• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 3:25 PM
AKILIMALI: Ifahamu mikate ya ng’ombe kutoka Kalro

AKILIMALI: Ifahamu mikate ya ng’ombe kutoka Kalro

NA RICHARD MAOSI

KILOMITA 16 hivi kutoka mjini Nakuru tunawasili katika makazi ya Miriam Wangare, mkazi wa Wanyororo B, eneo la Lanet ambaye ni mkulima mdogo wa ng’ombe wa maziwa.

Huu ni mwaka wa pili tangu aanze kulisha mifugo wake na aina maalum ya nyasi zinazotengeneza lishe ya kisasa, mikate ya ng’ombe, zilizovumbuliwa na Shirika la Utafiri wa Kilimo na Ufugaji (Kalro).

Anasema awali alikuwa akitumia nyasi za kawaida kama vile napier, kulisha ng’ombe wake lakini akahudhuria kongamano la wakulima 2017 kujifundisha nyenzo mbalimbali za kuboresha mazao ya mifugo wake kupitia lishe.

Alieleza Akilimali kuwa lishe hizi hutengenezwa, baada ya kukausha aina ya nyasi zinazojulikana kama Brachiaria (nyasi za kigeni), kisha zikachanganywa na virutubishi vya protini, kuokwa na kukaushwa.

“Mifugo hufurahia aina hii ya lishe kwa sababu ina ladha nzuri kuliko aina nyingine ya nyasi ambazo hazina madini ya kutosha,” anasema.

Pili alieleza kuwa nyasi ya brachiaria hustahimili hali ngumu ya mazingira kama vile ukame uliokidhiri na ukosefu wa rutuba katika mchanga, hivyo basi gharama ya kukuza nyasi hizi mara nyingi huwa ni nafuu. Picha/ Richard Maosi

Pili alieleza kuwa nyasi ya brachiaria hustahimili hali ngumu ya mazingira kama vile ukame uliokidhiri na ukosefu wa rutuba katika mchanga, hivyo basi gharama ya kukuza nyasi hizi mara nyingi huwa ni nafuu.

Brachiaria huchukua miezi mitatu tu kukomaa ambapo mkulima huwa tayari kuzivuna kisha akazihifadhi katika ghala ama kulisha mifugo wake moja kwa moja zikiwa mbichi.

Kwa upande Wangare anasema mkulima anaweza kuongezea lishe hizi thamani kwa kuchanganya molasses, chumvi ya kawaida na kuoka mchanganyiko huu kisha akatengeneza miundo ya mikate .

Miundo hii inaweza kuhifadhiwa katika sehemu yenye joto jingi kama vile ndani ya kitalu ama kwenye jua ili iweze kushikamana vyema na kupoteza unyevu.

Wangare alisema kuwa mara ya mwisho alivuna mazao yake mwezi wa Novemba, mwaka wa 2019 na sasa anasubiri mazao ya pili kufikia mwezi wa Februari mwaka wa 2020.

Miriam Wangare akiwa katika shamba lake la Wanyororo Lanet Nakuru akiwalisha mifugo wake mikate ya kisasa. Picha/ Richard Maosi

Kwa ujumla anaungama kuwa tangu aanze kulisha mifugo wake na Feedblocks, amaeongeza faida kwa mazao yake ya maziwa ambapo yaliongezeka zaidi ya mara dufu chini ya kipindi cha wiki moja.

Awali alikuwa akipata lita 4 za maziwa kutoka kwa ng’ombe mmoja, lakini sasa anaweza kupata baina ya lita 8-10 kwa siku kwa kutegemea yeye huwalisha mifugo wake mara ngapi kwa wiki.

Tatu anasema kuwa ni rahisi kukuza aina hii ya nyasi za barachiaria kwani hahitaji uangalizi mkubwa iwapo shambani, kama vile kuondoa magugu wala kupalilia muradi mkulima awe ametumia mbegu zinazostahili.

Hatua za kutengeneza mikate ya ng’ombe

Hatua chache kutoka kwake Akilimali ilitembelea shirika la Kenya Agricultural and Livestock Research Organisation kupambanua namna ya kutengeneza mikate(feedblocks) inayoweza kudumu kwa muda mrefu.

Gharama ya kukuza lishe hii iko chini. Picha/ Richard Maosi

Tulikutana na Daktari Naftali Ondabu mtafiti wa lishe za mifugo ambaye alitupatia utaratibu wa kuandaa aina hii ya mikate, ambayo ndiyo uvumbuzi wa kwanza kabisa kufanyika humu nchini.

Anasema kuwa katika hatua ya kwanza pindi mkulima anapovuna nyasi zake(brachiaria, lucern ama Desmodium), anaweza kuzihifadhi katika jua ili ziweze kukauka kabla ya kuzioka.

Aliongezea kuwa sio nyasi za aina yoyote zinazoweza kutumika, kwa sababu ya kiwango tofauti cha madini yanayopatikana ndani ya malisho ya ngombe yanayokuzwa.

“Kwa mfano nyasi za brachiaria zinaongoza kwa kiwango cha juu cha protini ambacho kinaweza kufikia zaidi ya asilimia 70,”akasema.

Alieleza kuwa mara tu baada ya nyasi za brachiaria kukauka zinaweza kuchanganywa na molasses, kisha zikahifadhiwa katika sehemu isiyokuwa na unyevu zipate kukauka.

Anasema kwa kutumia maji ya moto ndani ya beseni ya kimo cha kawaida, mkulima anaweza kuchanganya nyasi zake zilizokauka na kuongezea chumvi ya kjawaida ili kuzipatia ladha.

Kutoka kwenye mchanganyiko huo mkulima anaweza kupata baina ya mikate 3-4 yenye kimo cha wastan ambayo inatosha kulisha ng’ombe wawili kwa siku nzima, bila kuongezea lishe nyingine.

Mara nyingi sio vyema kuhifadhi lishe zako katika sehemu yenye majimaji, kwa sababu maradhi ya vimelea vya fangasi yanaweza kuzuka na kuharibu ubora wa nyasi za brachiaria.

Anasema lishe za Feed blocks(mikate) haziwezi kufananishawa na aina nyingine ya lishe kwa sababu zimefanyiwa majaribio ya kimaabara na wakulima wana hakikisho kuwa zimepiku mifano ya hay.

“Wakulima wanaolengwa zaidi wakiwa ni wafugaji kutoka maeneo kame wanaopata changamoto kutafuta lishe wakati wa kiangazi kulisha mifugo wao,” akasema.

Alitaja maeneo kama Samburu, Marsabit ,Wajir , kajiado na Narok kama baadhi ya maeneo ambayo tayari yanaonekana kuja kufaidika na lishe hizi.

Aidha Ondabu alitoa tahadhari kwa wakulima wasitumie makapi ya mahindi kutengeneza lishe hii ,kwa sababu mahindi huwa yamebeba kiwango kikubwa cha sukari na ungaunga.

Nyasi za brachiaria zimeagizwa kutoka nchini Brazili lakini humu nchini zimepatiwa lakabu ya Maasai au Mombasa grass kutokana na kimo chake kirefu.

“Mkulima anaweza kuvuna tani 18 ya nyasi hizi kutoka katika kipande cha ardhi cha ekari moja, lakini akizikausha na kuzihifadhi kisha katengeneza hay uzito hupungua hadi tani 10,”akasema.

You can share this post!

AKILIMALI: Kukuza nyanya kwa mvungulio kuna faida tele

China ilivyomfunga Uhuru mdomo

adminleo