• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 8:55 AM
ONGARO: Yapo mengi atakayokumbukwa nayo Moi

ONGARO: Yapo mengi atakayokumbukwa nayo Moi

Na LAWRENCE ONGARO

RAIS mstaafu Daniel Arap Moi aliyefariki Jumanne katika Nairobi Hospital ana historia ndefu ambapo atakumbukwa kwa kuiongoza Kenya, lakini pia kama mtu mnyenyekevu na mtulivu.

Alizaliwa mwaka wa Septemba 2, 1924, katika kijiji cha Kurieing’wo, Sacho, Wilaya ya Baringo kulingana na maelezo kwenye maandiko.

Akiwa na umri wa miaka minne pekee babake Kimoi arap Chebii alifariki.

Ingawa hivyo, mwaka wa kuzaliwa Moi unapingwa na watu wa karibu naye waliomjua vizuri.

Alibaki chini ya uangalizi wa nduguye mkubwa Bw William Tuitoek ambaye alimfaa pakubwa na kumwelekeza katika shughuli ya kulisha mifugo.

Baada ya kukamilisha masomo yake alijiunga na Chuo cha walimu cha Tambach Teachers’ Training College katika wilaya ya Keiyo kabla ya kuanza kazi ya ualimu.

Mara yake ya kwanza kujitosa katika ulingo wa siasa ilikuwa mwaka wa 1955 alipokuwa mwanachama mmojawapo wa LEGCO.

Mzee Moi alikuwa mmoja wa waanzilishi wa chama cha KADU kwa ushirikiano na Bw Ronald Ngala wa Pwani ambaye ndiye alikuwa kinara wa chama huku akiwa mwenyekiti wake.

Hata hivyo kwa upande wa siasa Moi alitajwa kama mkakamavu alipokuwa Makamu wa Rais huku akivumilia mawimbi makali yaliyomkabili kupitia wandani wa Rais wa kwanza wa Kenya Hayati Mzee Jomo Kenyatta.

Kila mara alipokosolewa na kupokea matusi kutoka kwa viongozi hao, Mzee Kenyatta alikuwa mstari wa mbele kumtetea na hiyo ilimfanya yeye kuhifadhi kiti hicho cha makamu wa rais kwa muda wa miaka 12.

Wakati mgumu zaidi aliopitia ni mwaka wa 1976 mjadala wa kubadilisha katiba ulipochacha huku wandani wa rais Kenyatta wakati huo wakitaka kumzuia asiwahi kuchukua nafasi ya urais iwapo nafasi hiyo ingebaki wazi.

Wale waliotaka mabadiliko hayo ni aliyekuwa Waziri wa Masuala ya Kigeni Dkt Njoroge Mungai,  aliyekuwa Waziri wa Fedha James Gichuru, aliyekuwa Waziri wa Ardhi Jackson Angaine, na aliyekuwa Waziri wa Ushirika na Maendeleo Paul Ngei.

Wakati huo pia kulikuwa na mrengo uliopinga kubadilishwa kwa Katiba nao ni wa aliyekuwa mbunge wa Mvita Shariff Nassir, na aliyekuwa mbunge wa Kajiado Kaskazini Stanley Oloi Tiptip pamoja na viongozi wengine 98.

Kulingana na mjadala wa kubadilisha Katiba, aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wakati huo Bw Charles Njonjo aliingilia kati na kuzima juhudi hizo wa viongozi hao walioshinikiza mpango huo.

Viongozi hao wote waliitwa na Rais Kenyatta mwaka wa 1976 kwa mkutano wa dharura katika Ikulu ya Nakuru, ambapo Rais aliwasuta na kuzima mjadala huo mbele ya Bw Njonjo ambaye aliidhinisha matamshi ya Kenyatta.

Kati ya mwaka wa 1977 na 78 mkuu wa polisi katika Bonde la Ufa Bw James Mungai alibuni kikosi maalum cha Ngoroko ambacho wakati fulani kiliweza pia kumhangaisha Rais Moi alipokuwa akielekea kwake Kabarak.

Hata hivyo kikosi hicho cha watu 250 kilivunjiliwa mbali mara tu Rais Moi alipochukua usukani huku afisa huyo wa polisi Bw Mungai akikimbilia ulaya nchini Uswisi akihofia kutiwa nguvuni.

Alilazimika kuchukua gari la serikali lililomfikisha Sudan, ambako aliabiri ndege na kutokomea Ulaya.

Baada ya kifo cha hayati Mzee Kenyatta mwaka wa Agosti 22, 1978, mwendo wa saa 9 za alfajiri mjini Mombasa, mkuu wa mkoa wa eneo hilo wakati huo Bw Eliud Mahihu, aliwasiliana na mzee Moi na kumwarifu ya kwamba ‘Taa ya Kenya imezimika’. Kwa hivyo alitakikana asafiri haraka Nairobi ili aapishwe kama rais wa pili.

Wandani wa mzee Kenyatta walishtushwa na habari hiyo huku rafikiye wa dhati Mbiyu Koinange,akipatwa na mshtuko mkubwa.

Baada ya kuapishwa kama rais alilazimika kukamilisha siku 90 kabla ya kushikilia usukani kamili.

Hata hivyo mapinduzi ya Agosti Mosi 1982, yalibadilisha mkondo wa uongozi wa Moi ambaye alikuwa mpole aligeuka kuwa mtu wa kipekee kwani hakumuamini yeyote yule na alikuwa na makachero kila sehemu hadi vijijini.

Mawaziri wengi walipata habari za kuteuluiwa nyadhifa zao kupitia taarifa ya habari ya KBC jambo lililofanya kila kiongozi kutekeleza wajibu wake kwa makini.

Ilipofika Machi 19, 2002, chama cha Kanu na NDP cha Raila Odinga viliungana na kufanya kazi pamoja.

Moi alichaguliwa kuwa Mwenyekiti, Raila Odinga akawa katibu mkuu naye Yusuf Haji alichaguliwa kama mwekahazina.

Wengine ni Uhuru Kenyatta, Musalia Mudavadi, Kalonzo Musyoka, na Katana Ngala ambao walikuwa manaibu wa mwenyekiti katika muungano huo.

Makamu wa Rais wakati huo marehemu Prof George Saitoti na Joseph Kamotho, wandani sugu wa Rais Moi walichujwa nje ya uchaguzi huo bila matarajio yao.

Siasa za kugeuza kipegee cha Katiba cha 2A ili kuwe na vyama vingi mwaka wa 1991 zilianza kugeuza siasa za nchi huku shinikizo zikitoka nchi za nje na mashirika za kutetea haki za wananchi zikija juu ili kuwe na mageuzi za uongozi.

Hata hivyo Mzee Moi alistaafu kwa heshima mwaka wa 2002 ambapo alimkabidhi mamlaka Bw Mwai Kibaki kama Rais wa tatu wa nchi ya Kenya naye akafululiza hadi kwake Kabarak ambako alikuwa akitembelewa na viongozi tofauti ili kupata ushauri kutoka kwake.

Baada ya kukabiliana na uzee na maradhi ya kimwili kwa miezi michache iliyopita aliaga dunia Februari 4, 2020, saa 5:20 alfajiri katika Nairobi Hospital.

You can share this post!

Uteuzi wa kikosi cha riadha ya AK ni wikendi hii

SANAA: Bendi ya Ricky na Marafiki ina wanachama wenye...

adminleo