• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
GOLD COAST AUSTRALIA: Wanaotegemewa na Kenya mita 800 kwa wanawake

GOLD COAST AUSTRALIA: Wanaotegemewa na Kenya mita 800 kwa wanawake

Na CHRIS ADUNGO

WANARIADHA Margaret Nyairera Wambui, Eglay Nalyanya na Emily Cherotich Tuwei wanatazamiwa Alhamisi kufuzu kwa fainali za mbio za mita 800 kwa upande wa wanawake na kuiweka Kenya katika nafasi nzuri ya kujizolea nishani tatu kwa mpigo zitakazoipaisha kwenye msimamo wa jedwali la Michezo ya Jumuiya ya Madola nchini Australia. 

Nalyanya atakuwa wa kwanza kushuka uwanjani kuwania tiketi ya fainali kwa matarajio ya kumpiku bingwa wa Afrika Kusini, Caster Semenya aliyejizolea dhahabu katika mbio za mita 1,500 kwa upande wa wanawake mnamo Jumanne baada ya kumzidi maarifa Mkenya Beatrice Chepkoech.

Semenya aliyeweka rekodi mpya kitaifa na kwenye Michezo ya Jumuiya ya Madola kwa kukata utepe baada ya dakika 4:00.71 katika mbio za Jumanne anapigiwa upatu kuitawala pia fani ya mita 800.

Ingawa hivyo, huenda akatolewa kijasho na Docus Ajok wa Uganda, Natalia Evangelidou (Cyprus), Keely Small (Australia), Angela Petty (New Zealand) na Mwingireza Alexandra Bell.

Wapinzani wengine watakaopeperusha bendera za mataifa yao katika Kundi la kwanza la mchujo ni Gayanthika Artigala Aberathna wa Sri-Lanka na Mariama Conteh wa Slovenia.

Kundi la pili linalomjumuisha Nyairera ndilo linalotazamiwa kutawaliwa na ushindani mkali zaidi kutoka kwa Natoya Goule wa Jamaica, Shelayna Oskan-Clarke (Uingereza) na Mganda Halima Nakaayi.

Wengine watakaonogesha kampeni za kufuzu kutoka Kundi hilo ni Tsepang Sello (Lesotho), Brittany Mcgowan (Australia), Agnes Abu (Ghana) na Ciara Mageean wa Ireland Kaskazini.

Tuwei anapigiwa upatu wa kutawala Kundi la tatu la mchujo ambalo litawashirikisha Lynsey Sharp wa Scotland, Georgia Griffith (Australia), Alice Ishimwe (Rwanda), Nimali  Arachchige (Sri-Lanka), Winnie Nanyondo (Uganda) na Mwingereza Adelle Tracey

You can share this post!

GOLD COAST AUSTRALIA: Kibarua kizito kumbwaga Nijel Amos...

GOLD COAST AUSTRALIA: Unyonge wa Wakenya mbio za masafa...

adminleo