao watatu kuhujumu mipango yake.

“Ninajua wengine hapa wamesikia juma lijalo ninaleta mke wa nne. Tayari wameshaanza kueneza fitina kwa wake zangu. Komeni kabisa,” jamaa aliwaonya.

Akina dada hawakufurahishwa na vitisho hivyo.

“Ukijitakia sifa kama za babu kutokana na kuwa na wake wengi, sisi hatuna shida. Lakini huu upuzi na ujinga wa kutuzomea peleka kwingine,” walimkemea ndugu yao.

Muda si muda mkutano ukiendelea, wake wa jamaa walifika ghafla kikaoni na kumkabili.

“Anajifananisha na wazee wa zamani bila kujua nyakati zimebadilika. Anajifanya tu lakini hawezi lolote,” wanawake wakamuanika kalameni, lakini alishikilia msimamo wake.

You can share this post!

Serikali kujenga daraja kuu kukabili ongezeko la maafa

JAMVI: Odinga na Ruto wanavyoyumbisha umoja wa Mulembe

adminleo